Na Mwandishi wetu
Waziri Ujenzi, Ardhi, Makazi
Maji na Nishati, Mhe. Ramadhan Abdalla Shaaban, amesema watu waliopewa nyumba
za maendeleo na Rais wa Kwanza wa Zanzibar, marehemu Abeid Amani Karume, katika
maeneo mbali mbali Unguja na Pemba, hawatahamishwa, lakini watakapofariki
familia zao zitalazimika kuzilipia kodi.
Akitoa ufafanuzi kuhusu mswada
wa sheria ya kuanzisha Shirika la Nyumba katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi
jana, alisema familia hizo zitapewa mikataba ya kuzilipia nyumba hizo.
Aidha alisema, wale ambao
walivunjiwa nyumba zao kupisha ujenzi wa nyumba hizo wakati wa utawala wa
serikali ya awamu ya kwanza na kulipwa fidia hawataguswa badala yake wapewa
hati za kumiliki nyumba hizo kwa sababu ni zao.
Mapema Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Mhe.
Mwadini Makame, alisema lengo la kuanzishwa shirika hilo ni kuhakikisha
wananchi wanapata makaazi bora.
Hata hivyo, Wawakilishi
waliitaka wizara hiyo kuhakikisha shirika hilo linawezeshwa ili kuondoa uwezekano
wa kufanya kama ilivyotokea kwa mashirika mengine.
Wajumbe wa Baraza hilo
waliupitisha mswada huo kuwa sheria na sasa unasubiri kusainiwa na rais ili
kuanza kutumika.
No comments:
Post a Comment