Na
Salum Vuai, MAELEZO
WAANDISHI
wa habari visiwani Zanzibar wamekuja na wazo la kuanzisha taasisi ya
kumuenzi mwanahabari mkongwe marehemu
Mussa Haji Foum, aliyefariki dunia Septemba 24, 2016.
Wazo
la kuanzisha taasisi hiyo kwa jina la ‘Mussa Haji Foundation’, lilitolewa na
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Hassan
Abdalla Mitawi, wakati wa hitma ya mwandishi huyo aliyewahi kuifanyia kazi
Sauti ya Tanzania Zanzibar (sasa ZBC).
Baada ya hitma hiyo iliyofanyika jana
katika jengo la ZBC Radio Rahaleo, Mitawi alisema mtu aliyetumia muda wake
mwingi katika tasnia ya habari pamoja na kuwafundisha wengine, hawezi kupita
hivihivi bila kuwepo alama itakayotambulisha mazuri yote aliyoyafanya.
Mitawi alimsifia marehemu kwa namna
alivyokuwa mchapa kazi, mwalimu kwa waandishi aliowatangulia, mpenda ushirikiano
na wenzake pamoja na sifa ya kujiamini katika kazi.
“Mimi pamoja na nafasi za uteuzi
nilizopata, lakini kwa marehemu Mussa Haji nimejifunza mengi na kuchota sehemu
ya hazina ya maarifa aliyojaaliwa na Mwenyezi Mungu,” alieleza.
Alisema atahakikisha anasimamia vyema
azma hiyo wanahabari watakapokuwa na nguzo imara kwa jina la marehemu ambayo
inaweza kutumika kuzalisha na kuwaendeleza waandishi waliopo na watakaokuja.
Mkongwe wa tasnia ya habari Zanzibar
Enzi Talib Aboud, alisema mtu hawezi kutaja majina ya wanahabari wakubwa bila
kuwemo jina la marehemu Mussa Haji, ambaye alisema alijitolea maisha yake yote
kuiendeleza fani pamoja na kujisomesha.
“Hata kifo chake kimemkuta akiwa
kazini, hiki ni kielelezo cha mtu aliyethamini kazi yake, lakini la kufurahisha
zaidi hakuwa mtu wa kuota kuvaa joho la ukubwa kwa kulilia vyeo,” alifahamisha.
Baadhi ya watoto wa marehemu
waliohudhuria kisomo hicho, waliishukuru ZBC na wanahabari wote kwa kuonesha
upendo kwa mzazi wao huyo, huku wakiomba wapatiwe zaidi taarifa zake ili
iwe kumbukumbu nzuri kwao na kwa wajukuu
zake.
Mapema, mtangazaji wa ZBC Radio
Sheikh Mlekwa Muhidin, akitoa mawaidha, aliwakumbusha watu wote kufahamu kwamba
kifo ni faradhi isiyoweza kukimbilika kwani kiko mbele ya binadamu na sio nyuma
yake.
“Kila unapofanya sherehe za kutimiza
miaka kadhaa ya kuzaliwa, elewa kuwa unapunguza masafa kati yako na mauti
ambayo yako mbele yako unayafuata, hivyo tujue maisha ya duniani ni mafupi na
tujiandae kwa kesho,” alisema.
Marehemu Mussa Haji Foum aliyefariki
dunia Septemba 24 baada ya kugongwa na gari na kuzikwa siku iliyofuata kijijini
Pitanazako Kikombetele Wilaya ya Kaskazini ‘A’ Unguja, alizaliwa mwaka 1943 na
kuanza kazi ya utangazaji katika Sauti ya Unguja mwaka 1963.
No comments:
Post a Comment