MUHTASARI
WA RIPOTI YA KAMATI YA FEDHA, BAISHARA NA KILIMO YA BARAZA LA WAWAKILISHI KWA
MWAKA 2016/2017
Mheshimiwa Spika,
Kwanza kabisa hatuna budi
kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma mwenye kurehemu aliyetujaalia afya na
uzima na tukaweza kukutana tena hapa katika Baraza hili kwa ajili ya kutekeleza
majukumu yetu tuliyokabidhiwa na wananchi. Vile vile, sina budi kukushukuru
wewe binafsi kwa kunipatia fursa hii kuwasilisha mbele ya Baraza hili kwa niaba
ya Kamati yetu Ripoti ya Kamati ya Fedha, Biashara na Kilimo, tunaomba kwa
ruhusa yako Muhtasari huu usomwe sambamba na Ripoti yetu na ziingizwe kwenye
Hansard.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa dhati kabisa, tunatoa
shukrani zetu kwa mashirikiano makubwa tuliyoyapata wakati wa kutekeleza
majukumu yetu ya Kamati kwa uongozi wa Wizara ya Fedha na Mipango, Wizara ya
Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi na Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko
pamoja na pamoja na Taasisi zote zilizo chini ya Wizara hizo ambao ndio
wahusika wakuu waliofanikisha hadi Kamati yetu inawasilisha Ripoti hii mbele ya
Baraza lako.
Mheshimiwa
Spika,
Aidha, napenda kutoa shukrani
zangu za dhati kwa wadau na wananchi wote wa Unguja na Pemba ambao walishiriki
kikamilifu pale Kamati ilipotaka kukutana nao kwa ajili ya kutekeleza majukumu
ya Kamati, jambo hili liliipa faraja kubwa sana Kamati kuona ni kwa kiasi gani
wananchi wapo karibu na chombo chao cha Baraza la Wawakilishi na kuthamini
juhudi zinazofanywa na Wajumbe wa Baraza lako tukufu.
Mheshimiwa
Spika,
Vile vile, naomba
nitoe shukrani kwa wajumbe wa Kamati ya Fedha, Biashara na Kilimo pamoja na
Makatibu wetu ambao ndio waliofanikisha ufanisi na umahiri wa wajumbe katika
kutekeleza majukumu yao. Naomba kwa ruhusa yako niwatambue kwa majina Wajumbe
na Makatibu hao kama hivi ifuatavyo:
1. Mhe. Yussuf Hassan Iddi - Mwenyekiti
2. Mhe. Hamida
Abdalla Issa - Makamu
Mwenyekiti
3. Mhe. Ali Salum
Haji - Mjumbe
4. Mhe. Bihindi Hamad
Khamis - Mjumbe
5. Mhe. Ussi Yahya
Haji - Mjumbe
6. Mhe. Moh’d Mgaza
Jecha - Mjumbe
7. Mhe. Hamad Abdalla
Rashid - Mjumbe
8. Ndg. Salum Khamis
Rashid - Katibu
9. Ndg. Asma Ali
Kassim - Katibu
WIZARA
YA FEDHA NA MIPANGO
Mheshimiwa
Spika,
Ni ukweli kwamba
Wizara hii ndio roho ya nchi yetu kwani imepewa jukubwa kubwa sana la kusimamia
ukusanyaji wa mapato ya nchi na usimamizi wa matumizi ya fedha za wananchi.
Kamati yetu imeridhishwa na juhudi za ukusanyaji wa mapato zinazofanywa na
Wizara pamoja na Taasisi zake ikiwemo Bodi ya Mapato ya Zanzibar (ZRB) na
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) jambo ambalo limepelekea kuongezeka kwa mapato
ikilinganishwa na makusanyo ya mwaka ulioisha. Kuongezeka kwa mapato haya
kumetokana na juhudi na mikakati ya Wizara katika kuhakikisha makadirio ya
mapato yaliyokusudiwa kukusanywa na Serikali yamefikiwa lengo.
Mheshimiwa
Spika,
Hata hivyo, pamoja na
mikakati hiyo iliyowekwa Kamati yetu inaamini kuwa bado tatizo la kuvuja kwa
mapato lipo na vile vile bado yapo maeneo ya ukusanyaji wa mapato hayajafikiwa,
kwahivyo Kamati yetu inaitaka Wizara kuongeza juhudi ya kuweka mikakati
madhubuti ili kuhakikisha mapato ya nchi hayavuji na kila anayestahiki kulipa kodi
basi alipe bila ya kuwa na muhali wowote.
