Habari za Punde

Dk Shein azindua miradi ya Umeme katika visiwa vya kisiwa Panza na Makoongwe


  
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Pemba                                                                   20.9.2015
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein leo amefungua miradi miwili mikubwa ya umeme katika visiwa vya Makongwe na Kisiwa Panza huko Pemba na kusema kuwa hizo ni juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuhakikisha huduma zote muhimu ikiwemo ya umeme zinawafikia wananchi popote pale walipo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo kwa nyakati tofauti katika uzinduzi wa mradi wa usambazaji wa umeme katika visiwa vya Makongwe pamoja na Kisiwa Panza vyote viliyopo Mkoa wa Kusini Pemba.

 Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Wizara, Bwana Shafi Haji Mussa,  ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya ZECO, Mkurugenzi na wafanyakazi wote wa ZECO pamoja na wafanyakazi wote wa Shirika hilo.

Akiwa Kisiwa Panza Dk. Shein alisema kuwa wapo walioamini na wapo wasioamini kama umeme umefika, aliwakumbusha kuwa hiyo ni ahadi yake aliyoitoa mwaka 2010 wakati wa Kampeni za uchaguzi Chanjani Chokocho katika uwanja wa Black Wizard ambapo aliahidi kuufikisha umeme kisiwa Panza na Makongwe.


Alisema kuwa shughuli hiyo imepangwa kwa muda mrefu, umeme umezinduliwa tayari na alisema kuwa amekuwa akifuatilia hatua kwa hatua huku akisisitiza kuwa kazi ya kuleta maendeleo imefanywa pamoja waliokuwemo serikalini pamoja na wananchi na hakuna atakaejisifu kuwa kafanya peke yake.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa ipo siku barabara ya kisiwa Panza itatengezwa kwa kiwango kinachohitajika kutoka Mtondooni hadi Panza nayo itajengwa na kuwa ya kileo hukua akisema kuwa kufikishwa umeme Kisiwapanza ni jitihada za watu wote na matokeo yake yanaonekana hivileo.

Alisisitiza kuwa tayari huduma zote muhimu zimeshafika katika visiwa hivyo zikiwemo huduma za umeme,maji, afya skuli pamoja na huduma nyengine muhimu.

Alisisitiza kuwa ipo haja ya kuwepo Gati ndogo, ili wananchi wa sehemu hiyo waweze  kusafiri bila ya usumbufu na kueleza kuwa bado ana nia ya kutafuta utaratibu mzuri zaidi wa uvukaji vizuri ili watu wa KiswaPanza wasafiri kutoka Chokocho hadi KisiwaPanza."....muda ukifika nitakuja kulieleza vizuri suala hili",alisema Dk. Shein.

Alisema kuwa Biashara mbali mbali zinazotegemea umeme zitashamiri sana katika visiwa hivyo na kuwataka wananchi hao wafanye hivyo huku akiwahakikishia huduma hiyo itabadilisha maisha yao.

Alieleza kuwa maisha ya mwanaadamu hubadilika mara baada ya kupatikana kwa umeme na kusisitiza kuwa Serikali  ina mipango mengi iliyojiwekea katika upatikanaji wa huduma hiyo huku akiwaeleza hatua zinazoendelea za mabadiliko ya mitambo ya umeme hivi sasa nchini kote na aliwataka wasitaharudki na hilo.

Akieleza haja ya kutunzwa kwa miundombinu ya umeme Kisiwani humo alisema kuwa ni pamoja na kutojenga karibu na nguzo, kutochimba mchanga chini ya nguzo hizo hata vibanda vya mazungumzo na kuwataka kila mmoja awe mlinzi. "....itunzwe ili tuweze Kuitumia sisi, watoto wetu, wajukuu wetu, vitukuu vyetu..", alisema Dk. Shein.

Dk. Shein alisema kuwa Serikali imo katika jitihada za kutafuta umeme mbadala hapa Zanzibar kwani uliopo unanunuliwa kutoka Tanzania Bara kwa fedha nyingi na kuwataka wananchi kulipia huduma hiyo kwa ajili ya kuepuka usumbufu hapo baadae sambamba na Serikali kupata fedha za kuulipia.

Serikali inafanya taratibu za kutendeza umeme kwa taka, upepo, gesi au mawimbi ya bahari na hivi sasa wataalamu wamo katika utafiti na baada ya muda si mrefu watatoa jibu. Aidha, alisema kuwa hatua hiyo inakuja kutokana na kukua kwa shughuli za maendeleo Unguja na Pemba zitakazohitajia huduma zaidi za umeme.

Alisema kuwa Shirika aliliagiza aliliagiza Shirika la Umeme na kulielekeza kuwa wale waliokuwa hawana fedha wapatiliwe umeme na watakuwa wanalipa kidogo kidogo deni hilo na kupongeza kutokana na kuendeleza utaratibu huo.

