Habari za Punde

Wadau wa Ujenzi Watakiwa Kulitambua Baraza la Taifa la Ujenzi Ili Kuepuka Migogoro.

Jovina Bujulu - MAELEZO.
Wadau wa Ujenzi wameshauriwa kutumia huduma za kitalaam zinazotolewa na Baraza la Taifa la Ujenzi ili kuepuka migogoro inayojitokeza wakati wa utekelezaji wa miradi mbalimbali ya ujenzi nchini.

Wito huo umetolewa leo jijini Dar es salaam na Afisa Mtendaji Mkuu wa Baraza hilo Mhandisi Dkt. Leonard Chamuriho wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu majukumu ya baraza hilo katika utatuzi wa migogoro inayotokea katika maeneo mbalimbali.

Mhandisi Chamuriho amesema kuwa migogoro ya miradi ya ujenzi inayojitokeza mara kwa mara baina ya wadau husika hutokana na kukosekana kwa ushirikiano baina yao.

" Wadau wanatakiwa kushirikiana kulingana na makubaliano yao ili mradi husika ukamilike"  Alisema na kuongeza kuwa tofauti kati ya wadau wa miradi ya ujenzi hujitokeza kutokana na ukubwa na ugumu wake.

Aidha, Dkt. Chamuriho amesema kwamba migogoro ya ujenzi isiposuluhishwa mapema hugharimu pesa nyingi, muda wa wadau na fursa za matokeo ya miradi inayojengwa.

"Ninajua njia mahususi ya utatuzi wa migogoro inayoajitokeza nchini ni kutumia mahakama ambayo mashauri yake huchukua muda mrefu, ili kuokoa muda huu, utatuzi mbadala katika ujenzi ni kulitumia Baraza la Ujenzi" alisisitiza  Mhandisi Dkt. Chamuriho.

Akitaja majukumu mengine ya Baraza hilo amesema kuwa ni kutoa huduma za ushauri , usuluhisi wa migogoro, mafunzo, ukaguzi wa kiufundi, utafiti na kutoa machapisho ya kiufundi.

Alisema kuwa Baraza la Taifa la Ujenzi lilianzishwa kwa mujibu wa sheria ya Bunge na 20 ya mwaka 1976 na kuanza kutekeleza majukumu yake.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.