Mheshimiwa
Spika,
Kuna kauli ambazo
huzungumzwa na baadhi ya watu kuwa, mapato yote yanayokusanywa na TRA –
Zanzibar hupelekwa Tanzania Bara, Lakini naomba kuchukuwa nafasi hii kuwaambia
wananchi kuwa, mapato yanayokusanywa na TRA – Zanzibar yanaingia katika Mfuko
Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na yanatumika Zanzibar, wanaokaa
wakisambaza fikra potofu kama hizo kwa wananchi hawaelewi ukweli wa mambo na
tunaomba wananchi wa Zanzibar waondoe fikra hizo na waone kuwa Muungano wetu
haupo kwa kukandamiza Zanzibar bali ni kwa kuinua uchumi wa Zanzibar.
Mheshimiwa
Spika,
Katika suala la
usimamizi wa fedha za umma kwa ujumla bado kuna tatizo, hii inatokana na ukweli
kwamba Sheria ya Manunuzi na Kanuni zake hazifuatwi apasavyo, na sote
tunafahamu kuwa asilimia 70 ya matumizi ya fedha yanakwenda kwenye manunuzi.
Ukiukwaji huu wa Sheria ya Manunuzi unapelekea upotevu mkubwa wa fedha za umma,
kwani Kamati imebaini kuwa zipo baadhi ya Taasisi ambazo hufanya manunuzi hewa
lakini vile vile kutokana na uhaba wa maafisa wanunuzi zipo baadhi ya Taasisi
ambazo wahasibu au washika fedha ndio wanakuwa wanunuzi. Tunaomba sana wakati
itakapoanza kutumika Sheria mpya ya Manunuzi iliyopitishwa na Baraza hili iwe
ndio suluhisho la matumizi ya fedha yasiyofuata utaratibu wa Sheria.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yetu ilifanya ziara
katika mashamba ya Mipira kisiwani Pemba, katika ziara hiyo Kamati ilikutana na
viongozi na wafanyakazi wanaoyashughulikia mashamba hayo ambao wameunda kikundi
kinachojulikana kwa jina la JIWEZESHE GROUP. Kabla ya mashamba hayo kutumiwa na
kikundi hiki, Serikali kupitia Wizara ya Fedha iliingia mkataba na Kampuni ya
AGROTEX ambapo Kampuni ilitakiwa kulipa USD 100,000/- (Dola laki moja) kwa kila
mwaka. Hatima yake, Kampuni hii
ilishindwa kulipa fedha hizo kwa Serikali kwa kipindi cha miaka minne (4) na
vile vile iIishindwa kulipa mishahara kwa wafanyakazi. Hadi Kamati yetu
inawasilisha Ripoti mbele ya Baraza hili, Kampuni hii inadaiwa na Serikali USD
400,000/- (Dola laki nne) kama ni kodi ya mashamba hayo.
Wafanyakazi ambao walikuwa
wanayashaghulikia mashamba haya, waliamua kujikusanya pamoja na kuunda kikundi
hicho kwa ajili ya kuendeleza shughuli za uvunaji wa mpira. Idhini ya matumizi
ya mashamba hayo yalitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini – Pemba kupitia barua
ya tarehe 10 Februari, 2016 yenye Ref: NO. MKP/K.6/3/1/VOL.VII/115.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yetu haikuridhishwa na
uidhinishaji wa matumizi ya mashamba hayo uliofanywa na Mkuu wa Mkoa wa
Kaskazini Pemba. Kwani wakati uamuzi huu unafanywa mkataba kati ya Serikali na
AGROTEX bado haujavunjwa.
Vile vile, Kamati yetu
imesikitishwa sana kuona kuwa azma ya kuanzishwa kwa mashamba haya ambayo
ilikuwa ni kuinua pato la Taifa na uchumi wa nchi haijafikiwa, kwani mapato
mengi ya Serikali yaliyokusudiwa kuingia katika Mfuko wa Serikali kupitia
mashamba haya yamepotea.
Maoni na maagizo ya Kamati juu
ya kadhia hii yanaonekana katika ripoti ya Kamati, lakini Kamati inasisitiza
kuwa Wizara ihakikishe Kampuni ya Agrotex inalipa deni hilo.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yetu
inampongeza sana Mhasibu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kipindi
kifupi alichokaa katika nafasi hii mabadiliko yamenza kuonekana katika
ukusanyaji wa mapato na matumizi ya fedha. Kamati imeridhishwa na utaratibu
ulioanza kwa baadhi ya Taasisi kukusanya mapato kwa kulipa Bank na sio kulipa
cash, jambo hili ni moja kati ya mambo yaliyopelekea kuongezeka kwa mapato,
hata hivyo Kamati yetu inamtaka Mhasibu Mkuu wa Serikali utaratibu huu
wakulipia benki utumike kwa Taasisi zote za Umma ili kuziba mianya ya kuvuja
kwa mapato.
Mheshimiwa
Spika,
Suala la uwekezaji ni
moja sekta ambazo zinasimamiwa na Wizara hii kupitia Mamlaka ya Uwekezaji na
Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA), juhudi zinazofanya na ZIPA zinaonekana kwani
ipo miradi mingi inayoendelea ambayo imetokana na kuwepo kwa Mamlaka hii. Hata
hivyo, bado yapo malalamiko makubwa sana juu utendaji wa Mamlaka hii ambapo
malalamiko haya yanaleta picha mbaya katika sekta ya uwekezaji nchini. Kamati
inaitaka Wizara ya Fedha na Mipango kukaa pamoja na ZIPA kuona chanzo cha
malalamiko haya yaliyopo yanasababishwa na nini (ni utendaji kazi wa Mamlaka au
ni Uendeshaji wa Afisi ya Mamlaka). Vile Kamati inaitaka ZIPA itekeleze
majukumu yake kwa uwazi ili kuepusha malalamiko yaliyopo na kuweza kuwavutia
wawekezaji nchini.
Mheshimiwa
Spika,
Mfuko wa Hifadhi ya
Jamii ambao upo chini ya Wizara ya Fedha unalojukumu kubwa la kulipa viinua
mgongo na pencheni kwa wastaafu, hata hivyo kwa kutaka kuimarisha Mfuko huu
miradi mbali mbali ya maendeleo imeanza kufanywa ili kuimarisha maendeleo ya
Mfuko kwa maslahi ya wanachama wake. Kamati inaitaka ZSSF kuhakikisha
inasimamia vizuri miradi yake ili lengo lililokusudiwa la kuimarisha Mfuko
lifikiwe kwa maslahi ya wanachama wake. Vile vile, suala la ukataji wa Bima
katika miradi hii ni la msingi sana ili kuifanya miradi hii iwe salama zaidi na
kutumika kwa muda mrefu, lakini bado ipo miradi ya ZSSF ambayo haijakatiwa
Bima. Kamati inaitaka Wizara ya Fedha kusimamia ukataji wa Bima kwa miradi ya
ZSSF katika Shirika Bima la Zanzibar.
WIZARA
YA BIASHARA, VIWANDA NA MASOKO
Mheshimiwa
Spika,
Wizara hii ni moja ya Wizara
ambazo imekusanya sekta muhimu sana katika kuimarisha uchumi wa nchi. Ni ukweli
usiopingika kuwa nchi nyingi zilizoendelea zimeendelea kutokana na kuimarika
kwa sekta ya viwanda na biashara, kwani sekta huinua uchumi wan chi kwa kasi
kubwa sana. Kuimarika kwa sekta hizi kunatokana na kuwepo kwa Sheria na Sera
ambazo zitaweka mazingira mazuri ya kuwavutia wawekezaji katika kuanzisha
viwanda ambavyo baadae hupelekea kuimarika kwa biashara.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa kuwa azma ya Serikali katika
awamu hii ni kuimarisha sekta ya viwanda nchini bado ipo haja kubwa sana ya
kuziangalia Sheria na Sera zetu zinazohusu masuala ya uwekezaji wa viwanda
nchini, lakini vile vile kuwe na mipango madhubuti ambayo itapelekea kuimarika
kwa sekta hii, hata hivyo kuwa na mipango ni suala moja na kusimamia
utekelezaji wa mipango hiyo ni suala la jengine, kwa hivyo mambo haya mawili
yanatakiwa yaende sambamba ili kuona kuwa mipango tunayojipangia inatekelezwa.
Kamati yetu pamoja na Wajumbe wa Baraza hili tunaamini kuwa jambo litakalowezesha
kufanikiwa katika kuimarisha sekta hizi ni ni kuwepo kwa mashirikiano ya dhati
baina ya Serikali na wawekezaji.
