Habari za Punde

Walimu watakiwa kuzidisha juhudi ili kuhakikisha wanafunzi wanafaulu mitihani yao

Na Hanifa Salim , Pemba

WALIMU wametakiwa kuzidisha juhudi ya kufundisha na kusimamia maendeleo ya wanafunzi ili kuhakikisha wanafaulu katika mitihani yao.

Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba, Mwanajuma Majid Abdalla, alipokua akizungumza na walimu na wanafunzi wa Skuli ya Sekondari ya Vitongoji, wakati wa makabidhiano ya uwezekaji wa mabanda matano ya Skuli hiyo.

Alisema   waalimu ni vyema kushirikiana kwa pamoja katika ufundishaji wa wanafunzi na kuzitumia fursa walizonazo  katika uwajibikaji kama inavyotakiwa.

“Lazima tuhakikishe tumetoa vigezo vizuri katika Skuli yetu, tuhakikishe tunapasisha wanafunzi katika kiwango kizuri, hizi fursa tuzitumie vizuri waalimu tuwajibike inavyotakiwa” alisema Mkuu huyo.

Aliwataka wanafunzi kusoma kwa bidii na kuachana na vitendo vya udhalilishaji ambavyo vimekuwa vikijitokeza katika Skuli mbali mbali sambamba  na kujiepusha vishawishi watakavyo kumbana navyo ili kujijengea maisha mazuri ya baadae.

“Wanafunzi jitahidini  musome mambo mengine kwani  mtayakuta baadae hakuna haja ya kukimbilia maisha lengo lenu ni kusoma tu wakati ukifika yatakuja wenyewe baada ya kujijengea maisha yenu”, alisema.

Hata hivyo aliwataka walimu kushirikiana kwa pamoja na kamati ya Skuli ili kujipanga zaidi kudhibiti matendo machafu yanayojitokeza yakiwemo ya udhalilishaji ili kuweza kufikia lengo linalokusudiwa.

Kwa upande wake ,Mkurugenzi wa Baraza la mji Chake chake Pemba,Nassor Suleiman Zaharan,akithibitisha uchangiaji wa Baraza la Mji kwa Skuli hiyo, alisema ni jukumu lao baraza kufanya hayo kwa wananchi ili kuwaletea wananchi maendeleo.

Alisema Baraza lake liliamuwa kuchangia ujenzi wa Skuli hiyo baada ya kuona Wazazi na Walimu wa Skuli hiyo kuamuwa kujenga Skuli hiyo na hivyo baraza likatowa mchango wa kuezeka.

Nae, Mwalimu wa Skuli ya Sekondari Vitongoji, Hamad Abdalla Hamad, wakati   akisoma risala ya makabidhiano hayo alisema analiamini baraza kwa kuwaunga mkono na kuwaomba wendelea kuwasaidia katika changamoto mbali mbali zinazowakabili Skulini hapo.

Alisema   hadi kufikia kuweka linta Skuli hiyo ,tayari ilishatumia jumla ya Shilingi 29,790,000/= harama  ambayo haikujumuisha gharama ya uezekaji ambapo   ilifanywa na Baraza la Mji Chake chake.

“Fedha iliyotumika katika ujenzi hadi kufikia hatua ya uwekaji linta umejuisha mchango wa wahisani ambayo ni Shilingi 7,000,000/= na 19,334,000/= zikiwa ni michango ya wazee na Skuli” alisema.

Alisema changamoto zinazowakabili katika banda hilo la Skuli ni ukamilishaji hatua ya upigaji plasta, uwekali wa sakafu na apron ambapo kwa makisio ni Shilingi 29,510,000/= ambazo bado ni mzigo mzito kwa Skuli na jamii iliyowazunguka.

Nae ,Mwalimu Mkuu wa Skuli hiyo, Yussuf Ali Abrahman, alishukuru kupatiwa msaada huo wa uwezekaji wa Skuli yao kupitia Baraza la Mji Chake chake na alilitaka baraza kuendelea kuwaunga mkono kwa kuwasaidia ili kuondokana na changamoto zinazowakabili.

“ Hatuna budi kulishukuru baraza la Mji wa Chake Chake , kwa msaada wao mkubwa waliotupatia , hata hivyo tunawaomba isiwe mwisho kutusaidia kwani tuhaitaji misaada mbali mbali kwa ajili ya maendeleo ya Skuli yetu.” Alisema.


Jumla ya bati 340 zimeezekwa katika Vyumba  vitano vya Skuli ya Sekondari ya Vitongoji zenye thamani ya Shilingi milioni 15,000,000/=  ambazo zimegharamiwa kupitia baraza la Mji Chake chake.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.