Habari za Punde

Dk Shein Ajumuika na Wananchi wa Wete Pemba katika Futari,

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Pemba                                                                                                                                  1.7.2015
---

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein jana aliungana pamoja na wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Pemba katika futari maalum aliyowaandalia, ikiwa ni miongoni mwa utamaduni anaouendeleza wa kufutari pamoja na wananchi wa Mikoa yote ya Zanzibar kila ufikapo mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Hafla hiyo ya futari ilifanyika katika viwanja vya Ikulu ndogo ya Wete na kuhudhuriwa na wananchi pamoja na viongozi mbali mbali wa Mkoa huo pamoja na baadhi ya viongozi wa Serikali.

Aidha, Mama Mwanamwema Shein naye aliungana pamoja na akina mama wenzake wa Mkoa huo katika futari hiyo ya pamoja.

Sheikh Majid Mohammed Abeid  kutoka Wete akitoa neno la shukurani kwa niaba ya wananchi hao waliofutarishwa na Alhaj Dk. Shein alitoa pongezi na shukurani kwa mwaliko huo wa Rais.

Katika shukurani hizo Sheikh Majid alitumia fursa hiyo kutoa pongezi na kwa mafanikio makubwa ya kimaendeleo yaliofikiwa katika Mkoa wao wa Kaskazini Pemba chini ya uongozi wa Alhaj  Dk. Shein.

Sheikh Majid alisema kuwa katika uongozi wa Dk. Shein wameshuhudia uimarishwaji na utekelezaaji wa miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo miundombinu ya barabara za kisasa katika Mkoa huo ambapo kabla ya hapo walikuwa wakipata usumbufu mkubwa wa usafiri wa barabara katika shughuli zao za kiuchumi na kijamiii.

Alisema kuwa mbali ya uimarishwaji wa miundombinu ya barabara katika Mkoa wao huo pia, juhudi kubwa zimefanywa chini ya uongozi wa Alhaj Dk. Shein katika usambazaji wa huduma ya maji safi na salama katika maeneo mbali mbali ya Mkoa huo.

Aidha, Sheikh Majid alitumia fursa hiyo kueleza mafanikio makubwa yaliopatikana katika kutatua migogoro kadhaa ya ardhi chini ya uongozi wa Dk. Shein pamoja na kupongeza mafanikio katika sekta nyengine za maendeleo na hata za kijamii.

Sambamba na hayo, Sheikh Majid hakuchelea kutoa pongezi zake kwa niaba ya wananchi hao wa Mkoa wa Kaskazini Pemba kwa mafanikio makubwa yaliopatikana katika kuendeleza amani na utulivu chini ya uongozi wa Dk. Shein huku akisisitiza haja ya kudumishwa na kuendeleza kwa manufaa ya Wazanzibari wote.

Sheikh Majid alitumia fursa hiyo kutoa ombi kwa Alhaj Dk. Shein la kujengewa Bandari yao ya Wete hatua ambayo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imo katika mchakato wa ujenzi wa Bandari hiyo sambamba na ukarati wa Bandari iliyopo hivi sasa.


Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.