Habari za Punde

Dk. Shein Amesema Tafauti za Kisiasa Zisitumike Kuvuruga Amani Zanzibar.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Pemba                                                                7.1.2016
---
RAIS wa  Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  amesema tofauti za kisiasa Zanzibar kamwe zisitumike kuvuruga amani na utulivu ambayo ndiyo siri kubwa ya maendeleo yaliyopatikana katika visiwa vya Unguja na Pemba.

Dk. Shein ambaye alikuwa akizungumza na wananchi wa Wete waliokwenda kumsalimia mara baada ya kagua ujenzi wa soko na Ofisi ya Baraza la Mji Wete alisema kuwa suala la amani halina mbadala huku akiahidi kuendelea kuisimamia amani ya Zanzibar na kusikitishwa na wale wote wanaotaka kuvuruga amani kwa kisingizio cha kuiongoza Zanzibar.

Alisema kuwa amani na utulivu uliopo ndio msingi wa maendeleo ya Zanzibar hivyo Wazanzibari wanapaswa kuienzi na kuilinda kwa nguvu zao zote.

Dk. Shein alisisitiza kuwa kila mwananchi anataka kuishi kwa amani na utulivu na kuwataka wananchi wa Zanzibar kutambua kuwa wao ni ndugu na kuwasihi baadhi ya wananchi wanaotaka kuvuruga amani na kuendelea kutisha wenzao kwani Zanzibar inaongozwa kwa Sheria na Katiba.

“watu wasihemkwe wala wasichagawe kwani kila mmoja anataka kuishi kwa amani na utulivu sisi ni wamoja wa kusini Pemba, Kaskazini Pemba wa Kusini Unguja na  Kaskazini Unguja...tumetofautiana kwa kuishi na kutafuta maisha tu”,alisema Dk. Shein.

Kwa upande wa mradi huo Dk. Shein alirejea kauli yake kama aliyoizungumza wakati akiitembelea miradi kama hiyo katika miji ya Wete na Chake kwa kusema kuwa hizo ni miongoni mwa ahadi zake alizowaahidi wananchi za kuimarisha miji yote ya Zanzibar.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alisema kuwa mradi huo wa (ZUSP) sio mradi uliozuka bali umebuniwa na Serikali na ni mkopo wa Dola milioni 38 kutoka Benki ya Dunia.

Mapema Dk. Shein alikagua ujenzi wa barabara ya Ole-Kengeja ambao ujenzi wake unaendelea na kwa maelezo ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano Dk. Juma Malik Akili barabara hiyo inatarajiwa kuanza kutiwa lami mnamo mwezi Septemba mwaka huu,

Kwa mujibu wa maelezo ya Mkurugenzi wa Baraza la Mji Wete Mgeni Othman Juma alisema kuwa ujenzi wa mradi huo wa soko umeanza April 4 mwaka jana na unatarajiwa kumaliza April mwaka huu, kwa mkopo wa Benki ya Dunia.

Mkurugenzi huyo alieleza kuwa katika soko hilo kuna milango 35 ya biashara, milango 80 ya biashara ya mboga mboga, milango 15 ya biashara nyengine, kituo cha mabasi, banda la kusubiria gari na sehemu nyenginezo za kibiashara.

Katika maelezo hayo Tshs. Bilioni 1 zinatarajiwa kutumika na kwa hivi sasa ujenzi wa mradi huo umeshafikia asilimia 60 huku uongozi huo ukieleza kuwa lengo la mradi huo ni kufanya biashara na kuwalenga wafanyabiashara kufanya shughuli zao katika mazingira bora.

Sambamba na hayo, alieleza kuwa hatua hizo ni miongoni mwa juhudi za kupamabana na umasikini chini ni Dira ya 2020 pamoja na Mkakati wa Kukuza uchumi na Kupunguza Umasikini (MKUZA).

Nae Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Omar Khamis Othman aliahidi kuzishughulikia changamoto zilizopo hivi sasa katika eneo hilo la ujenzi na kuahidi kupata mafanikio.

Ujenzi wa soko hilo ni miongoni mwa mageuzi ya Serikali za Mitaa ambao utagharibu Dola laki 8.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.