Mheshimiwa
Spika,
Moja ya chombo muhimi ambacho
kinaweza kupelekea mazingira bora ya uwekezaji na biashara ni Baraza la
Kusimamia Utoaji wa Leseni ambalo limeundwa kwa mujibu wa Sheria Namb. 13 ya
2013 ambapo jukumu kubwa la Baraza hili ni kusimamia Taasisi zote zilizopewa
mamlaka ya utoaji wa leseni kwa lengo la kuweka mazingira bora ya utoaji wa
leseni. Kamati yetu inampongeza Waziri wa Biashara kwa kuliunda Baraza hili
hivi karibuni. Baraza hili kutokana na upya wake linakabiliwa na Changamoto
kama zinavyoonekana katika ripoti ya Kamati. Hata hivyo, Sheria iliyounda
Baraza hili limetoa uwezo kwa Baraza kutaka taarifa zinazohusuana na masuala ya
leseni kwa Taasisi yoyote inayohusika na utoaji wa leseni, lakini bado kuna
baadhi ya Taasisi ambazo zimetakiwa kuwasilisha taarifa hizo lakini bado
hazijawasilisha. Chombo kipo kwa mujibu wa Sheria na kinatekeleza majukumu yake
kwa mujibu wa Sheria, tunaomba sana Taasisi yoyote ambayo ilitakiwa kuwasilisha
taarifa zake mbele ya Baraza basi kamati inawaomba wawasilishe taarifa hizo.
Mheshimiwa
Spika,
Zao la Karafuu ni zao ambalo
linaingiza mapato katika nchi na kuchangia pato la taifa, usimamizi wa zao hili
ni suala moja muhimu sana hasa ikizingatiwa kuwa Zanzibar tunalitegemea zao
hili katika kuimarisha uchumi wetu. Ni wazi kuwa asilimia zaidi ya 90 ya zao
hili inatoka katika kisiwa cha Pemba, ipo haja kubwa sana ya kuendelea kuweka
mazingira mazuri kwa wakulima wa zao hili ili washajihike katika kuliimarisha
zao la karafuu. Tunafahamu kuwa Serikali inayodhamira ya dhati katika kuhakikisha
inaimarisha zao hili, hii inatokana na kuwepo kwa Sheria maalumu ambayo
inasimamia masuala ya karafuu.
Mheshimiwa
Spika,
Serikali imekuwa ikichukuwa
jitihada mbali mbali katika kuhakikisha inazuia magendo ya karafuu jambo ambalo
limekuwa ni tatizo kubwa sana hasa katika kisiwa cha Pemba, lakini bado tatizo
hili limeonekana kuwepo kwa baadhi ya watu kuendelea na biashara hii ya magendo
ya karafuu jambo ambalo linaweza kupelekea athari kubwa sana kwa karafuu yetu
ya Zanzibar katika masoko ya nje. Kamati inaiomba sana Serikali kuzidisha
juhudi katika kuhakikisha kuwa inadhibiti moja kwa moja magendo ya karafuu na
kama sheria ya karafuu ina mapungufu basi tunaiomba wizara ilete marekebisho ya
sheria hiyo ili tuipe meno na nguvu zaidi kwa ajili ya kuilinda na kuihifadhi
karafuu yetu.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yetu ilifanya ziara
katika nyakati tofutti kisiwani Pemba na kutembelea baadhi ya vituo vya kuuzia
karafuu, ni jambo la kusikitisha sana kuona kuwa asilimia kuwa ya karafuu
inazalishwa Pemba lakini hadi hii leo vituo vya kuuzia karafuu vinatumia vifaa
vya zamani katika kusafisha karafuu. Kamati yetu inaitaka Serikali kupitia
Wizara ya Biashara kuhakikisha kuwa inapeleka mashine za kisasa za kusafisha
karafuu kisiwani Pemba ili kupungunguza gharama za karafuu kuanza kusafishwa
Pemba na baadae zikifika Unguja zisafishwe tena.
Mheshimiwa
Spika,
Taasisi ya Viwango
Zanzibar (ZBS) ni moja ya Taasisi ambayo inasimamiwa na Wizara ya Biashara, na
jukumu lake kubwa ni kuhakikisha kuwa bidhaa zote zinazoingia nchini zinakuwa
na ubora kwa ajili ya matumizi ya mwanaadamu. Taasisi kwa Zanzibar bado ni
changa lakini hata hivyo tayari imeshaanza kutekeleza majukumu yake. Uchanga wa
Taasisi hii na ufinyu wa Bajeti bado unapelekea kushindwa kutekeleza majukumu
yake ipasavyo. Hata hivyo, Kamati imeridhishwa na jitihada za Serikali kutaka
kuipatia ZBS vifaa mbali mbali vya maabara pamoja kujenga maabara za kisasa.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yetu
inaendelea kusisitiza kuwa, utendaji kazi wa taasisi hii unategemea wataalamu,
maabara za kisasa na vifaa vya maabara, tunaomba sana ili kumlinda mtumiaji
kuweza kutumia bidhaa yenye ubora Serikali iharakishe kuimarisha taasisi hii.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati
yetu ilipata kutembelea Afisi za Shirika la Ubora la Tanzania (TBS) na kuona
hatua kubwa zilizofikiwa za kimaendeleo kwa Shirika hili ikiwemo pamoja na
kuwepo kwa maabara zenye mashine za kisasa kwa ajili ya kupima ubora wa bidhaa
mbali mbali. Vile vile imeanzisha Afisi zake katika baadhi ya Mikoa ya Tanzania
ambayo inapitisha bidhaa kwa wingi. Maendeleo haya hayakufikiwa isipokuwa ni
kupatiwa bajeti za kutosha pamoja na kuwa na wataalamu ambao hutumia taaluma zao
kwa ajili ya maendeleo ya Shirika.
WIZARA YA KILIMO, MALIASILI,
MIFUGO NA UVUVI
Mheshimiwa Spika,
Ni
dhahiri kuwa Wizara hii ndio uti wa mgongo wan chi yetu, uhai wa wananchi upo
katika Wizara hii. Wizara hii imejumuisha sekta nne muhimu sana katika maisha
ya mwanaadamu ambazo ni sekta ya kilimo, sekta ya maliasili, sekta ya mifugo na
sekta ya uvuvi. Katika kila siku za maisha yetu sekta hizi tunazifanyia kazi na
wadau wakuu wa sekta hizi ni wakulima, wafugaji na wavuvi na wanaonufaika na
sekta hizi ni wananchi wote kwa sababu kila siku sote tunakula kupitia bidhaa
za kilimo, tunajenga na kupika kupitia maliasili, tunawekeza kupitia bidhaa za
mifugo na za baharini. Mifano hii ni kuthibitisha kuwa Wizara hii ndio uhai wa
wananchi na hakuna anaweza kubeza umuhimu wa kuwepo kwa Wizara hii.
Mheshimiwa Spika,
Wajumbe
wa Baraza hili pamoja na wananchi wanapaswa kufahamu kuwa jukumu la kuimarisha
sekta hizi sio la Serikali wala sio la Waziri bali ni jukumu letu sote, na
majukumu haya yatafanikiwa pale tutakapokuwa na mashirikiano mazuri baina ya
Serikali, Wajumbe wa Baraza hili na wadau wa sekta hizi pamoja na wananchi
wote. Kamati imeridhishwa na jitihada za Serikali kupitia Waizri wa Kilimo
katika kuhakikisha kuwa sekta hizi kuu nne zinaimarika, na ni wazi kuwa
kuimarika kwa sekta hizi ni kuimarisha uchumi wa nchi na kuinua kipato cha
mwananchi wa kawaida.
Mheshimiwa
Spika,
Suala la kuwepo kwa
wataalamu wa kutosha ni jambo lisiloweza kuepukika katika nchi yoyote ambayo
inajipanga kupiga hatua ya maendeleo, na moja ya Wizara ambayo inatakiwa kuwa
na wataalamu wa kutosha basi ni Wizara hii kwani Wizara hii inatoa huduma moja
kwa moja kwa wananchi kupitia sekta zake. Hata hivyo, Kamati yetu imebaini
kuwepo kwa tatizo la wataalamu wa kutosha katika Wizara hii jambo linapelekea
malalamiko makubwa kwa wadau wa sekta hizi. Pamoja na jitihada zinazochukuliwa
na Wizara katika kuhakikisha kuwa inasomesha watumishi wake lakini pia bado
kuna tatizo la kuweka vipao mbele vya kuwasomesha watumishi ili kupunguza uhaba
wa wataalamu. Katika suala hili, Kamati yetu inaitaka Wizara sasa ianze kuweka
mpango maalumu wa kuwa na vipao mbele kulingana na mahitaji ya wataalamu katika
Wizara wakati wanapotoa nafasi za kuwasomesha watumishi wao. Lakini vile vile
suala hili liende sambamba na kuweka masharti maalumu kwa mtumishi yoyote
atakayesomeshwa na Wizara kuendelea kubaki katika Wizara kwani imeonekana kuwa
lipo tatizo kwa baadhi ya wataalamu wakishakusomeshwa na Wizara kuacha kazi au
kuchukuwa likizo bila ya malipo.
