Habari za Punde

Muinjilisti auawa akimuombea mgonjwa

Na Rose Chapewa, Mbeya
WATU watatu wamefariki dunia mkoani Mbeya katika matukio tofauti akiwemo Mwinjilisti wa Kanisa la Baptist kufariki baada ya kupigwa mchi wa kutwangia kichwani,wakati akimuombea mgonjwa wa akili  huku mwingine akifariki baada ya kuchomwa mkuki na mtoto wake wa kambo, na mwingine akiuwawa kwa deni la shilingi 500.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi mkoa huo, Ahmed Msangi, mwinjilisti huyo alitambuliwa kwa jina la Ambumbulwise Mwasomola (35) mkazi wa kijiji cha Lukasia tarafa ya Busokelo wilaya ya Rungwe.

Alisema tukio hilo lilitolea  Septemba 27 saa 5:30 usiku ambapo alipigwa na  mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la  Swalapo Mwaisanila  (56) mkazi wa kijiji cha Lwangwa anayedaiwa kuwa ni mgonjwa wa akili.

Alisema chanzo cha tukio hilo kilisababishwa na marehemu kutaka kumuombea mtuhumiwa huyo, baada ya kusumbuliwa na ugonjwa wa akili muda mrefu na hivyo kuinuka na kumpiga na mchi kichwani.

Akizungumzia tukio la pili, alisema mtu mmoja aliyefehamika kwa jina moja na Kabote (41) mkazi wa kijiji cha Mwanavala wilayani Mbalali, alifariki dunia baada ya kuchomwa mkuki sehemu mbalimbali za mwili wake na mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Nyamaniengo Kinanga ambaye ni mmiliki wa klabu cha pombe za kienyeji.

Tukio hilo lilitokea Septemba 28 saa 5 usiku Mwanavala tarafa ya Rujewa ambapo inadaiwa mauaji hayo yalitokea baada ya marehemu huyo kushindwa kulipa deni la shilingi 500 alilokuwa akidaiwa mara baada ya kunywa pombe kilabuni hapo.


Kutokana na tukio hilo watu 13 waliokuwepo eneo la tukio wanashikiliwa na polisi kwa mahojiano.

Na mtu mmoja aliyefahmika kwa jina la Richard Nelson Fwambo  (50) mkazi wa kijiji cha Utambalila wilaya ya Mbalali alifariki dunia baada ya kukatwa katwa na kitu chenye ncha kali  sehemu za kikichwani na Khamis Mgala (32) mkazi wa Mlowo Mbozi  ambaye ni mtoto wake wa kambo.

Tukio hilo lilitokea Septemba 28 mwaka huu saa 7 usiku katika kitongoji cha Magamba wilayani Mbozi, ambapo inadaiwa mtuhumiwa kabla ya kutenda kosa hilo alivunja mlango kisha kuingia ndani na kuanza kumshambulia marehemu.

Ilidaiwa mtuhumiwa alianza kumshambulia marehemu ndani kwake akiwa amelala na mke wake aliyefahamikwa kwa jina la Yustina Kashapamba (40) maarufu kwa jina la Nakamanga   ambaye ni mama mzazi wa mtuhumiwa.


Alisema chanzo cha tukio hilo,mtuhumiwa alikuwa hapendi mama yake aishi na marehemu ambaye ni baba yake wa kambo, baada ya baba yake mzazi kufariki, na kwamba mtuhumiwa baada ya kufanya mauaji hayo alikimbia na kutokomea kusikojulikana na anatafutwa na jeshi la polisi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.