Habari za Punde

Serikali ya Kuwait kutoa Bil 84/- kwa ajili ya matengenezo makubwa Hospitali ya Mnazimmoja

 Waziri wa Afya Mahamoud Thabit Kombo akizungumza na  Balozi wa Kuwait  nchini Tanzaania Jasem Al Najim  alipomtembelea Ofisini kwake kumuelezea juu ya Mradi wa kuifanyia matengenezo makubwa Hospitali Kuu ya Mnazimmoja, Mjini Zanzibar.
 Balozi wa Kuwait nchini Tanzania akizungumza katika mkutano huo uliohudhuriwa pia  na  baadhi ya Wakurugenzi na Wakuu wa vitengo vya Wizara ya Afya.

 Mkurugenzi  Mipango, Sera na Utafiti  wa Wizara ya Afya Abdul-latif Khatb Haji (katikati) akitoa maelezo juu ya  hatua iliyofikiwa ya mradi wa matengenezo ya Hospitali kuu ya Mnazimmoja  wakati Balozi wa Kuwait alipofanya mazungumzo na Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo.
  Mwenyekiti  wa Baraza la Wakunga na Wauguzi Zanzibar ambae pia ni Mhadhiri wa Chuo cha Sayansi za Afya  ya Binaadam Prof. Amina Abdulkadir akimuelezea Balozi wa Kuwait  Jasem Al-Najim maendeleo na mitaala inayofundishwa na Chuo hicho.
 Waziri wa Afya Mahamoud Thabit Kombo  akiwa na mgeni wake  Balozi wa Kuwait nchini Tanzania  akimtembelea Hospitali Kuu ya Mnazimmoja ambayo itafanyiwa matengenezo makubwa na Serikali ya nchi hiyo.


 Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo na Balozi wa Kuwait nchini Tanzania wakitembelea  wagonjwa waliolazwa katika wodi ya wanaume waliopata ajali katika Hospitali Kuu ya Mnazimmoja.
 Balozi wa Kuwait Jasem Al-Njim akiangali chumba cha kuhifadhia maiti (mortuary) ya Hospitali Kuu ya Mnazimmoja ambapo alisema sehemu hiyo itakuwa ya kwanza kufanyiwa matengenezo  makubwa.


PICHA  NA ABDALLA OMARA/HABARI MAELEZO ZANZIBAR

NA RAMADHANI ALI-MAELEZO ZANZIBAR             

Serikali ya Kuwait itayafanyia matengenezo makubwa majengo yote makongwe ya Hospitali Kuu ya Mnazimmoja, mradi utakaogharimu zaidi ya shilingi bilioni 84 za Tanzania.

Akizungumza na Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo Ofisini kwake Mnazimmoja, Balozi wa Kuwait nchini Tanzania Jasim  Al-Najim alisema Serikali ya nchi yake tayari imekubali kutekeleza mradi huo haraka iwezekanavyo.

Alisema timu ya wataalamu kutoka Kuwait  inatarajiwa kuwasili Zanzibar mwezi Ogasti kwa ajili ya kufanya uchunguzi yakinifu  na kazi za matengenezo  ya Hospitali zitaanza mara tu baada ya wataalamu hao kumaliza kazi hiyo.

Aliongeza kuwa kufanikiwa kwa mradi huo mkubwa utafungua milango kwa Serikali ya Kuwait kupitia Mashirika ya misaada ya nchi hiyo kusaidia miradi mengine midogo midogo na vifaa kwa ajili ya  maendeleo ya sekta ya Afya na sekta nyengine za kiuchumi na kijamii.

Balozi Al-Nagim alisema hatua hiyo ni kuonyesha umoja, ushirikiano na mapenzi ya dhati  yaliopo  kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Kuwait.

Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo aliishukuru Serikali ya Kuwait kwa kukubali kutekeleza mradi huo mkubwa ambao utawasaidia wananchi wote wa Zanzibar.

Aidha alizishukuru Wizara za Fedha za Serikali ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mpinduzi ya Zanzibar, ambazo zilikubali kutekelezwa kwa mradi huo ndani ya Wizara ya Afya.    

Balozi Al-Najim alipata nafasi ya kutembelea baadhi ya wodi za kulaza wagonjwa na sehemu ya kuhifadhia maiti ya Hospitali Kuu ya Mnazimmoja, ambapo kutokana na kuguswa na sehemu hiyo, alisema itakuwa ya kwanza kufanyiwa matengenezo mradi huo utakapoanza.   

IMETOLEWA NA HABARI MAELEZO

1 comment:

  1. Ndugu zetu wazanzibaa kuweni makini na misaada ya hao waarabu, wanajifanya wazruri kwa nje lakini kumbe wanataka kuwatoa katika jamuhuri ua muungano wa tanzania na hatimae kuwatawala.

    Lzima ifikie wakati tutekeleze kwa vitendo kauli za viongozi wetu wakuu ya kujitegemea na kuachana na misaada yenye masharti.

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.