Na Mariam Cyprian, Tanga
MTU mmoja asiyefahamika jina
wala mahala anapoishi anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 35 amefariki dunia na
mwili wake kusokomezwa kwenye kalavati la daraja na baadhi ya viungo vyake
yaani kichwa na sehemu za siri vimeondolewa.
Tukio hilo limetokea wilayani
Lushoto mkoani Tanga.
Akithibitisha Kamanda wa polisi
mkoa wa Tanga, Fresser Kashai, alisema tukio hilo lilitokea juzi katika kijiji
cha Katurupesa Kwemkwazu, majira ya saa 8:00 usiku ambapo uligundulika mwili wa
mwanamme asiyefahamika jina wala mahali anapoishi akiwa ametupwa katika
kalavati hilo.
Alisema chanzo cha tukio hilo
bado hakijafahamika na jeshi la polisi kwa kushirikiana na wanachi wa eneo hilo
wanaendelea na uchunguzi kubaini viungo vya mtu huyo vimepelekwa wapi.
Alisema mwili wa marehemu
umezikwa na wananchi wa kijiji hicho baada ya kufanyiwa uchunguzi na madaktari wilayani
humo, ambapo mpaka sasa watuhumiwa kuhusiana na tukio hilo bado hawajakamatwa.
Katika tukio jingine mtu mmoja
aliyefahamika kwa jina la Amiri Bakari (65) mkazi wa kijiji cha Komkonga kata
ya Mkata wilayani Handeni amefariki dunia baada ya pikipiki waliyokuwa
wakiitumia wakati wakienda kuwinda wanyama pori kuanguka baada ya kushindwa
kupanda mlima.
Akitoa taarifa ya hali ya
uhalifu mkoa wa Tanga, Kamanda Kashai, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo
ambapo alisema lilitokea Septemba 27 mwaka huu majira ya saa 4:00 za asubuhi.
Alisema mtu huyo alikuwa na
mwenzake katika pikipiki wakielekea porini kuwinda huku kila mmoja akiwa
amebeba silaha yake aina ya gobole na ndipo walipofika kilima cha Lugala
pikipiki yao ilishindwa kupanda mlima huo na kuanza kurudi nyuma na kuanguka.
Alisema katika tukio hilo
silaha aliyokuwa ameibeba dereva wa pikipiki hiyo ayefahamika kwa jina la Kiduo
Rajabu (35) ilifyatuka na kwa kuwa ilikuwa na baruti gololi ilimjeruhi abiria
huyo ubavu wake wa kushoto na kusababisha kifo chake.
Alisema mtuhumiwa katika tukio hilo amekamatwa
na upelelezi kuhusiana na tukio hilo.
No comments:
Post a Comment