Akiwa katika kisiwa cha Makongwe Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza kuwa matukio hayo ni ahadi alizozitoa kwa visiwa vya Makongwe na Kisiwa Panza kufikisha umeme ndani ya miaka mitano ya uongozi wake na kuahidi kisiwa cha Shamiani, baada ya muda si mrefu nao watapata huduma hiyo.

Alisema kuwa umeme utawasaidia kuimarisha shughuli zao za  maendeleo zikiwemo kilimo, ufugaji, uvuvi, kutumia mashine za kusagia, mafriji, kuwa na vyombo vya habari vitakavyowasaidia kupata habari mbali mbali za ndani na nje ya nchi yao.

Dk. Shein alisema kuwa ahadi ya kuleta umeme katika visiwa vidogo vidogo aliitoa Dk. Shein na kusisitiza kuwa upelekaji umeme katika visiwa ni muendelezo wa Sera za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuhakikisha kuwa huduma zote muhimu ikiwemo ya umeme inawafikia wananchi popote pale walipo.

Nae Waziri wa Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati Mhe. Ramadhani Abdalla Shaaban aliwaomba wananchi wa Kisiwa Panza pamoja na Makoongwe kuutumia umeme huo kwa maendeleo yao kwani umeme hivi sasa sio anasa tena bali ni nyenzo muhimu katika maendeleo ya binaadamu.

Aidha, alieleza kuwa kwa kutumia umeme mwananchi ataweza kufaidika kwa kuhifadhi vyakula, samaki, kufanya biashara ndoondogo na pia, wnafunzi wataweza kujisomea wakayti wa usiku kwa uhakika.

Alisema kuwa Wizara yake kupitia ZECO wameweza kukamilisha mradi wa usambaza umeme katika kisiwa hicho ambapo kazi zilizofanyika ni ujenzi wa njia kubwa za umeme za msongo wa 33kV zenye urefu wa km tatu ambazo zimejengwa katika upande wa Chokocho na ndani ya Kisiwa Panza.

Kazi nyengine ni uwekaji wa vituo viwili vya transfoma kila moja yenye uwezo wa 100kVA ambazo zimewekwa Mitondooni skuli na Panza, ujenzi wa laini ndogo za umeme zenye urefu wa kilomita nne pamoja na  ulazaji wa waya wa baharini wenye urefu wa kilomita mbili kutoka Chokocho hadi Mitondooni.

Waziri Shaaban alisema kuwa kazi za usambaji umeme Kisiwa Panza zimegharimu jumla ya shilingi 1,128,810, 174.00 mchango ambapo kati ya fedha hizo shilingi 604,960,764.00 zilitolewa na Serikali Kuu na Tshilingi 523,849,410 zimetolewa na Shirika la Umeme (ZECO).

Alisema kuwa waya wa baharini umetengenezwa nchini Ufaransa katika kiwanda kinachomilikiwa na Kampuni ya General Cable ya nchini Norway.

Kwa upande wa kazi za  ushauri Waziri Shaaban alisema kuwa kazi za ushauri wa matengenezo ya waya wa baharini pamoja na ulazaji wake zote za kupeleka umeme visiwani humo zimesimamiwa na wataalamu wa ZECO na hivyo kupelekea kuokoa kiasi cha shilingi milioni 363,832,917.00 fedha ambazo zingetumika kuwalipa wataalamu kutoka nje kwa ajili ya kutoa Ushauri na Usimamizi wa kazi za ulazaji waya wa baharini.

Kwa upande wa Kisiwa cha Makongwe Waziri Shaaban alitoa pongezi kwa Dk. Shein kwa kuzindua mradi mkubwa wa umeme kisiwani humo na kusema kuwa  ni fursa kwa wananchi wa Makongwe na pia, ndoto yao ya kupata umeme sasa imekuwa ya kweli.

Alisema kuwa  kazi za usambazaji umeme katika kisiwa cha Makongwe zimegharimu jumla ya Shilingi 855,229,452.00 ambapo kati ya fedha hizo Shilingi milioni 604,960,764.00 zimetolewa na Serikali Kuu na Shilingi milioni 250, 268,688 zzimetolewa na Shirika la umeme

Alitoa pongezi kwa wananchi wa Makongwe ambao mara tu kufika huduma hiyo ambapo siku ya mwanzo waliungiwa umeme wananchi 115.

Nao wananchi wa visiwaa hhivyo walitoa pongezi zao kwa Rais Dk. Shein pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Za nzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein kwa kuwafikishia huduma hiyo muhimu sambamba na huduma nyengine ambazo zimeshawafikia hivi sasa zikiwemo afya, maji, elimu na nyenginezo.

Wananchi hao walieleza kuwa neema hizo walizozipata ni lazima wamshukuru Mwenyezi Mungu na kumshukuru na kumuombea Dua Dk. Shein kwa kuwajali na kuwathamini na kusisitiza kuwa uongozi wake ndani ya miaka mitano umewaletea maendeleo makaubwa.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.