Habari za Punde

CCM yataja sababu 7 kwanini Lowassa alikatwa kugombea Urais kupitia CCM 2015 (Taarifa hii imekanushwa na CCM)




TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Siku za hivi karibuni kumeibuka baadhi ya watu ambao wamekuwa kwa makusudi na kwa malengo maalum wakitunga na kujiandikia taarifa, za uongo, kujenga hofu na au kupotosha na kisha kuzisambaza kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii kwa malengo mahsusi dhidi ya Chama Cha Mapinduzi.

Watu hao katika nyakati tofauti wamekuwa wakitengeneza uzushi na uongo huo na kuusambaza kwenye mitandao pamoja na baadhi ya vyombo vya habari kwa lengo lisilo wazi.

Baadhi ya uzushi na uongo uliotungwa na kusambazwa na watu au kikundi hicho ni pamoja na hii ya leo inayoeleza mambo mbalimbali juu ya Ndugu Edward Lowasa na ambayo watunzi wake wameandika kuwa imetolewa na Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi Ndugu Nape Moses Nnauye.

Ifahamike kuwa uzushi huo na mwingine uliofanywa na watu au kikundi hicho umekusudia kujenga msukumo ambao haupo ili kuujengea umma hofu ya huruma dhidi yao ili kusukuma na kushinikiza agenda zao.

Jambo hilo ni uzushi mtupu kwa sababu kwanza Ndugu Nape na wajumbe wote wa Sekretarieti hawapo jijini Dar es Salaam badala yake wapo mikoani kushiriki katika zoezi la kura ya maoni kwa ajili ya uteuzi wa wagombea Udiwani na Ubunge zoezi ambalo litakamilika Agosti Mosi, 2015.

CCM inasisitiza kuwa habari hizo si za kweli, zimeandikwa na watu kwa malengo binafsi ya kugombanisha, kujenga chuki na uhasama baina ya Ndugu Nape, Chama, Wajumbe wa Sekretarieti na wananchi kwa ujumla bila sababu.

Viongozi, wana-CCM na wananchi kwa ujumla hawana budi kupuuza uzushi wowote ule unaotolewa na kusambazwa na watu au vikundi vya hovyo vinavyotumiwa na watu kwa maslahi binafsi, badala yake CCM itakuwa inatoa taarifa sahihi kwa wakati ili kutoruhusu uwepo au kuibuka kwa ombwe la mawasiliano baina ya umma na Chama.

Imetolewa na:-

Kitengo cha Mawasiliano na Umma
Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM
Lumumba, Dar es Salaam.
29/07/2015 

Kumradhi wadau wa ZanziNews, Baada ya kufuatilia kwa kina taarifa hii haikutolewa na CCM baada ya kusoma kanusho la CCM


Ndugu wananchama wa Chama cha Mapinduzi-CCM ni wiki mbili tangu tulipo maliza mchakato ndani ya chama kumpata mgombea wa Urais hapo Octoba 25, 2015. 

Kwa mara ya kwanza wananchama 41 waliomba kuteuliwa na chama. Hii inaonyesha kwamba demokrasia imekuwa ndani ya chama. Kati ya wanachama wa CCM waliochukua fomu alikuwa ni mheshimiwa waziri mkuu mstaafu Ndugu Edward Lowasa. 

Utaratibu wa chama ulifuatwa ili kumpata mgombea ikiwa ni pamoja kamati ya maadili, kamati kuu na halmashauri kuu ya taifa na mkutano mkuu. Katika mchakato pia chama kilitumia idara mbalimbali kama usalama wa taifa, takukuru na tume ya maadili ya umma kupata taarifa mbalimbali kuhusu wagombea hasa za uadirifu, usalama wan nchi na kadhalika.

Baada ya mchakato kumalizika baadhi ya wagombea na wanachama hawakuridhika na matokea, katika chama kikubwa kama CCM haizekani wanachama wote wakaridhika na maamzi. 

Ndugu wanachama na watanzania tunaomba kuelewa kuwa kumpata kiongozi mkubwa wa nchi kama Rais siyo kazi rahisi. Baadhi ya wanachama ambao hawakuridhika na maamzi ya chama ni Ndugu Edward Lowasa, amekuwa akizungumza nje ya chama kuhusu kutotendewa haki na baade kuhama chama na kujiunga na chamacha demokrasia na maendeleo-CHADEMA.

Kwa nini Ndugu Lowasa hakuteuliwa kuwa mgombea wa CCM?

Ndugu wanachama na watanzania, Mheshimiwa Lowasa alijenga hisia na kuamini kuwa ndani ya CCM wagombea wote walistahili kuenguliwa isipokuwa yeye. Hii siyo demokrasia, baada ya kupitia repoti mbalimbali Ndugu LOWASA alienguliwa kwa sababu zifuatazo:-


1. Kukiuka taratibu za chama kwaani alionekana kufanya kampeni badala ya kutafuta wadhamini
2. Kutoa rushwa kwa wanachama mbalimbali hivyo kukigawa chama na kama angepishwa kuwa mgombea CCM ilikuwa katika hatari ya kuwekewa pingamizi mahakamani lakini pia angeweka watu wake kwenye utawala kuwalipa fadhira.

3. Edward Lowasa aliwahonga wajumbe katika uchaguzi wa wajumbe NEC uliofanyika miaka iliyopita ili kupata watu wake ndani ya NEC.

4. Kuanza kampeni kabla ya wakati, alikuwa akisafirisha watu mbalimbali na kuwalipa fedha nyingi kisha kutoa taarifa kuwa walikuwa wakimtaka kugombea Urais, hii ni hadaa na hatari kwa chama.

5. Kuwa na kashfa nyingi za ufisadi na matumizi mabaya ya ofisi ya umma akiwa waziri.

6. Kusemwa semwa kuhusika kuhusika na tuhuma za kutumia watu kudhuru baadhi ya watanzania na viongozi, hili lipo kwenye vyombo vya dola kwa uchunguzi, uchunguzi ukikamilika sheria itachukua mkondo wake.

7. Utajiri na mali usiokuwa na maelezo alizipataje kama vile kumiliki majumba nje ya nchi kama uingereza, singapole na nk.

Mwisho chama kimesikitishwa sana na kauli kuwa amekuwa akionewa na kusingiziwa kuwa alihusika na kashfa ya RICHMOND, ndugu wanachama kashfa ya RICHMOND ilianzia bungeni, CCM haikuhusika na kumwondoa kwenye uwaziri mkuu, lakini kwa kuwa imekuwa inajengeka kuwa alionewa tunaviomba vyombo vya sheria kulipeleka jambo hili mahakamani ili kuondoa dhana inayojengeka kuwa serikalia ya CCM inaonea wanachama wake. Doa linalotakwa kujengeka litapatiwa ufumbuzi na iwapo inathibitika kulikuwa na njama binafsi wote waliohusika kulidanganya bunge watachukuliwa hatua na chama lakini pia sheria itachukua mkondo wake.

Imetolewa na :-
Nape M.Nnauye
KATIBU WA HALMASHAURI KUU YA TAIFA
ITIKADI NA UENEZI

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.