Habari za Punde

Migomo ilivyowaathiri wajasiriamali wanawake kisiwani Pemba

 DUKA la mjasiriamali Siti Rashid Salim wa Wawi Chakechake, ambalo kwa sasa liko hoi, baada ya kutonunuliwa bidhaa zake kwa sababu za kisiasa, ambapo kabla alikuwa limejaa na kupata mauzo kati ya shilingi 150,00 hadi shilingi 160,000 kwa siku, wakati sasa anapata shilingi kati ya 10,000 hadi shilingi 15,000 (Picha na Haji Nassor, Pemba)
MJASIRIAMALI katika mji wa Chakechake anaeuza nguo, ambae hakupenda jina lake litajwe, akizungumza na waandishi wa habari mjini Chakechake katika soko la Jumapili, ambae yeye hakuathiriwa na migomo iliokuwepo kisiwani Pemba, (Picha na Abdi Juma, Pemba)


          -Jinamizi la ‘kidigitali’ kwa uchumi wa wanawake
-Wapo waliokwisha uwaga umaskini, sasa warejea tena  


Na Haji Nassor, Pemba
“UMASKINI nilishauwambia bayi….bayi…., lakini sasa naurejea taratibu maana…!!!!...’’,aliniambia mwanamke mjasiriamali.

Yeye ni mcheshi wastani na mchangamfu wakati wote na hasa anapokuwa kwenye biashara yake ya duka la vinywaji na vyombo vya matumizi ya nyumbani, eneo la Wawi wilaya ya Chakechake ndani ya kisiwa cha Pemba.

Siti Rashid Salim (39), ni mrefu wastani, mwenye uso wa duwara unaon’gaa wakati wote, ambae kwa sasa ameshatalikiwa na aliekuwa mume wake miaka minne iliopita. 
Alianaza biashara ya duka akitokea kwenye kilimo cha jembe la mkono, tokea mwaka 2012, akiamini kuwa huko ataagana na umaskini.

“Naam….. biashara ya vyombo, juisi, soda na vitafunwa ilinikubali kisawa sawa na mimi nilishaagana na umaskini kitambo, na maisha yangu yalikuwa juu na nikawa mwanamke wa kutegemewa na familia’’,alituhadithia.
Nae kama walivyo watu wengine, aliamua kufanya biashara na kujikusanyia idadi ya wateja wastani wa 40 wa siku moja, na wakati akifunga duka mishale ya saa 3:30 usiku mapato hakuyaamini.

“Mimi ilikuwa nahesabu mauzo, na kisha najikuta na shilingi 150,000 hadi shilingi 160,000 na hapo sasa familia ilianza kuniangalia kwa jicho la utajiri’’,alifafanua.
Nikizungumza nae kwenye duka lake eneo la Wawi, kwa muda wa saa moja, bila ya kutokea mteja kutokana na kugomewa kwa sababu ya chama anachokishabikia, anasema sasa yeye na umaskini yuko karibu mno mithili ya meno na ulimi.

“Ahaa…duka lilikuwa limejaa hadi bidhaa nyengine kama chupa za chai zilikuwa nimezipanga chini hadi nje barazani, sasa unaona… kama lililoingia moto, hakuna liwalo na umaskini umeshanipiga mbeleko’’,alinieleza kwa huzuni.

Mbeleko kwa Pemba ni kumchukua na kumuweka mgongoni mtu na hasa mtoto, kwa kutumia kanga ama kitenge, ndivyo mjasiriamali huyu, anavyojifananisha yeye na kurejea tena kwenye umaskini, baada ya kubaguliwa na wanakijiji wenzake.

Kwenye biashara yake hiyo mchanganyiko, alininong’oneza kwa sauti nyembamba huku akichezea chezea mkoba wangu wa kamera, kuwa uuzaji wa kinywaji cha juisi pekee aliokuwa akiitengeneza mwenyewe, akiuza kati ya shilingi 35,000 hadi shilingi 40,000 kwa siku moja.

Kumbe ndoo nne za juisi kwa wakati huo kabla ya kugomewa, 
zilimtosheleza kumudu gharama za kodi (pango) ya mlango, ambao ni shilingi 40,000 kwa mwezi mmoja.

Mwanamke huyu mfanyabiashara, ikifika mwezi Oktoba mwaka huu, atakuwa ameshajikusanyia deni la kodi ya mlango la mwaka mmoja, la shilingi 480,000 sawa na shilingi 240,000 kwa kila miezi sita.

Maana kabla ya kususiwa na wateja wake, alikuwa akiuza wastani wa shilingi 150,000 kwa siku, muda wa saa 15 anazofungua duka, kiasi ya shilingi 10,000 kwa kila saa moja, ambapo kwa sasa hazizidi shilingi 10,000 kutoka saa 1: 00 asubuhi hadi saa 3:00 usiku.

