STATE HOUSE
ZANZIBAR
OFFICE OF THE
PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Jakarta, Indonesia 07.03.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amesisitiza haja ya kuimarisha mashirikiano kwa nchi
wanachama wa Jumuiya ya Nchi zinazopakana na Bahari ya Hindi (IORA), hatua
ambayo itasaidia kwa kiasi kikubwa kukuza uchumi kwa nchi hizo sambamba na kuzitafutia
ufumbuzi changamoto zilizopo.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo katika Mkutano wa Kwanza wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya
Nchi zinazopakana na Bahari ya Hindi (I0RA), unaofanyika mjini Jakarta
Indonesia, mkutano ambao unaenda sambamba na maadhimisho ya miaka 20 ya Jumuiya
hiyo.
Katika hotuba yake
aliyoisoma katika Mkutano huo, uliowashirikisha viongozi wakuu wa nchi za
Jumuiya hiyo, Dk. Shein alisema kuwa umefika wakati kwa nchi hizo wanachama wa
Jumiya ya IORA kuimarisha zaidi ushirikiano pamoja kutatua changamoto zilizopo zikiwemo
hali ya usalama, kupambana na uharamia baharini, vita dhidi ya madawa ya
kulevya, ugaidi, athari za tabianchi na mambo mengine yanayoweza kuleta athari
katika nchi wananchama.
Dk. Shein, alitoa wito
kwa nchi hizo wanachama wa Jumuiya ya IORA kuongeza kasi katika utekelezaji wa
malengo na maazimio ya Jumuiya hiyo ikiwa ni pamioja na kuitekeleza dhana ya
uchumi wa bahari iliyoanzishwa mwaka 2015 na Jumuiya hiyo.
Aliongeza kuwa nchi
zilizopo katika eneo la Ukanda wa Bahari ya Hindi ambazo zina idadi ya watu
zaidi ya Bilioni 2 na pato la Taifa la jumla kwa Mataifa hayo lipatalo tirioni
9, iwapo zikishirikiana vizuri zinaweza kuleta maendeleo ya haraka hasa katika
sekta nzima ya biashara za kimataifa na uwekezaji katika eneo hilo.
Aliongeza kuwa,
Jumuiya hiyo ina umuhimu mkubwa kwa nchi wanachama, kwani katika kipindi cha
miaka 20 imefanya mambo mengi kwa nchi hizo ikiwa ni pamoja na kuimarisha sekta
ya uvuvi, miradi ya kuendeleza na kudumisha utalii, Mradi wa Kudumisha
Ushirikiano wa Utamaduni, kuimarisha usafiri wa bahari na Mpango wa kuwawezesha
wanawake kiuchumi na mengineyo.
Kwa niaba ya Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Pombe Joseph Magufuli, Dk. Shein alisaini
makubaliano yaliyofikiwa na Jumuiya hiyo katika mkutano huo na kuahidi kuwa
Tanzania itachukua juhudi za makusudi katika kuyatekeleza makubaliano hayo kwa
lengo la kuiimarisha Jumuiya hiyo.
Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kuwakaribisha wajumbe kutoka katika nchi wanachama wa Jumuiya hiyo
kuhudhuria mkutano utakaofanyika Zanzibar katika mwezi wa Septemba utakaohusiana
na Utekelezaji wa Mikakati yenye kulenga kuimarisha uongozi wa masuala ya
uvuvi, bahari pamoja na rasilimali zake.
Aidha, Dk. Shein aliwapongeza
wananchi wa Indonesia kwa mapokezi yao mazuri na ukarimu wao kwa viongozi na
wageni waliohudhuria mkutano huo na kutoa pongezi kutoka kwa Rais John Pombe
Magufuli aliyemuwakilisha katika mkutano huo kwa kutayarisha vyema mkutano huo
ambao umepata mafanikio makubwa.
Dk. Shein alitoa
pongezi zaidi kwa Sekretarieti ya Jumuiya hiyo kwa ushirikiano mzuri na
Serikali ya Indonesia kwa maandalizi mazuri waliyoyafanya ya mkutano huo wenye
kauli mbiu ya maadhimisho ya mika 20 ya Jumuiya hiyo isemayo “Kuimarisha
ushirikiano wa bahari kwa lengo la kudumisha amani na usalama katika Bahari ya
Hindi”.
Pamoja na hayo, Dk.
Shein alitoa pongezi kwa Washirika wa
mazungumzo ambao jumla yao ni nchi saba zikiwemo Jamhuri ya Watu wa China,
Misri, Ufaransa, Japan, Uingereza, Marekani na Ujerumani kwa kufanya kazi kwa
karibu na nchi wanachama wa Jumuiya ya IORA hatua ambayo imewezesha kupata
mafanikio makubwa ya kiuchumi na kimaendeleo katika nchi za ukanda wa bahari ya
Hindi.
Jumuiya hiyo ambayo
imetimiza miaka 20 tokea kuanzishwa kwake ina wanachama 21 wakiwemo Australia,
Bangladesh, Comoro, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Thailand, Umoja wa Falme za
Kiarabu, Indonesia, Malaysia, Madagascar, Msumbiji, Srilanka, Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Yemen, India, Kenya, Mauritania, Oman, Singapore,
Shelisheli, Afrika Kusini na Somali.
Viongozi wa nchi mbali
mbali kutoka Jumuiya hiyo walipata fursa ya
kutoa hotuba zao ambapo walisisitiza haja ya kuimarisha mashirikiano kwa
nchi wanachama katika mipango ya kujiletea maendeleo sambamba na kuweka
mikakati madhubuti katika kutatua changamoto zilizopo pamoja na kuutumia vyema
ukanda wa Bahari ya Hindi.
Walieleza kuwa hali ya
amani na utulivu sambamba na kuweka mazingira mazuri ya kiuchumi iwapo
yatafikiwa kwa pamoja maendeleo makubwa yataendelea kupatikana katika Jumuiya
hiyo.
Mapema akitoa hotuba
yake katika uzinduzi wa Mkutano huo wa viongozi wakuu, Rais wa Jamhuri ya
Indonesia ambaye pia, ni Mwenyekiti wa
Mkutano huo, Joko Widodo alitoa pongezi kwa viongozi wote wa Jumuiya ya
IORA na kusisitiza kuwa azma ya Jumuiya hiyo ni kuimarisha mashirikiano na
urafiki kwa nchi wanachama wa Jumuiya hiyo ili kuona zinaendelea kupiga hatua
kimaendeleo, kiuchumi na kisiasa.
Aliongeza kuwa
kuimarika kwa Jumuiya hiyo tokea ilipoasisiwa mwaka 1997, imeweza kuleta
mafanikio makubwa kwa nchi wanachama na ikiwa ni pamoja na kutekeleza lengo la
kukuza uchumi na kusisitiza haja ya uhifadhi wa mazingira hasa ya bahari,
uwezeshaji wanawake kiuchumi na kueleza kuwa ukuaji wa teknolojia nao utasaidia
kuimarika kwa Jumuiya hiyo.
Mikakati mbali mbali
ilielezwa na Wenyeviti wa vikao vilivyotangulia vikiwemo vikao vya Mawaziri
pamoja na Wadau wengine kutoka nchi wanachama katika uzinduzi wa Mkutano huo wa
Kwanza wa Wakuu wa Nchi na Srrtikali wa Jumuiya ya Nchi zinazopakana na Bahari
ya Hindi (IORA) unaofanyika Mjini Jakarta Indonesia.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment