Habari za Punde

Kutoka baraza la Wawakilishi: Hakuna vipimo vya kitaalamu na vya kisasa kugundua bidhaa feki


Na Abdulla Ali Maelezo- Zanzibar                                 21/01/2015

 

Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko Mhe. Nassor Ahmed Mazrui amesema kutokuwepo kwa mashine za kisasa za kupimia bidhaa ndiko kunakopelekea kukosekana kwa vipimo vya kisasa, vya kitaalamu na vya uhakika vya bidhaa hizo na kupelekea uingizwaji wa bidhaa feki.

 

Hayo ameyaeleza katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani Zanzibar wakati akijibu swali la Mwakilishi wa Jimbo la Kwahani Mhe. Ali Salum Haji. 

 

Waziri Mazrui ametanabahisha kuwa kutokana na ukosefu wa vifaa hivyo ikiwemo mashine ya ICP kunafanya baaadhi ya bidhaa kushindwa kufanyiwa vipimo wakati zinapoingizwa nchini na kusababisha hasara na madhara makubwa kwa watumiaji wa bidhaa hizo kwani nyingi zao huwa ni feki. 

 

Waziri Mazrui amesema kutokana na ukuaji wa biashara nchini kumejitokeza baadhi ya wafanyabiashara ambao huingiza bidhaa feki za kulainisha vyombo vya moto kama vile Girisi na Oil pamoja na vyakula vilivyokwisha muda wake.

 

“Kwanza naomba kukiri kuwa kwa hivi sasa Wizara yangu haina utaratibu wa kukagua bidhaa za vilainisho ingawa nakubaliana na mjumbe kuwa hii ni mojawapo ya bidhaa au huduma nyengine zinazopaswa kusimamiwa”, alieleza Waziri Mazrui.

 

Aidha Waziri Mazrui amewaomba viongozi na Wajumbe wa Baraza hilo kushirikiana na taasisi nyengine za serikali kuangalia mfumo bora wa kusimamia biashara hizo ambazo kwa sasa hazina mfumo mzuri wa kuzisimamia sambamba na kuwataka wananchi kutoa taarifa kwa Wizara yake pale ambapo wanagundua uingizwaji au uuuzwaji wa bidhaa feki madukani.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.