Habari za Punde

Maalim- Awataka Wawekezaji na Wafanyabiashara Kutumia Fursa katika Uwekezaji Afrika. Mashariki

Na Khamis Haji, Istanbul                                    
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad amesema hali ya amani na utulivu katika eneo la Afrika Mashariki ni ya kuridhisha na wawekezaji vitegauchumi pamoja na wafanyabiashara wanaotaka kutumia fursa zilizopo katika eneo hilo waje na waondowe hofu.

Maalim Seif ameyasema hayo katika mkutano wa Uchumi wa Dunia (WEF) unaoendelea katika jiji la Istanbul nchini Uturuki alipotakiwa kutoa maoni yake juu ya hali ya usalama katika eneo hilo la Afrika Mashariki.

Amesema iliwahi kujitokeza hali ya kukithiri vitendo vya kiharamia vilivyo sababishwa na kukosekana utulivu katika nchi ya Somalia, lakini matukio hayo hivi sasa yamepungua kwa kiasi kikubwa kutokana na mashirikiano ya pamoja kati ya nchi zilizopo jirani pamoja na Jumuiya ya Kimataifa.

Amesema nguvu hizo za jumuiya ya kimataifa zinapaswa kuendelezwa, ikiwemo kuzijengea uwezo nchi za Afrika katika kukuza upatikanaji wa ajira kwa vijana, ili kuwaepusha na uwezekano wa kushawishiwa na makundi ya watu waovu ambayo yamekuwa chanzo cha kuongezeka matendo maovu.

“Hali katika eneo la Afrika Mashariki ni salama sana kuna vivutio vya kila aina,  wawekezaji tumieni fursa hii kuja kufungua miradi yenu”, amesema Maalim Seif.
Amesema ni jukumu la Jumuiya ya Kimataifa kuzipa msukumo nchi zenye matatizo ya uchumi, likiwemo tatizo kubwa la uhaba wa ajira miongoni mwa vijana, ambalo litawaepusha vijana  na tabia ya kurubuniwa kuingia katika matendo yasiofaa.


Waziri Mkuu wa Mali, Moussa Mara akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo, amesema mataifa yakiungana kupiga vita matendo ya ugaidi yanayojitokeza katika maeneo tafauti Duniani yanaweza kudhibitiwa.

“Mataifa yana wajibu wa kuungana na kukusanya nguvu kupiga vita matendo ya kigaidi ambayo hayajui mipaka”, amesema.

Amesema mkutano huo wa Dunia wa masuala ya Uchumi uwe ni hatua ya kufungua ukurasa mpya katika kukabiliana na matendo ya ugaidi ambayo licha ya kutoa mchango mkubwa katika kurejesha nyuma maendeleo ya kiuchumi, lakini pia husababisha maafa makubwa kwa jamii zote.

“Ugaidi Duniani hivi sasa ni kama maradhi ya Saratani, njia pekee ya kuweza kuyatibu ni mataifa kushirikiana katika kuandaa mikakati ya pamoja kuyakomesha”alishauri.

Baadhi ya wajumbe katika mkutano huo wamesema changamoto zilizopo katika eneo la Afrika chini ya Jangwa la Sahara zimekuwa zikichangiwa kwa kiasi kikubwa na hali ya mapigano, kukiukwa kwa haki za bianaadamu na kukosekana utawala wa kisheria katika baadhi ya maeneo.

Hata hivyo, walisema kumekuwa na mafanikio makubwa katika kuleta mabadiliko ya kiuchumi na kijamii katika eneo hilo kutokana na juhudi kubwa zinazoendeela kuchukuliwa na mataifa ya eneo hilo.

Mkutano huo ulifunguliwa na Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan, ukibeba ajenda kuu ya kuwepo matumizi mazuri ya rasilimali kwa maendeleo ya mataifa na kuweka hali ya usalama.

Katika hotuba hiyoya  Rais Erdogan, ametoa wito kwa Jumuiya ya Kimataifa kushirikiana na nchi yake katika kuleta demokrasia, Utawala Bora na amani ya kudumu katika nchi zilizopo jirani na Uturuki, zikiwemo Irak na Syria.

Amesema migogoro inayojitokeza katika nchi hizo imekuwa chanzo kikuu cha matendo ya kigaidi, pamoja na kuibua madhara makubwa kwa nchi yake yanayotokana na wimbi la wakimbizi wanaokimbia machafuko katika nchi zilizopo jirani na Uturuki.

Amesema hadi sasa kuna wakimbizi wapatao milioni 1.5 wanaohifadhiwa katika nchi yake na kuilazimisha nchi hiyo kuwa na mikakati mikubwa ya kuweka ulinzi katika mpaka wake na nchi jirani zenye mizozo.      

   

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.