Habari za Punde

Ni Dk Shein

  
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
 Zanzibar                                                      21.3.2016
---
MWENYEKITI wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) Mhe. Jecha Salim Jecha leo amemtangaza rasmi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwamba amechaguliwa kihalali na wananchi wa Zanzibar kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kupata kura 299,982 sawa na asilimi 91.4.

Akitangaza matokeo hayo huko katika ukumbi wa Salama, Hoteli ya Bwawani,  Mhe. Jecha alisema kuwa  Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar tayari imeyathibitisha matokeo ya wagombea na imeridhia kuwa matokeo hayo ni sahihi na hivyo kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar, 1984 kifungu cha 34 na Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar ya mwaka 1984 kifungu cha 42 (4).

Kwa mujibu wa maelezo ya Mhe. Jecha wapiga kura waliothibitishwa kwa kupiga kura baada ya uhakiki wa Daftari la Kudumu la wapiga kura ni 503,580 ambapo wapiga kura waliopiga kura kumchagua Rais wa Zanzibar walikuwa ni 341,865 sawa na asilimia 67.9 ya watu waliokuwa na sifa ya kupiga kura.

Alisema kuwa kura zilizoharibika zilikuwa ni 13,538 sawa na asilimia 0.4 ambapo kura halali alizopata kila mgombea zilikuwa ni Mhe.  Khamis Idd Lila wa ACT WAZALENDO alipata kura 1,225 sawa na asilimia 0.4, Mhe. Juma Ali Khatib wa ADA- TADEA alipata kura 1,562 sawa na asilimia 0.5, Mhe. Hamad Rashid Mohammed wa ADC kura 9,734 sawa na asilimia 3.0.

Mhe. Said Soud Said wa AFP kura 1,303 sawa na asilimia 0.4, Ali Khatib wa CCK kura 1,980 sawa na asilimia 0.6, Mhe. Mohammed Rashid Masoud wa  CHAUMMA kura 493 sawa na asilimia 0.2, Seif Sharif Hamad wa CUF kura 6,076 sawa na asilimia 1.9, Tabu Mussa Juma wa D- MAKINI kura 210 sawa na asilimia 0.1, Mhe. Abdulla Kombo Khamis wa DP kura 512 sawa na asilimia 0.2.


Wengine ni Mhe. Kassim Bakari Aly wa Jahazi Asilia kura 1,470 sawa na asilimia 0.4, Mhe. Seif Ali Iddi wa NRA kura 266 sawa na asilimia 0.1, Mhe. Issa Mohammed Zonga wa SAU kura 2,018 sawa na asilimia 0.6 na Mhe. Hafidh Hassan Suleiman wa TLP kura 1,499 sawa na asilimia 0.5.

Katika hotuba yake Mwenyekiti huyo wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar aliwaomba wafuasi wa vyama vyote vya siasa na wananchi, kumuunga mkono Rais Dk. Shein na kushirikiana katika kupigania maendeleo ya visiwa vya Zanzibar katika kipindi kijacho cha miaka mitano.

Nae Dk. Shein kwa upande wake alitoa pongezi kwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, chama cha CCM pamoja na wananchi wote waliomchagua na wasiomchagua kwa kupanda ushindi huo wa kishindo.

Dk. Shein alisema kuwa anaheshimu na anathamini sana heshima hiyo ya ushindi alioupata na kuahidi kuwa ataitumikia Zanzibar na watu wake kwa nguvu zake zote tena bila ya ubaguzi.

Aidha, Dk. Shein aliahidi kutenda haki kwa wananchi wote wa Zanzibar huku akihakikisha kuwa Zanzibar inapata maendeleo makubwa sana .

Dk. Shein pia, aliwapongeza wagombea wenziwe wote 13 wa kiti cha Urais wa Zanzibar na kueleza kuwa wamejitokeza na wameamua na hatimae kuonesha uwezo wao hukua akieleza kuwa atatumia uzoefu, uwezo alionao katika kuhakikisha changamoto zilizopo zinapatiwa ufumbuzi.

Dk. Shein pia alikutumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa vyombo vya ulinzi na usalama kwa kusimamia ulinzi na usalama katika kipindi chake chote cha uongozi wake sambamba na wakati wote wa uchaguzi wa Zanzibar.

Sambamba na hayo, alitoa pongezi kwa Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama hapa nchini Mhe. John Pombe Magufuli kwa kusimamia amani na utulivu kwani aliahidi hilo na ametekeleza kwani kauli yake alikuwa thabiti.

Alisema kuwa amani itaendelea kudumishwa na hatakuwa tayari amani iliyopo ivunjwe kwani Zanzibar inasifika kwa amani iliyonayo, jina lake, historia yake na kwa hivi sasa inahitaji maendeleo ya haraka haraka.

Pamoja na hayo, Dk. Shein aliahidi maendeleo ya haraka kwa Zanzibar na kusisitiza azma yake ya kuuimarisha uchumi wa Zanzibar kwa kwa kufikia asilimia 8 hadi 9 kwani lengo ni kupunguza utegemezi kutoka kwa wahisani na badala yake Zanzibar itegemee rasilimali zake ziliopo.

Dk. Shein aliomba mashirikiano sambamba na kuishi kwa pamoja kwani Wazanzibari wote ni ndugu.

Mapema akitoa maelezo kwa niaba ya wagombea wa kiti cha Urais wa Zanzibar,  Mhe. Hamad Rashid aliwaomba wananchi wote wakiwemo viongozi wa kisiasa kumpa mashirikiano makubwa Dk. Shein katika uongozi wake.

Mhe. Rashid alieleza haja ya kutafutiwa ufumbuzi changamoto mbali mbali zinazowakabili wananchi hapa Zanzibar huku akieleza kuwa huu ndio wakati wa kuvijenga vyama vyao sambamba na nchi yao kwa jumla.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822  
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.