STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Pemba
1.7.2015
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein jana aliungana pamoja na wananchi wa Mkoa
wa Kaskazini Pemba katika futari maalum aliyowaandalia, ikiwa ni miongoni mwa
utamaduni anaouendeleza wa kufutari pamoja na wananchi wa Mikoa yote ya
Zanzibar kila ufikapo mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Hafla hiyo ya
futari ilifanyika katika viwanja vya Ikulu ndogo ya Wete na kuhudhuriwa na
wananchi pamoja na viongozi mbali mbali wa Mkoa huo pamoja na baadhi ya
viongozi wa Serikali.
Aidha, Mama
Mwanamwema Shein naye aliungana pamoja na akina mama wenzake wa Mkoa huo katika
futari hiyo ya pamoja.
Sheikh Majid
Mohammed Abeid kutoka Wete akitoa neno
la shukurani kwa niaba ya wananchi hao waliofutarishwa na Alhaj Dk. Shein
alitoa pongezi na shukurani kwa mwaliko huo wa Rais.
Katika shukurani
hizo Sheikh Majid alitumia fursa hiyo kutoa pongezi na kwa mafanikio makubwa ya
kimaendeleo yaliofikiwa katika Mkoa wao wa Kaskazini Pemba chini ya uongozi wa
Alhaj Dk. Shein.
Sheikh Majid
alisema kuwa katika uongozi wa Dk. Shein wameshuhudia uimarishwaji na utekelezaaji
wa miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo miundombinu ya barabara za kisasa
katika Mkoa huo ambapo kabla ya hapo walikuwa wakipata usumbufu mkubwa wa
usafiri wa barabara katika shughuli zao za kiuchumi na kijamiii.
Alisema kuwa
mbali ya uimarishwaji wa miundombinu ya barabara katika Mkoa wao huo pia,
juhudi kubwa zimefanywa chini ya uongozi wa Alhaj Dk. Shein katika usambazaji
wa huduma ya maji safi na salama katika maeneo mbali mbali ya Mkoa huo.
Aidha, Sheikh
Majid alitumia fursa hiyo kueleza mafanikio makubwa yaliopatikana katika
kutatua migogoro kadhaa ya ardhi chini ya uongozi wa Dk. Shein pamoja na
kupongeza mafanikio katika sekta nyengine za maendeleo na hata za kijamii.
Sambamba na hayo,
Sheikh Majid hakuchelea kutoa pongezi zake kwa niaba ya wananchi hao wa Mkoa wa
Kaskazini Pemba kwa mafanikio makubwa yaliopatikana katika kuendeleza amani na
utulivu chini ya uongozi wa Dk. Shein huku akisisitiza haja ya kudumishwa na
kuendeleza kwa manufaa ya Wazanzibari wote.
Sheikh Majid
alitumia fursa hiyo kutoa ombi kwa Alhaj Dk. Shein la kujengewa Bandari yao ya
Wete hatua ambayo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imo katika mchakato wa
ujenzi wa Bandari hiyo sambamba na ukarati wa Bandari iliyopo hivi sasa.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment