Habari za Punde

JWTZ wajaribu kumkomboa mwanajeshi aliefungwa. Ni mtoto wa muasisi wa Mapinduzi Z’bar

Na Khamis Amani
Baada ya kuhukumiwa kutumikia gerezani kwa muda wa siku 15  kila mmoja kwa watoto sita wa muasisi wa Mapinduzi ya Zanzibar, marehemu Khamis Daruweshi, askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) jana walifika Mahakama Kuu Vuga, kuomba mmoja ya wafungwa hao ambae ni mtumishi wa jeshi, aruhusiwe akatumikie adhabu mahabusu ya jeshi.

Zanzibar Leo iliwashuhudia askari wa jeshi hilo zaidi ya 10, wakiingia mahakamani na kufanya mazungumzo na Mrajisi wa mahakama, George Kazi, ambae ndie alietoa adhabu hiyo.

Mtumishi huyo wa jeshi aliehukumiwa kifungo kwa kosa la kudharau amri ya mahakama pamoja na wenzake watano ni Darwesh Khamish Darwesh.

Juzi Mrajisi huyo ambae pia ni Hakimu wa mahakama ya Mkoa, aliwatia hatiani watoto hao sita wa familia moja kutumikia Chuo cha Mafunzo kwa muda wa siku 15 kila mmoja kwa kosa la kudharau amri halali ya mahakama.

Wadaiwa wengine katika shauri hilo ni Shaabani, Said, Asia, Atinji pamoja na Atika ambao wote hao ni watoto wa marehemu Khamis Darwesh, ambao inadaiwa walikataa amri halali ya mahakama ya kutakiwa kuhama katika nyumba yao inayobishaniwa baada ya mahakama kutoa maamuzi ya kuuzwa.


Hata hivyo, Mrajisi huyo aliwakatalia wanajeshi hao kumchukua mwanajeshi mwenzao kwenda kutumikia adhabu jeshini, akisema uamuzi huo umefanywa kwa mujibu wa sheria.

Aidha aliwambia  wanajeshi hao kuwa wana nafasi ya kuwasilisha ombi la mapitio ya shauri hilo mahakama kuu ili liweze kusikilizwa.

Baada ya kauli hiyo, wanajeshi hao waliondoka katika maeneo ya mahakama.

Habari za uhakika zilizopatikana baadae jana zinasema baada ya zoezi la kumuomba Mrajisi kumuachia mwanajeshi huyo, askari wengine wawili wa JWTZ walifika ofisini kwa Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu, kwa kile kilichoelezwa kutafuta njia ya kumnasua mwanajeshi mwenzao.

Mwanajeshi huyo na wenzake walikumbwa na mkasa huo baada ya kushindwa kuielezea mahakama sababu iliyowafanya washindwe kuhama ndani ya nyumba iliyoachwa na marehemu baba yao Khamis Darwesh iliyouzwa kwa amri ya mahakama.

Nyumba hiyo iliyopo Kilimani Kiungani plot namba 15, 17 na 18 iliuzwa na kampuni ya mnada ya Kumekucha kwa idhini ya mahakama baada ya kufunguliwa kesi ya madai iliyohusisha familia ya marehemu.


Mara baada ya nyumba hiyo kuuzwa, kampuni ya Kumekucha iliwaandikia barua wakaazi wa nyumba hiyo kuhama ili akabidhiwe mmiliki halali  aliyeinunua lakini familia hiyo ilikataa wakidai nyumba hiyo marehemu baba yao ambao aliiweka wakfu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.