Hafsa Golo
na Habiba Zarali
LICHA ya Rais
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein,
kuwataka wafanyabiashara kupunguza bei za bidhaa katika mwezi mtukufu wa
Ramadhan, wafanyabiashara wamepuuza agizo hilo .
Uchunguzi
uliofanywa na gazaeti hili umebaina bei za bidhaa zinazotumiwa na Waislamu kwa
ajili ya futari, zimepanda mara dufu katika masoko yote makuu Unguja na Pemba .
Katika soko
kuu la Mombasa, bei ya ndizi mbichi, magimbi, viazi vikuu, ndizi mbivu
zimepanda karibu kwa asilimia 30.
Katika soko hilo ndizi mbichi aina ya
mkono wa tembo inauzwa baina ya shilingi 30,000 hadi 50 na kidole kimoja
kinauzwa baina ya shilingi 3,000 na 5,000 wakati fungu la viazi vitamu linauzwa
shilingi 2000 na 5,000.
Muhogo ambao
uliozoeleka kuuzwa shilingi 1,000 kwa fungu moja, bei imebakia pale pale lakini
wafanyabiashara wamepunguza ukubwa wa fungu.
Nazi
zimepata bei ya kutisha kutoka shilingi 5000 hadi shilini 18,000 huku samaki
wamekuwa adimu na hao wanaopatikana wanauzwa kwa bei kubwa hadi shilingi 10,000
kwa kipande.
Hata hivyo,
bei ya nyama imebakia baina ya shilingi 8000 na 9000 kwa kilo moja.
Wakizungumzia
hali hiyo baadhi ya wafanyabiashara walisema wanalazimika kupandisha bei
kutokana na wakulima kupandisha bei huku bidhaa zikiwa pungufu masokoni.
Mmoja ya wauza
ndizi, Kihange Haji Juma, alisema wanalazimika kuuza bei ya juu kwa sababu
ndizi zimekuwa adimu na hizo zinazopatikana wanauziwa bei kubwa.
Nae
mfanyabiashara wa nazi, Abdi Mohammed, alisema nazi zimekuwa adimu na kwa jumla
wananunua kati ya shilingi 1200 na 1600 kwa nazi moja.
Katika
masoko ya Mwanakwerekwe na Darajani, hali ni mbaya zaidi hali iliyosababisha
wananchi wengi kumiminika katika soko la Mombasa .
Kisiwani
Pemba, pia hali sio nzuri kutokana na bidhaa nyingi kupanda bei na kusababisha
wananchi kulalamika.
Katika soko
kuu la Qatar, ndizi mbichi zinauzwa hadi shilingi 20,000 na kusababisha
Waislamu wengi kukimbilia futari za nafaka.
Hassan Kombo
(45), mkaazi wa Chake Chake, alisema wafanyabiashara wengi huweka mbele tamaa
ya pesa ifikapo mwezi wa Ramadhani, bila ya kuzingatia hali za maisha ya wananchi
ambao wengi wao ni maskini.
“Hali
inatisha, wafanyabiashara hawana hata huruma, tunashindwa kununua bidhaa za
shambani na tunakimbilia nafaka,” alisema.
Bibi Zuhura
Khamis (33), mkaazi wa Wesha, alisema imekuwa kawaida kwa wafanyabiashara
kuongeza bei ifikapo mwezi wa Ramadhani licha ya serikali kuwataka kupunguza
bei.
Amour Juma
(49), mkaazi wa Chake Chake, alisema mwezi wa Ramadhani si wa kufanyia uchumi,
bali ni wa kusaidiana lakini wafanyabiashara wanashindwa kufahamu hilo .
Kwa upande
wao wafanyabiashara kisiwani humo, walisema kupanda bei kwa vyakula katika
mwezi wa Ramadhani kunatokana na kupanda ushuru.
No comments:
Post a Comment