Habari za Punde

Balozi wa Cuba Nchini Tanzania Azungumza na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Shein Ikulu Zanzibar leo.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                         19.4.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameipongeza Serikali ya Cuba kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya na kueleza haja ya kuendelea na hatua hiyo kwa sekta nyengine ili kuzidisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na nchi hiyo.

Akizungumza na Balozi mpya wa Cuba katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Lucas Domingo Hernandez Polledo Ikulu mjini Zanzibar,  Dk. Shein alieleza kuwa uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya  Cuba na Zanzibar una historia kubwa kwani nchi hiyo ni ya mwanzo kuyatambua Mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964 na kuanzisha ushirikiano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar tokea kipindi hicho hadi hii leo.

Katika Mazungumzo hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa Cuba ina historia kubwa katika juhudi za kuiunga mkono Zanzibar kwenye sekta za maendeleo hasa sekta ya afya kwani tokea mwaka 1966 nchi hiyo imekuwa ikileta madaktari wake kwa awamu kuja kufanya kazi katika sekta hiyo hapa Zanzibar.

Alieleza kuwa mbali ya madaktari hao kuja kufanya kazi kwa kutoa huduma ya afya kwa jamii hapa nchini, pia, Cuba imekuza uhusiano wake kupitia sekta ya afya kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuanzisha chuo cha Udaktari ambacho tayari kimeshaanza kuzaa matunda kwa kutoa Madaktari Wazalendo ambao hivi sasa wanatoa huduma za afya hapa nchini.

Dk. Shein alisema kuwa Madaktari hao kutoka nchini Cuba wamekuwa wakifanya kazi ya kutoa huduma ya afya kwa wananchi wa Unguja na Pemba usiku na mchana kwa kushirikiana na madaktari wazalendo.

Aidha, Dk. Shein alieleza kuwa mbali ya ushirikiano katika sekta ya afya ipo haja ya kuanzishwa ushirikiano katika sekta ya utalii kutokana na Cuba kupiga hatua kubwa na kupiga hatua katika sekta hiyo.

Aliongeza kuwa Zanzibar ina mengi ya kujifunza katika sekta ya utalii kutoka Cuba kutokana na nchi hiyo kujiimarisha kwenye sekta ya hiyo na kuweza kupata mafanikio makubwa  sambamba na kuendeleza vyanzo vyake vya utalii likiwemo eneo maarufu la ukanda wa  kitalii la ‘Varadero’.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alisema kuwa ushirikiano huo, ni vyema ukahusishwa na  Miji Mikongwe ya Zanzibar na Cuba ukiwemo Mji Mkongwe wa Zanzibar na Mji Mkongwe wa Havana ambayo yote  ina historia kubwa pamoja na vivutio kadhaa  vya kitalii ndani yake.

Akieleza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta hiyo ya utalii, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa kumalizika kwa jengo la abiria katika uwanja wa ndege Kimataifa wa Abeid Amani Karume nako kutachangia ujio wa watalii wengi kutoka nchi mbali mbali duniani wanaokuja kuitembelea Zanzibar.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumuekleza Balozi huyo haja ya kuwepo kwa mashirikiano katika sekta ya elimu hasa kwa kuvihusisha vyuo vikuu vya Zanzibar kikiwemo Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) na vile vya nchini kubwa hasa katika suala zima la ufanyaji wa tafiti mbali mbali ambazo zitasaidia masuala mbali mbali kati ya pande mbili hizo.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alisisitiza haja kwa viongozi wa nchi mbili hizo kuimarisha uhusiano kwa kutembeleana na kubadilishana uzoefu na ujuzi huku akitumia fursa hiyo kuwakarisha wanachi wa Cuba kuja kuitembelea Zanzibar hatua ambayo itazidi kuimarisha uhusiano na ndugu zao wa Zanzibar ambao nao watatumia fursa hiyo kwenda kutembelea nchi hiyo.

Dk. Shein alimuhakikishia Balozi huyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendeleza uhusiano na ushirikiano wake na Cuba kwa lengo la kuimarisha udugu na umoja wao uliopo wenye kihistoria kwa pande mbili hizo.
                        
Nae Balozi mpya wa Cuba katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Lucas Domingo Hernandez Polledo alimueleza Dk. Shein kuwa Cuba inathamini sana uhusiano na ushirikiano wa kihistoria kati yake na Zanzibar na kuahidi kuwa nchi yake itaendelea kuudumisha.

Balozi Polledo alimuhakikishia Dk. Shein kuwa Cuba iko tayari kuendeleza uhusiano huo kwa kuimarisha sekta nyengine za maendeleo ikiwemo sekta ya utalii, elimu na nyenginezo huku akieleza kuwa hatua ya nchi yake kuleta madaktari wake hapa Zanzibar  itaendelea kwani ni ya kihistoria sambamba na madaktari wa Cuba kutoa mafunzo ya udaktari hapa nchini.

Alisisitiza kuwa madaktari wa Cuba wanaofanya kazi zao hapa Zanzibar wameridhishwa na kufarajika na mashirikiano wanayoyapata kutoka kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na madaktari wazalendo na  wananchi wake ambao wanazipenda huduma wanazozitoa.

Balozi huyo mpya wa Cuba alimueleza Dk. Shein hatua za makusudi atakazozichukua katika kuhakikisha nchi hiyo inaimarisha sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo afya, elimu, utal;ii na nyenginezo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.