Habari za Punde

Rais Dk Shein: Serikali kuendelea kuwekeza kwenye sekta ya afya


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                  11.11.2016
---

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amezindua wodi Mpya ya Watoto na Wazazi katika hospitali ya Mnazi Mmoja na kuahidi kuwa Serikali itaendelea kuwekeza na kuongeza bajeti yake ya kila mwaka katika sekta ya afya na elimu kwa kutambua kuwa maendeleo ya taifa lolote lile yanaletwa kwa nguvu kazi yenye afya bora na yenye elimu.

Katika hotuba yake kwa mamia ya wananchi waliohudhuria uzinduzi wa majengo hayo yenye vifaa vya kisasa, Dk. Shein alisema ujenzi wa majengo hayo ni kuendeleza dhamira ya serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma bora za afya.   

Mbali ya kutekeleza dhamira hiyo,Dk. Shein alibainisha kuwa kukamilika kwa ujenzi huo ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi yake ya kuipandisha daraja hospitali ya Mnazi Mmoja kuwa ya rufaa.

Alifafanua kuwa kukamilikam kwa wodi hizo mpya itakuwa chachu katika kuendeleza mafanikio yaliopatikana ya kupunguza idadi ya vifo vya watoto na akina mama vitokanavyo na uzazi na sababu nyenginezo hapa nchini.

Katika hotuba yake Dk. Shein alisema kuwa takwimu zinaonesha kwamba, uwiano wa vifo vitokanavyo na uzazi umeshuka kutoka vifo 288 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2010 hadi vifo 236 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2015.

Alisema kuwa kuwepo kwa majengo hayo yenye nafasi ya kutosha, vifaa vya kisasa na mazingira yenye faragha na stara ya kutosha, kutasaidia sana kuendeleza mafanikio yaliopatikana katika kushajiisha kina mama kujifungulia hospitali na katika vituo vya afya.


Aidha, Dk. Shein aliwahakikishia wananchi, kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuitekeleza ahadi aliyoitoa ya kutoa huduma za afya bure kwa wazazi wote.

Alisema kuwa  alitoa ahadi hiyo ili kuimarisha usalama wa kinamama wanaojifungua na kuwapa fursa pana zaidi wale wenye uwezo mdogo wa kuweza kufaidika na huduma hizo ili hatimae kwa pamoja kupata mafanikio yanayopatikana ya kupunguza idadi ya vifo vitokanavyo na uzazi.

Pia, Dk. Shein aliwahakikishia wananchi kwamba Serikali itaendelea kutoa huduma za chanjo kwa watoto ili kuwakinga na maradhi mbali mbali pamoja na kuhakikisha huduma za uchunguzi wa maradhi kama vile ‘X-ray’ ‘ultrasound’ na ‘CT-Scan’ na baadae ‘MRI’ zitaendelea kutolewa bure.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa Serikali ya Uholanzi kwa kutoa ushirikiano wake katika ujenzi wa wodi mpya ya wazazi na kuweka vifaa vipya vya kutowa huduma za kujifungua.

Alitumia fursa hiyo kukishukuru Chuo Kikuu cha Haukeland na Serikali ya Norway kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika ujenzi wa jengo jipya la watoto pamoja na kuweka vifaa vipya.

Aidha, Dk. Shein alisisitiza kwamba wale wote waliopewa dhamana ya kusimamia mpango na utaratibu wa kuagiza na kugawa dawa kwa wananchi lazima waongeze ari ya uadilifu na uaminifu mkubwa huku wakihakikisha kuwa dawa zinazoagizwa zinakidhi viwango vilivyowekwa na zinawafikia wananchi, kama ilivyopangwa.

Katika hotuba yake, Dk. Shein aliitaka Wizara ya Afya kuwaajiri wale wote waliotayari kufanya kazi sehemu zote za Unguja na Pemba kwa mujibu wa Mkataba wa ajira ulivyo na kutowaajiri wale wote wasiotaka kufanyakazi Pemba au mashamba.

Aliitaka wizara hiyo kuwaagiza wamiliki wote wa maduka ya dawa, Unguja na Pemba, kuzingatia taratibu za uuzaji dawa, kwa mujibu wa sheria na vibali walivyopewa.

Agizo hilo la Dk. Shein limekuja kutokana na hivi sasa kuwepo malalamiko mengi kutoka kwa wananchi juu ya kutokuwepo na utaratibu mzuri wa kufuatilia na kudhibiti uuzaji dawa unavyofanywa na wamiliki wa maduka ya dawa Unguja na Pemba.

Dk. Shein aliitaka Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Taasisi ya Viwango Zanzibar (ZBS), kulishughulikia ipasavyo kadhia ya ongezeko la kuwepo dawa bandia ambazo baadhi yake zinatengenezwa majumbani na kuishia katika maduka ya dawa pamoja na uingizaji wa bidhaa za vyakula na vinywaji visivyokidhi viwango na kuwachukulia hatua wale wote wanaohusika na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria.

Nae Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo alitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa kuendelea kutekeleza kwa kasi ahadi zake alizowaahidi wananchi wa Zanzibar.


Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.