NA HAJI
NASSOR, PEMBA
WANANCHI wa
wilaya ya Mkoani kisiwani Pemba, wameitaka Tume ya Kurekebisha Sheria Zanzibar,
kuingiza kipengele cha watoto wanaoanzia miaka 14 kulipwa fidia, wakati
wanapopata ajali wakiliokoa zao la taifa la karafuu.
Walisema wachumaji wakubwa wa zao la karafuu
ni watoto wenye umri kati ya miaka 14 hadi 17, hivyo ni vyema kwenye
marekebisho ya sheria ya fidia, watoto wenye umri huo nao wakatambuliwa na
sheria ili kulipwa fidia.
Wananchi hao walieleza hayo mbele ya
Tume ya Kurekebisha Sheria, inayoongozwa na Mwenyekiti wake Jaji Mshibe Ali
Bakari, wakati ilipokutana na wananchi hao, ili kukusanya maoni yao, juu ya
kuzifanyia mapitio sheria za usalama kazini na ile ya fidia zote za mwaka 2005.
Maoni ya wananchi hao, yalikuja kufutia
sheria ya sasa ya fidia ya mwaka 2005 kwamba, haimtambui kifidia kwa mtu
alienguka wakati akichuma karafuu, kama hajafikia umri wa miaka 18.
Mjumbe wa mkutano huo Juma Bakar
Shoka, alisema wachumaji hasa wa zao la karafuu ni watoto wenye umri kuanzia miaka
14 na kuendelea, hivyo lazima sheria iwatambue kulipwa fidia.
“Mimi napendekeza kwenye sheria mpya
ijayo ya fidia, na hawa watoto walipwe fidia, maana ndio hasa wenyewe
wanaozichuma karafuu na hata skuli wakati mwengine hufungwa’’,alipendekeza.
Nae Salum Omar alisema watu wenye
umri mkubwa, wengi wao sio wachumaji hasa wa zao taifa la karafuu, na badala
yake watoto wenye umri wa kati, ndio wahusika wakuu.
“Hata mimi napendekeza sheria ya
fidia ijayo, iwatambue watoto wenye umri kuanzia umri wa miaka 14 na kuendelea,
maana tukifanya kinyume chake, tutawakosesha haki yao ya kujifunza kuchuma
karafuu’’,alisema.
Kwa upande wake Rashid Abdalla,
alisema hata sheria inayokuja ielekeze wapi fedha hizo zinapatikana na kusiwe
na urasimu, na kumfanya mpatwa na ajali kujuta kuzifuatilia.
Akifungua mkutano huo Mwenyekiti wa
Tume ya Kurekebisha Sheria Zanzibar Jaji Mshibe Ali Bakar, alisema ingawa
sheria za kimataifa zinakataza mtoto kufanyishwa kazi zenye kuhatarisha maisha
yake, lakini hilo wataliangalia kwa ukaribu.
Katika hatua nyengine Mwenyekiti
huyo, alisema lengo la kuzifanyia marekebisho sheria za fidia na ile ya usalama
kazini za mwaka 2005, kuhakikisha wananchi wote wanaishi kwa usawa.
Sheria ambazo Tume ya Kurekebisha
Sheria Zanzibar inazifanyia mapitio ni ile sheria ya fidia ya kazini no 15 ya
mwaka 1986 pamoja na marekebisho yake ya mwaka 2005 na sheria ya usalama kazini
no 8 ya mwaka 2005.
No comments:
Post a Comment