Ukifika ndani ya duka lake lililo nje kidogo ya mji wa Chakechake, utakaribishwa na vikamba kamba, alizokuwa akifungia biashara za kuning’inia sambamba na fremu za miti, zikiwa tupu alizokuwa akitunzia bidhaa.

Siti ambae ni mjane, anaeishi na mama yake wa kambo na baba yake mzazi akiwa na watoto watano, wanaomtegemea na mmoja aliekuwa akimsomesha darasa la kumi na mbili, sasa anaelekea kusita masomo kwa ukosefu wa ada kwenye shule binafsi Unguja.

Pamoja na kuambiwa uso kwa uso na baadhi ya watu kwamba amegomewa, lakini mwezi wa Machi mwaka huu, alibandikiwa karatasi ikitoa onyo kwamba kusiwe na mtu atakae mnunulia mfanyabiashara huyo.

Tangazo si ruhusa mtu yoyote kutumiya duka la siti atakaeonekana kazi kwake’ ilieleza karatasi aliobandikiwa kwenye mlango wake wa duka.

 “Mimi sitoachana na chama changu kwa sababu wengine tu hawakipendi, wao wanachama chao na sisi tuna chetu, sasa vyama na biashara havina uhusiano, maana vipo vingi kusudi mtu achague atakacho’’,alilalamika.

Siti, ni mmoja tu lakini kwa mujibu wa Chama cha Mapinduzi CCM Kisiwani Pemba, wapo wanawake 20 kisiwani Pemba, wakiwa wamegomewa biashara zao, kutokana na kushiriki uchaguzi wa marudio uliofanyika mwezi Machi 20 mwaka huu, hapa visiwani.

Wilaya ya Wete, ikiwa na wanawake wafanyabiashara sita (6), Micheweni tisa (9), Mkoani wawili (2) na wilaya ya Chakechake ikikusanya wanawake wafanyabiashara watatu (3) nao walikumbwa na hasara kwa kugomewa.

Mwanaali Ali (40) wa shehia ya Kizimbani wilaya ya Wete, yeye anasema biashara yake ya chakula bandarini wete, ameiaacha moja kwa moja, kutokana na kugomewa na wateja wake.
 “Ilikuwa mimi nauza wali, mikate, harage, chai na maandizi, na kwa siku nilikuwa nikijipatia faida kati ya shilingi 20,000 hadi shilingi 25, 000, sawa na shilingi 750,000 kwa mwezi lakini sasa wapi’’,alifafanua.  

Kabla ya kugomewa, hakuwa na tatizo la kuwahudumia watoto wake watano, wanaomtegemea, ingawa kwa sasa, hana miundombinu sahihi ya kujiipatia kipato.

Mwahija Al-masi Issa (25) wa kijiji cha Msuka Micheweni, akitoa malalamiko ya kususiwa na wateja wake mbele ya Makamu wa Pili wa rais alipowatembelea, alisema kwa sasa amelazimika kulifunga duka lake la chakula.

“Mimi kwa sasa nisharejea kwenye kilimo cha mwani, ambapo huko hupata fedha kiduchu shilingi 150,000  kila baada ya kuuza mwani nilioushughulikia kwa miezi mitatu, fedha nilizokuwa zikipata marambili kwa siku kwenye duka’’,alisema.
Lakini Sakina Pandu Makame (50) wa Kiwani wilaya ya Mkoani, yeye pamoja na kushiriki kwenye uchaguzi wa marudio, wala hajapa mtikisiko wa biashara yake, na anaendelea kula bata vyema.

‘‘Mimi nilikosa mauzo siku niliokwenda kwenye uchaguzi tu, lakini sasa biashara yangu imeneemeka, sana na wala sijaona kwamba kuna wateja wananikwepa, hakuna chama hapa kazi tu’’,alifafanua.

Fatma Kombo anaeuza biashara za nguo wa Chakechake mjini, wala hajaona tofauti kwenye mapato yake ya siku.

Maana kabla ya kuwepo kwa taarifa za migomo alikuwa akiuza shilingi 200,000 na sasa ana ongezeko la shilingi 25,000 katika mauzo yake.

“Migomo kwa kweli ipo, lakini mimi pamoja na chama nilicho, hakuna kususiwa hapa, maana kila mmoja anataka ang’ae anapotaka kwenda kwenye chama chake na nguo zangu ni za kiwango’’,alisema kwa kujiamini.

Wateja waliopo maeneo hayo, wanasema ipo kauli ya baadhi ya viongozi wa vyama vya kisiasa wametoa matamko ya kuwataka wasishirikiane na waliokubali kurejea uchaguzi wa marudio.

“Mimi lakini jina usinitaje, ni kweli chama kilitutaka tusishirikiane na walioshiriki demokrasia, moja ni hilo la kutowanunulia bidhaa zao’’,alisema.

