Habari za Punde

Kongamano la mahujaji watarajiwa

 Ustaadh Seif Shaaban akisoma Qur-an tukufu ikiwa ni ufunguzi wa kongamano lililoandaliwa na Umoja wa Taasisi za Hjja Zanzibar (UTAHIZA) lililowashirikisha mahujaji watarajiwa katika ukumbi  wa Beit al Yamin Malindi Mjini Zanzibar. (Picha na Makame Mshenga-Maelezo Zanzibar).
 Mwenyekiti wa Bodi ya Umoja wa Taasisi za Hijja Zanzibar  Sheikh Abdulhamid akifungua Kongamano la mahujaji watarajiwa katika ukumbi wa Beit al Yamin Malindi Zanzibar, kulia yake ni Mwenyekiti wa Umoja huo na kushoto Sheikh Othman Maalim.

 Ustaadh Khalid Mohammed Mrisho akiwasilisha mabadiliko ya taratibu mpya za Ibada ya Hijja katika kongamano la mahujaji watarajiwa lililofanyika Malindi Zanzibar.
 Baadhi ya mahujaji watarajiwa wakimsikiliza Sheikh Othman Maalim alipowasilisha mada ya umuhimu wa kutekeleza ibada ya hija na madhara ya kuchelewesha kutekeleza ibada hiyo katika kongamano liliofanyika Malindi Mjini Zanzibar.

Hujaji mtarajiwa Abass Imtiyaz akiuliza swali katika kongamano lililoandaliwa na Umoja wa Taasisi za Hijja Zanzibar katika ukumbi wa Beit al Yamin Malindi Zanzibar. 

Katibu wa UTAHIZA Ustaadh Ali Adam akitoa historia ya Umoja huo na kazi zake katika kongamano lililofanyika Malindi Zanzibar.

(Picha na Makame Mshenga-Maelezo Zanzibar).

Na Ramadhani Ali –Maelezo Zanzibar                 18.4.2015
Waislamu wa Zanzibar wanaotegemea kutekeleza Ibada ya Hijja mwaka huu wameshaurfiwa kukamilisha mipango ya safari hiyo mapema ili kuziwezesha Taasisi zinazosafirisha mahujaji kuweza kukamilisha taratibu mpya zilizowekwa na Serikali ya Saudi Arabia.

Akizungumza katika Kongamano la mahujaji watarajiwa lililofanyika  ukumbi wa Beit al Yamin Malindi, Afisa kutoaka Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana Ustaadh Khalid Mohammed Mrisho amesema Serikali ya Saudi Arabia imefanya mabadiliko makubwa ya taratibu za maandalizi ya Hijjah kuanzia mwaka huu.

Amesema wamefanya maamuzi hayo baada ya malalamiko yaliyokuwa yakitolewa na  mahujaji kutokana na vitendo vya udanganyifu  vilivyokuwa vikifanywa na baadhi ya Taasisi zinazosafirisha mahujaji kutoka mataifa mbali mbali duniani.

“Baadhi ya viongozi wa Taasisi zinazosafirisha mahujaji walikuwa wakiwatoza fedha mahujaji wao kwa ajili ya kulipia Viwanja vya ndege vya Makka na Madina lakini walikuwa hawalipi na mahujaji kuzuiliwa kwa saa kadhaa,”alisema Ustaadh Khalid.


Taasisi nyengine alisema zilikuwa zinawaahidi mahujaji kuwakodia nyumba nzuri za karibu  katika miji mitakatifu ya Makka na Madina lakini wanapofika huko huwekwa kwenye nyumba mbovu  na wengine hukosa huduma ya chakula.

Amesema katika kukabiliana na matatizo hayo Serikali ya Saudia Arabia kuanzia sasa imeziagiza Taasisi  zinazosafirisha mahujaji kufanya taratibu zote za maandalizi ya safari, makaazi na matembezi kwa njia ya mtandao na kulipa gharama zote wakiwa nchini mwao.

Amesema iwapo taratibu hizo hazikukamilika hujaji atakosa visa ya kuingia Saudi Arabia na atakuwa amekosa kutekeleza ibada ya Hijjah kwa mwaka huo.

Ameongeza kuwa  mwaka huu nchi hiyo imeweka hadi tarehe 27 Juni kuwa ni siku ya mwisho  kukamilisha taratibu za mahujaji na baada ya tarehe hiyo mtandao huo utakuwa umefungwa na itakuwa hakuna njia nyengine.

“Lengo la uwamuzi huo wa  Saudi Arabia  ni kuwaondoshea mahujaji usumbufu usio wa lazima  wakati wa kutekeleza  ibada hiyo,”alisisitiza Ustaadh Khalid.

Amewakumbusha mahujaji watarajiwa kuwa waangalifu na mizigo yao  wakati wa safari na wanapokuwa  nchini humo na watakaporejea kuchukua kiwango cha mizigo kinachokubalika kwenye ndege.

Akifungua Kongamano hilo lililoandaliwa na Umoja wa Taasisi za Hijja Zanzibar (UTAHIZA) Mwenyekiti wa Bodi Sheikh Khamis Abdulhamid amewasisitiza waislamu wenye uweze kutekeleza ibada ya hijja ili kukamilisha uislamua wao.
Mwaka huu Tanzania imepewa nafasi 3,000  kupeleka mahujaji nchini Saudi Arabia ambapo ibada hiyo hutekelezwa kila mwaka mwezi wa mfunguo tatu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.