Serikali itaendelea kudhibiti uingizwaji wa Dawa za kulevya ili kuwalinda na kuwapatia Tiba vijana walioachana na uraibu huo.
Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Mhe.Tabia Maulid Mwita ameyasema hayo katika Kituo cha Tiba na Kurekebisha Tabia Kidimni Wilaya ya Kati mara baada ya kufanya ziara katika kituo hicho.
Amesema Serikali imeweka mikakati ya kudhibiti Dawa za kulevya ili kuwakomboa Vijana kutokana na janga hilo.
Amefahamisha kuwa, Serikali itamchukulia hatua za kisheria Mtu yoyote atakaebainika anaingiza madawa hayo au kufanya uzembe katika kutekeleza Sheria ya Mamlaka ya Udhibiti na Utumiaji wa Dawa za kulevya.
Aidha ameitaka jamii kuwaunga mkono Wahanga wa uraibu waliopona ili waweze kuishi kwa furaha na kuaminika katika jamii.
Hata hivyo amewataka Wazazi na Walezi wa Wahanga hao, kuwapa moyo Vijana wao ili waweze kufuata maelekezo wanaopangiwa jambo ambalo litawasaidia kupata kwenda vizuri na kuishi kwa furaha katika jamii.
Sambamba na hayo, Waziri Tabia amewataka Vijana hao wasikubali kushawishiwa kurudi tena katika matumizi ya Dawa hizo na kuwa Waadilifu na Waaminifu katika jamii.
Nae Kamishna,Utawala, Raslimali Watu na Mipango kutoka Kituo cha Tiba na kubadilisha Tabia Khamis Vuai Rajab amesema, kituo hicho kinatoa tiba ya kurekebisha tabia pamoja na mafunzo mbali mbali ya ujasiriamali ikiwemo kilimo, Ufungaji na Gereji ya vyombo vya moto.
Aidha ametoa wito kwa Wazazi, kuwapeleka Vijana wao katika kituo hicho ili kupata tiba ya matumizi ya uraibu, vilevile kuwaweka mbali na vigenge vinavyoweza kuwarudisha katika matumizi hayo.
Akizungumza kwa niaba ya Watumiaji wa uraibu wenzake Mohamed Abdulwahid Monsour, amempongeza Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Mhe. Tabia Maulid Mwita kwa kuwaunga mkono Vijana hao jambo ambalo limewapa ari, na motisha katika utendaji wa kazi zao za kila siku.
Katika ziara hiyo, Mhe. Tabia amekabidhi Jezi seti nne na Mipira mitano kwa Waraibu hao pamoja na fedha taslim kwa Wanafunzi wanaojitolea kutoka Chuo Cha Zanzibar University (ZU).
No comments:
Post a Comment