Asha Mtende Hassan wa Wawi, anasema hawajali kuuporomoa uchumi wa mwanamke mwenzao, maana wanatekeleza maagizo ya chama chao cha CUF, ya kutoshirikiana na yeyote alieshiriki uchaguzi wa marudio.

Katibu wa CUF wilaya ya Chakechake Saleh Nassor Juma, anakiri kuwa kutowanunulia wanawake biashara zao ni kuwaangusha kiuchumi.

“Unajua hakuna dawa tamu, hii ni chungu kwa uchumi wa wanawake, lakini ndio maagizo ya chama chetu lazima tuyatii”,alisisitiza.

Katibu wa CCM Mkoa wa kaskazini Pemba Khadija Nassor Abdi, anakiri kuwa wapo wanachama wake wanawake waliogomewa kwenye biashara zao, na hivyo kuporomosha uchumi wao, ingawa chama kinajipanga kuwasaidia.

Lakini Chama cha waandishi wa habari wanawake Tanzania ofisi ya Zanzibar TAMWA, kupitia Mratib wake Mzuri Issa, hivi karibuni akizungumza na vyombo vya habari, alisema lazima udhalilishaji wa aina hii upigwe vita.

“Mwanamke kumzuilia kushiriki uchaguzi, au kumlazimisha kuchagua kiongozi anaetaka mwanamme au kumsusia biashara kwa sababu ya kutumia demokrasia yake ni udhalilisha wa kiuchumi’’,alisisitiza.

Haki ya kufanya kazi imetajwa ndani Katiba ya Zanzibar ya 
mwaka 1984, kwenye kifungu cha 21, ingawa kundi hili la wanawake kwa kususiwa kwao, wananyimwa haki hii.

Mwenyekiti wa Chama cha Wakulima taifa ‘AFP’ Said Soud Said, yeye anaona uchumi kwa kundi la wanawake unaweza kuporoka iwapo mamlaka husika hazikuwajibika.

“Kama kuna vyama au taasisi nyengine ni vyema zikae meza moja, ili kuondoa migomo, na kuona wanawake waliojiajiri hawarudi tena kwenye umaskini’’,alishauri.
Sheikh wa msikiti wa kijiji cha Ole Mchangani wilaya ya 

Chakechake, Khamis Hamad Ali, anasema hakuna namna ya kususia biashara kwa wanawake, kwa sababu za mambo ya kisiasa.

“Mwanamke ametajwa vyema sana kwenye Qur-an tukufu na hata hadithi za Mtume (S.A.W) kwamba anawajibu wa kufanya biashara, sasa lazimawapewe ushirkiano.

Mchungaji Benjamen Kissanga wa KKKT usharika wa Chakechake Vitongoji kwenye kongamano moja lililofanyika kituo cha huduma za sheria, alisema kususiana haimo katika bibilia.

“Wala kanisa halina shaka juu ya mwanamke kujitegemea kwa kufanya kama biashara, sasa wakianzisha kisha wakatemgwa kwa siasa ni kuwakabidhi umaskini’’,alifafanua.

Mkuu wa wilaya ya Mkoani Hemed Suleiman Abdalla, anasema kama ukimuelimisha mwanamke, ndio jamii hata kwenye uchumi hali iko hivyo.

Sasa wananchi niwashauri waache kuwakimbia baadhi ya wafanya biashara wanawake wa sababu za vyama vyao, waangalie jinsi wanavyoweza kuwarejesha kwenye umaskini.

Siti Rashid Salum, anashauri ili kuondoa migomo ya wafanyabiashara wanawake ni kuhakikisha vyombo husika vinakaa meza moja ili kuondoa siuntafahamu ya kisiasa.

Ingawa Mwanaali Ali, yeye anaona ili kuondoa hali hiyo, wanaoichochea wakaelimishwe ili watambue athari za za muda mrefu na mfupi.

Aliekuwa mgombe urais wa Zanzibar kwa tiketi ya chama cha JAHAZI ASILIA, Kassim Bakar Ali, anashauri kuwa, suala la vyama vya kisiasa lishughulikiwe kwenye vikao, badala ya kuhamia kwenye kuwabagua wafanyabiashara.

Viongozi wa dini, nao wamewataka waumini wao kufuata miongozo ya vitabu vyao wakati wote wa maisha yao, badala ya maagizo ya taasisi za vyama vya siasa.

Sheha wa shehia ya Micheweni Dawa Juma Mshindo, anasema wakati umefika kila jambo limalizwe kidemokrasia badala ya kuwaaumiza wanawake wenye biashara.

Mara baada ya Oktoba 28 mwaka jana Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar ZEC, Jecha Salim Jecha, kuyafuta matokeo ya uchgauzi mkuu wa vyama, hali ya kisiasa hakitulia.

Ndio maana wapo waliosusiwa kwenye biashara zao na hasa baada ya watu hao wakiwemo wanawake kukubali kurejea kwenye uchaguzi wa marudio uliofanyika Machi 20 mwaka huu.  
                   
  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.