Habari za Punde

WAANDISHI WA HABARI 8 WAIBUKA KIDEDEA TUZO ZA UMAHIRI KATIKA UANDISHI WA HABARI ZA TAKWIMU ZANZIBAR

                 ·    Redio jamii Pemba zaibuka kidedea kwa kuendeleza misingi                              ya usawa   wa kijinsia,    wakifuatiwa na gazeti la Zanzibar Leo

·  Asya Hassan wa Zanzibar Leo aibuka mshindi wa Jumla

·   Waandishi chipukizi nao wang’ara.

Jumla ya waandishi wa habari wanane (8) na vyombo vya habari vitatu (3) wameibuka kidedea katika tuzo za Umahiri za Uandishi wa Habari za Takwimu za wanawake na uongozi zilizoandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA ZNZ) kwa kushirikiana na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali (OCGS) pamoja na Jumuiya ya Wanawake wenye Ulemavu Zanzibar (JUWAUZA), Jumuiya ya Wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA) na Jumuiya ya Mazingira, Jinsia na Utetezi Pemba (PEGAO).

Miongoni mwa vipengele vilivyoshindaniwa ni kipengele cha radio, kipengele cha magazeti, kipengele cha mitandao ya kijamii, kipengele cha waandishi wa habari vijana (YMF) na kipengele cha vyombo vya habari vyenye kuendeleza na kukuza usawa wa kijinsia.

Kati ya washindi hao wanane, watano miongoni mwao walitoka katika kipengele cha waandishi wa Habari vijana ambao walitambuliwa kwa kuzawadiwa vyeti pamoja na iPad kwa kila mmoja. Washindi hao ni:

  1. Salum Ameir Salum
  2. Zurima Ramadhan
  3. Nihifadhi Abdulla Issa
  4. Fatma Hamad Faki
  5. Maryam Nassor Suleiman

Vilevile, Asya Hassan Bakar kutoka gazeti la Zanzibar Leo aliibuka kuwa mshindi wa jumla na mshindi katika kipengele cha gazeti, alizawadiwa cheki ya shilingi Milioni moja na Laki tano, cheti pamoja na trofi, mwengine ni Huwaida Nassor Moh’d kutoka Assalam Fm Radio ambae amekua mshindi wa kwanza katika kipengele cha Redio nae alizawadiwa cheki ya Shilingi milioni moja, cheti pamoja na trofi na mshindi wa kwanza katika kipengele cha mitandao ya kijamii ni Salum Ameir Salum alipokea cheki ya Shilingi milioni moja, cheti pamoja na trofi

Kwa upande wa Vyombo vya Habari jumla ya vyombo vitatu vya habari vilitambuliwa kwa juhudi zao katika kuendeleza na kukuza usawa wa kijinsia kwenye kazi zao za kila siku, vyombo hivyo vilizawadiwa cheki ya Shilingi milioni mbili (2,000,000) kwa kila kimoja pamoja na vyeti vya shukran. Vyombo vya habari vilivyoibuka washindi ni:

  • Redio Jamii Micheweni.
  • Redio Jamii Mkoani.
  • Shirika la Magazeti ya Serikali.

Waandaaji wa Tuzo hii wanatoa wito kwa waandishi wa habari wa na vyombo vya Habari kuendelea kuandika habari zinazohusu takwimu za wanawake na uongozi, kusimamia na kukuza usawa wa kijinsia, kuelezea mazuri yanayofanywa na wanawake na vikwazo mbalimbali vinavyowazuia wanawake wasifikie nafasi za uongozi.

Jumla ya kazi 235 kutoka vyombo vya habari vya aina zote vikiwemo magazeti, redio, televisheni pamoja mitandao ya kijamii, ziliwasilishwa kwa ajili ya kushindanishwa, ambapo jumla ya kazi 120 zilikabidhiwa kwa majaji kwa ajili ya kufanyiwa uchambuzi na hatimae kupatikana washindi hao.

Tuzo hizi ni sehemu ya utekelezaji wa programu ya Kuwawezesha Wanawake kushika nafasi za uongozi (SWIL), ambayo inatekelezwa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA ZNZ), Jumuiya ya Wanawake wenye Ulemavu Zanzibar (JUWAUZA), Jumuiyay a Mazingira, Jinsia na Utetezi Pemba (PEGAO) na Jumuiyay a Wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA), kwa ushirikiano na Ubalozi wa Norway nchini Tanzania.

Imetolewa na:

TAMWA ZNZ, JUWAUZA, ZAFELA & PEGAO.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.