Mheshimiwa
Spika,
Naomba
kwa ufupi sana kwa umuhimu wake niizungumzie Sekta ya Uvuvi, sekta hii ni moja ya sekta ambayo Serikali inaitegemea
kupata mapato yatokanayo na sekta hii. Lakini bado mapato katika sekta ya uvuvi
Zanzibar kulingana na rasilimali ya bahari tuliyonayo hayaridhishi na
hayaendani na ukubwa wa rasilimali yetu. Kwa mfano; katika bajeti ya mwaka wa
fedha 2016/2017 Makadirio ya bajeti katika sekta ya uvuvi ni Tshs. 1,000,949,000/- katika pato la Taifa.
Kulingana na ukubwa
wa rasilimali ya bahari tuliyonayo mchango wa Sekta ya uvuvi katika pato
laTaifa bado ni mdogo sana. Hatahivyo, Kamati yetu inaipongeza Serikali kupitia
Wizara hii kwa jitihada kubwa inazozifanya katika kuimarisha sekta ya uvuvi
nchini kwa lengo la kuinua kipato cha wananchi na pato la Taifa.
Tunaomba sana
jitihada za Serikali zizidishwe katika kuhakikisha kuwa rasilimali tuliyonayo
ya bahari inatumika ipasavyo kwa lengo la kuimarisha uchumi wan chi yetu.
Tunaamini kuwa Zanzibar inaweza kujiendesha kwa kuitumia bahari tu kwani ipo mifano
ya nchi nyingi za visiwa zilizoendelea kwa kutumia bahati tu. Kwa mfano, baadhi
ya wajumbe wa Kamati yangu walibahatika kutembea katika visiwa vya Maldeves
ambavyo ni visiwa vilivyoendelea sana na uchumi wao wanategemea bahari na
utalii tu. Kwakuwa na sisi rasilimali hii tunayo hatuna sababu na sisi kwanini
tusiwe zaidi ya wao. Hivyo kamati inaishauri Serikali Kuu kuyafanyia kazi
mapendekezo yaliyowasilishwa kuhusiana na safari ya Maldeves hatua kwa hatua.
Mheshimiwa
Spika,
Naomba nikumbushie
kwa Serikali kufanya uharaka wa kuieleta Sheria ya Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari
Kuu iliyopitishwa na Bunge la Jamhuri mbele ya Baraza hili ya Muungano ili
kukidhi masharti ya kifungu cha 132 cha Katiba ya Zanzibar.
Mheshimiwa
Spika,
Suala la kutumia
baadhi ya maliasili katika nchi limeruhusiwa kufuatana na taratibu zilizowekwa
kwa mujibu wa Sheria, Kanuni au Miongozo inayotolewa na Wizara. Hivi karibinu
Wizara ya Kilimo imekuwa ikitoa matangazo mbali mbali juu matumizi ya maliasili
ya mchanga jambo ambalo limepelekea kuelewaka vibaya kwa baadhi ya wananchi na
kuzidi kujengeka khofu juu ya kuendelea kutumia maliasili hiyo. Kutokana na
uelewa huo mdogo wa wananchi, Kamati yetu inaitaka Serikali kupitia Wizara ya
Kilimo kuwasilisha taarifa maalumu kuhusu “Hali halisi ya uchimbaji wa Mchanga
Zanzibar” ili Wajumbe wa Baraza hili na wananchi wote wapate kuelewa faida na
athari zilizopo na muwelekeo wa Serikali kwa baadae.
HITIMISHO
Mheshimiwa
Spika,
Naomba kutoa shukrani
zangu za dhati kwa Wajumbe wote wote wa Baraza hili kwa utulivu wao katika
kipindi chote ambacho nilikuwa nikiwasilisha Muhtasari huu wa Ripoti yetu ya
Kamati. Nawaomba sana waijadili kwa kina ripoti hii na hatimae kuikubali.
Mheshimiwa
Spika, Naomba kutoa hoja.
……………
Mhe:Yussuf
Hassan Iddi
Mwenyekiti,
Kamati ya
Fedha, Biashara na Kilimo,
Baraza la
Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment