STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 7.2.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amesema kuwa licha ya
kuwepo taasisi zinazosimamia haki na sheria lakini bado tatizo la udhalilishaji
wa wanawake na watoto limeendelea kushamiri katika jamii.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo katika hafla ya ufunguzi wa Mahakama ya Watoto huko Mahonda Mkoa wa
Kaskazini Unguja ikiwa ni miongoni mwa muendelezo wa sherehe za kuadhimisha
Siku ya Sheria, Zanzibar kwa mwaka huu.
Katika hotuba yake kwa
wananchi, Dk. Shein alisema kuwa vitendo vya aina hiyo ni kinyume na mafundisho
ya dini, malezi pamoja na Katiba na Sheria zilizopo ambazo baadhi yake zimepata
tunzo kwa ubora wake ikiwemo Sheria ya Mtoto Namba 6 ya mwaka 2011 ambayo
imepata tunzo huko Geneva kutokana na ubora wake duniani.
Hivyo, Dk. Shein
alizitaka taasisi zinazosimamia haki na Sheria kuitumikia Serikali yao kwa
uwazi na ukweli kwa lengo la kufikia malengo yaliowekwa pamoja na kuitaka jamii
kutoa mashirikiano katika kuipatia ufumbuzi changamoto hiyo.
Dk. Shein alisema kuwa
Jamii ina dhamana kubwa ya kulea vyema watoto kwani ni dhahiri kwamba kila
mmoja ana wajibu wa kuhakikisha haki za watoto zinalindwa na maslahi yao
yanazingatiwa kuanzia kwenye ngazi za familia na siyo kwenye vyombo vya sheria
pekee yake.
Aidha, Dk. Shein alisema
kuwa taarifa za Kitengo cha Urajisi cha Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali,
zinathibitisha kuongezeka kwa kesi za aina mbali mbali katika jamii zinazovunja
haki za watoto ambazo zimeripotiwa katika mwaka 2016 ikilinganishwa na mwaka
2015.
Alieleza kuwa katika
mwaka 2016, idadi ya kesi za watoto waliopewa ujauzito zilizoripotiwa ni 26,
ikilinganishwa na kesi 19 zilizoripotiwa mwaka 2015 ambapo wamo watoto wa
darasa la sita hadi Kidato cha Nne (Form 4).
Katika hotuba yake
hiyo Dk. Shein alisema kuwa kuwepo kwa chombo kinachoonesha vimelea vya urithi
vya wazee (DNA) katu sio sababu ya kumaliza tatizo hilo katika jamii kwani
chombo hicho kinasimamiwa na mwananadamu ambapo jambo kubwa linalotakiwa ni
kubadilika na kutofanya kazi kwa mazoea.
Dk. Shein alisema kuwa
fedha nyingi zimetumika katika ujenzi wa jengo hilo ikiwa ni kwa lengo la
kutekeleza haki za watoto sambamba na kupiga vita udhalilishaji wa watoto kwa
kuuondoa kabisa kadhia hiyo huku akieleza kuwa taasisi husika zitawekwa pamoja
katika kutafuta ufumbuzi wa changamoto hiyo kama alivyofanya kwenye changamoto
ya takwimu hivi karibuni.
Alisema kuwa juhudi
mbali mbali zimechukuliwa na Serikali katika kuhakikisha vitendo hivyo
vinaondoshwa kabisa ikiwa ni pamoja kuanzisha Kampeni ya miaka miwili ya Kupiga
Vita Ukatili na Udhalilishaji wa Wanawake na Watoto Zanzibar iliyozinduliwa
Disemba mwaka 2014 ambapo Serikali
kupitia Wizara husika imeamua kufanya tathmini.
Sambamba na hayo, Dk.
Shein alitoa wito kwa wananchi kujitokeza kwenda kutoa ushahidi pale
unapohitajika ili kuepuka kesi za udhalilishaji kuishia majumbani hatua ambayo
pia, itaisaidia Serikali kufikia malengo yake iliyojiwekea.
Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kutoa pongezi kwa Majaji, Mahakimu, Makadhi na Watumishi wote wa
Mahkama kwa kuendelea kutekeleza majukumu yao ya kutoa haki kwa wananchi.
Mapema, Waziri wa Nchi
Afisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora Haroun Ali
Suleiman alisema kuwa atahakikisha Wizara yake inaendela kutoa mashirikiano na
taasisi nyengine ili kuhakikisha sheria na haki nyengine zote za mtoto
zinapatikana.
Nae Jaji Mkuu wa
Zanzibar Omar Othman Makungu alieleza
kuwa tayari taratibu zote za kuanzishwa kwa Mahkama hiyo zimekamilika, zikiwemo
za kutoa Tangazo la Kisheria katika gazeti rasmi la Serikali ikiwa ni pamoja na
kumteua Hakimu wa Mkoa wa kuendesha Mahkama hiyo Nayla Abdulbasit.
Jaji Makungu alisema
kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inajali kuthamini sana utu na maendeleo
ya watoto jambo ambalo linathibitishwa na uwepo wa elimu bila ya malipo,
matibabu bure na kuweka sheria ya watoto Nam. 6 ya mwaka 2011 ambayo inataka
kuundwa kwa Mahkama maalum za watoto ambayo hiyo ni moja wapo.
Alisisitiza kuwa
Mahkama kwa upande wake inashirikiana na Serikali katika kupiga vita vitendo
vya ukatili na unyanyasaji wa watoto na kuhakikisha kesi za aina hiyo zinapewa
kipaumbele na hazichukui muda mrefu katika kumalizika kwake ambapo haitozidi
miezi sita.
Akitoa taarifa ya
mradi wa jengo hilo la Mahkama ya Watoto,
Mrajis wa Mahakama Kuu, George Joseph Kazi alisema kuwa ujenzi wa
Mahkama hiyo umedhaminiwa na Shirika la Maendeleo ya Watoto Ulimwenguni
(UNICEF) ambalo lengo lao kuu ni kutoa msaada wa kitaalamu na kifedha kwa ajili
ya maendeleo ya haki ya mtoto kulingana na sheria ya Mtoto No. 6 ya mwaka 2011.
Alisema kuwa ujenzi
huo ulianza rasmi tarehe 04.10.2015 na kukamilika mwezi Disemba mwaka 2016
mradi ambao ni wa jengo moja ambalo linajumuisha Ofisi ya Hakimu wa Mahkama ya
Watoto, Ofisi ya Waendesha Mashtaka, Ofisi ya Makarani, Ofisi ya Ofisa wa
Ustawi wa jamii, chumba cha Computer, mapokezi na nyenginezo.
Kwa maelezo ya Mrajis
huyo wa Mahakama Kuu, ujenzi wa Mahkama hiyo umegharimu kiasi cha shilingi za
Kitanzania milioni 106,996,220.
Mwakilishi wa UNICEF
katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bi Maniza Zaman katika hotuba yake
alisisitiza kuwa Shirika hilo la Umoja wa Mataifa litaendelea kushirikiana na
kuiunga mkono Zanzibar katika kuhakikisha watoto wanaendelea kupata haki zao za
msingi.
Viongozi mbali mbali walihudhuria katika Hafla hiyo
akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Kamishna wa
Polisi Zanzibar Hamdani Omar Makame, Mawaziri,
Manaibu Mawaziri, Majaji, Mahakimu na viongozi wengine wa Serikali na vyama vya
siasa.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address:
2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment