Waziri wa Afya Mahamoud Thabit Kombo akizungumza na Balozi wa Kuwait nchini Tanzaania Jasem Al Najim alipomtembelea Ofisini kwake kumuelezea juu ya Mradi wa kuifanyia matengenezo makubwa Hospitali Kuu ya Mnazimmoja, Mjini Zanzibar.
Balozi wa Kuwait nchini Tanzania akizungumza katika mkutano huo uliohudhuriwa pia na baadhi ya Wakurugenzi na Wakuu wa vitengo vya Wizara ya Afya.
Mkurugenzi Mipango, Sera na Utafiti wa Wizara ya Afya Abdul-latif Khatb Haji (katikati) akitoa maelezo juu ya hatua iliyofikiwa ya mradi wa matengenezo ya Hospitali kuu ya Mnazimmoja wakati Balozi wa Kuwait alipofanya mazungumzo na Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo.
Mwenyekiti wa Baraza la Wakunga na Wauguzi Zanzibar ambae pia ni Mhadhiri wa Chuo cha Sayansi za Afya ya Binaadam Prof. Amina Abdulkadir akimuelezea Balozi wa Kuwait Jasem Al-Najim maendeleo na mitaala inayofundishwa na Chuo hicho.
Waziri wa Afya Mahamoud Thabit Kombo akiwa na mgeni wake Balozi wa Kuwait nchini Tanzania akimtembelea Hospitali Kuu ya Mnazimmoja ambayo itafanyiwa matengenezo makubwa na Serikali ya nchi hiyo.
Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo na Balozi wa Kuwait nchini Tanzania wakitembelea wagonjwa waliolazwa katika wodi ya wanaume waliopata ajali katika Hospitali Kuu ya Mnazimmoja.
Balozi wa Kuwait Jasem Al-Njim akiangali chumba cha kuhifadhia maiti (mortuary) ya Hospitali Kuu ya Mnazimmoja ambapo alisema sehemu hiyo itakuwa ya kwanza kufanyiwa matengenezo makubwa.
PICHA NA ABDALLA OMARA/HABARI MAELEZO ZANZIBAR
NA RAMADHANI ALI-MAELEZO ZANZIBAR
Serikali ya Kuwait itayafanyia matengenezo makubwa majengo yote makongwe ya Hospitali Kuu ya Mnazimmoja, mradi utakaogharimu zaidi ya shilingi bilioni 84 za Tanzania.
Akizungumza na Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo Ofisini kwake Mnazimmoja, Balozi wa Kuwait nchini Tanzania Jasim Al-Najim alisema Serikali ya nchi yake tayari imekubali kutekeleza mradi huo haraka iwezekanavyo.
Alisema timu ya wataalamu kutoka Kuwait inatarajiwa kuwasili Zanzibar mwezi Ogasti kwa ajili ya kufanya uchunguzi yakinifu na kazi za matengenezo ya Hospitali zitaanza mara tu baada ya wataalamu hao kumaliza kazi hiyo.
Aliongeza kuwa kufanikiwa kwa mradi huo mkubwa utafungua milango kwa Serikali ya Kuwait kupitia Mashirika ya misaada ya nchi hiyo kusaidia miradi mengine midogo midogo na vifaa kwa ajili ya maendeleo ya sekta ya Afya na sekta nyengine za kiuchumi na kijamii.
Balozi Al-Nagim alisema hatua hiyo ni kuonyesha umoja, ushirikiano na mapenzi ya dhati yaliopo kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Kuwait.
Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo aliishukuru Serikali ya Kuwait kwa kukubali kutekeleza mradi huo mkubwa ambao utawasaidia wananchi wote wa Zanzibar.
Aidha alizishukuru Wizara za Fedha za Serikali ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mpinduzi ya Zanzibar, ambazo zilikubali kutekelezwa kwa mradi huo ndani ya Wizara ya Afya.
Balozi Al-Najim alipata nafasi ya kutembelea baadhi ya wodi za kulaza wagonjwa na sehemu ya kuhifadhia maiti ya Hospitali Kuu ya Mnazimmoja, ambapo kutokana na kuguswa na sehemu hiyo, alisema itakuwa ya kwanza kufanyiwa matengenezo mradi huo utakapoanza.
IMETOLEWA NA HABARI MAELEZO
Ndugu zetu wazanzibaa kuweni makini na misaada ya hao waarabu, wanajifanya wazruri kwa nje lakini kumbe wanataka kuwatoa katika jamuhuri ua muungano wa tanzania na hatimae kuwatawala.
ReplyDeleteLzima ifikie wakati tutekeleze kwa vitendo kauli za viongozi wetu wakuu ya kujitegemea na kuachana na misaada yenye masharti.