Habari za Punde

Jeshi la Polisi lanolewa juu ya haki za binadamu kipindi cha uchaguzi



Jaji Mstaafu Thomas Mihayo alipokuwa akitoa Mada katika Semina ya Siku mbili kwa Maafisa wa Jeshi la Polisi iliyoandaliwa na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu nchini ili kulijengea uwezo Jeshi la Polisi katika kulinda haki za binadamu kipindi cha uchaguzi. Semina hiyo imefanyika  huko Ukumbi wa Hotel ya Grand mjini Zanzibar.

Na Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar    29/07/2015


Jeshi la Polisi nchini limeshauriwa kuzisoma kwa kina na kuzielewa vyema Sheria na kanuni za Uchaguzi kabla ya kuzitekeleza.

Kufanya hivyo kutalipelekea Jeshi hilo kuepuka lawama na kufanya wajibu wao kikamilifu ili kuufanya Uchaguzi unaokuja uwe katika hali ya uhuru, haki na amani.

Wito huo umetolewa na Jaji Mstaafu Thomas Mihayo alipokuwa akitoa Mada katika Warsha ya Siku mbili kwa Maafisa wa Jeshi la Polisi iliyoandaliwa na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu nchini huko Ukumbi wa Hotel ya Grand mjini Zanzibar.

Amesema Jeshi hilo linawajibu wa kuhakikisha Sheria za nchi zinafuatwa lakini jambo la msingi ni kuzielewa Sheria hizo kabla ya kuzitekeleza.


Jaji Mihayo amesema inashangaza kuona kuwa Tanzania inaelekea katika kipindi cha uchaguzi Mkuu wakati Maafisa na Makamanda hawazielewi vyema Sheria na kanuni za Uchaguzi unaokuja.

Hivyo amewaomba Maafisa Wawaelimishe Makamanda wenzao juu ya Sheria na kanuni za uchaguzi ili wakati utakapofika watende haki na Wajibu wao bila ya upendeleo.

“Polisi kazi yenu nikuhakikisha Sheria zinafuatwa lakini zitafutwa vipi wakati wenyewe hamzijui..Jambo la msingu ni kuzisoma na kuzielewa kwanza ndio mufanye juhudi za kutekelezwa” alisema Mihayo.

Amefahamisha kuwa Jeshi hilo linapaswa kufuata Sheria za nchi bila kufuata matakwa ya Watawala na kwamba Watawala hao watabadilika kulingana na uchaguzi lakini Wananchi wataendelea kuwepo.

“Jeshi la Pilisi linawajibika kwa Wananchi na si Viongozi wa Serikali hivyo nakuombeni mzijue Sheria na muwe wakwanza kuzitekeleza” Alishauri Jaji Mihayo.

Kwa upande wake Kamishna wa Jeshi la Polisi Zanzibar Hamdan Makame ameshukuru Mtandao wa Watetezi wa haki za Binadamu kwa kuendesha Semina hiyo katika kipindi muafaka cha harakati za uchaguzi mkuu.

Amesema kila mtu ni mlinzi wa haki za binadamu katika kila sehemu anayofanyia kazi nakwamba jambo muhimu ni kuhakikisha Haki zinalindwa hasa ikizingatiwa kuwa suala la haki za binadamu ni lakimataifa.

Kwa upande wake Makamu mwenyekiti wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu nchini Harusi Mpatani ameliomba Jeshi hilo kuhakikisha linawalinda Wananchi wote ikiwemo Watetezi wa haki za binadamu.

Semina hiyo ya siku mbili iliyoandaliwa na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu nchini ni mwendelezo wa kulijengea uwezo Jeshi la Polisi katika kulinda haki za binadamu ili kuufanya uchaguzi unaokuja uwe huru,haki na Salama.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.