Na Mwanajuma Mmanga
MTU mmoja mkaazi wa Migombani
alietambuliwa kwa jina la Said Mohammed Said (45), ameuawa kwa kuchomwa kisu cha
ubavu.
Mauaji hayo
yametokea mtaa wa Kaburi Kikombe wilaya ya magharibi Unguja Agosti tano mwaka
huu.
Mtuhumiwa wa mauaji
hayo ametajwa kuwa ni Haji Maliki (40) ambae ni askari polisi anaefanya kazi
kituo cha polisi Fuoni.
Kamanda wa Polisi Mkoa
wa Mjini Magharibi, Mkadam Khamis Mkadam, alisema mauaji hayo yalitokea saa
8:00 mchana wakati askari huyo alipofika nyumbani kwao marehemu kwa lengo la
kuonana na mpenzi wake.
Alisema baada ya
familia ya marehemu kumzuia mtuhumiwa kumuona mpenzi wake na kumtaka asiende
nyumbani hapo kutokana na tabia zake mbaya, ndipo alipoamua kufanya mauaji
hayo.
Alieuliwa ni shemeji
wa mpenzi wa askari huyo ambae alifika nyumbani hapo kwa lengo la kumuona mama
mkwe wake.
“Baada ya kuzuiwa
mtuhumiwa alitoa kisu kidogo kilichokuwemo mfukoni kwake na kuanza kumchinja
marehemu mikononi na baadae kumchoma kisu cha kifua upande wa kushoto na
kusababisha kifo chake,” alisema.
Alisema baada ya
mauaji hayo mtuhumiwa alikimbilia kituo cha polisi Mwanakwerekwe kwa
kujisalimisha.
Alisema mtuhumiwa
atafikifishwa mahakamani baada ya ushahidi kukamilika kujibu shitaka la mauaji.
No comments:
Post a Comment