Habari za Punde

Dk. Shein afungua Semina ya viongozi na waandishi wa habari


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                   01.04.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amevitaka vyombo vya habari vya Serikali kufuatilia kwa karibu matukio na maendeleo ya Serikali kwa kujua vipaumbele vyake na kuwa vya mwanzo kutoa taarifa muhimu na zilizo sahihi ili jamii iendelee kujenga imani na Serikali yao.

Dk. Shein ameyasema hayo leo huko katika ukumbi wa Baraza la Zamani la Wawakilishi wakati akifungua Semina ya siku moja ya Viongozi, Watendaji Wakuu wa SMZ, Waandishi wa Habari, Wapiga Picha na Wahariri wa Vyombo vya Habari vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Katika hotuba yake ya ufunguzi huo, Dk. Shein alisema kuwa ni muhimu kwa waandishi wa habari wa vyombo vya umma kuvifahamu vyema vipaumbele vya serikali na masuala ambayo kwa wakati huu Serikali imeyatekeleza vizuri na kuwataka viongozi wa taasisi husika kushirikiana na waandishi wa habari wa vyombo vya umma kutangaza mafanikio hayo.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa historia ya vyombo vya habari vya Zanzibar na kusema kuwa Zanzibar ina historia ndefu ya vyombo vya habari ambapo Sauti ya Tanzania ya Zanzibar ilikuwa ya mwanzo kuanzishwa Afrika kwenye miaka ya 50 na ya mwanzo kuanzisha Televisheni ya rangi katika nchi za Afrika Mashariki na Kati.

Pia, Shein alieleza kuridhika kwake na mabadiliko makubwa yanayoendelea kufanywa hivi sasa katika Shirika la Habari la Utangazaji Zanzibar (ZBC) Radio na TV, pamoja na Gazeti la Zanzibar Leo ili kuhakikisha vyombo hivyo vinakwenda sambamba na sayansi na teknolojia.

Aidha, Dk. Shein aliwataka viongozi wa Serikali na Waandishi wa habari kujenga utamaduni wa kuweka kumbukumbu za matukio na ahadi za Serikali ili kuweza kufuatilia na kufahamu hatua za utekelezaji wa ahadi hizo na kwa wakati muwafaka kuiarifu jamii hali halisi.

Alieleza kuwa hatua hiyo itaondosha uwezekano wa watu wasioyayajua mambo hayo kueneza habari zisizokuwa za kweli “Siku hizi tumbaku zimekuwa nyingi na ili tumbaku zisitokezee ni jukumu la viongozi wa Serikali kutoa taarifa sahihi na wakati sahihi katika vyombo vya habari”,alisema Dk. Shein.

Dk. Shein alisema kuwa vyombo vya habari vina umuhimu wa pekee katika kusukuma mbele maendeleo ya nchi na kukuza demokrasia, hivyo ni lazima ifahamike kwamba inapodhamiriwa kuleta maendeleo endelevu na kujenga demokrasia ya kweli ni lazima iwepo jamii yenye uwelewa wa mambo ya ndani na nje ya nchi.

Alisisitiza kuwa ni jukumu la Serikali kuwapa wananchi taarifa kila inapobidi kupitia vyombo vya habari na ndipo kutokana na umuhimu huo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zimetambua umuhimu huo kwenye Katiba zake ambapo kwa upande  wa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, Sura ya tatu, kifungu cha 18(2).

Aliongeza kuwa vyombo vya habari vya Serikali vinapaswa kujenga taswira kwa umma kutokana na taarifa zake inazozitoa na vyombo binafsi na si mbadala wa vyombo vya Serikali bali vina kazi ya kuongeza nguvu kwa vyombo hivyo.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa vyombo vya Habari vya binafsi vina kazi ya kushirikiana pamoja na vyombo vya habari vya Serikali na si kuipinga Serikali kwani lengo ni kuwatumikia wananchi.

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliwataka viongozi wote wa Serikali kutoa taarifa kwa wananchi kuhusu utekelezaji wa mipango na mikakati ya Serikali kwenye vyombo vya habari na kutowaogopa waandishi wa habari au kuogopa maswali yao.

Dk. Shein alieleza matumaini yake kuwa baada ya semina hiyo ukurasa mpya wa maendeleo utafunguliwa katika utoaji wa taarifa kwa wananchi kupitia vyombo vya habari vya Serikali na hata vile vya binafsi.  

Katika maelezo yake Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa waandishi wa Habari wa vyombo vya Habari vya Serikali na vile vya binafsi kwa kazi nzuri wanazofanya za kutoa habari.

Nae Waziri wa Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo Rashid Ali Juma alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa kuwa na wazo zuri la kufanyika kwa Semina hiyo ambayo ni muhimu kwa viongozi na waandishi wa Habari kwa maendeleo ya nchi.

Aliongeza kuwa Semina hiyo italeta mashirikiano makubwa hatua ambayo itawasaidia wananchi kuendelea kupata habari kutoka vyombo vya habari vya Serikali na vile vya binafsi.

Mapema, Katibu Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alisema kuwa Semina hiyo ya siku moja ina madhumuni ya kujenga maelewano na mahusiano mazuri kati ya waandishi wa habari na viongozi ambao ni watunga Sera pamoja na kuelewa wajibu na majukumu ya viongozi na waandishi wa habari hasa wa vyombo vya umma.

Katika semina hiyo Mada ya Umuhimu wa Vyombo vya Habari na Maendeleo ya Taifa ilitolewa na Hassan Abdallah Mitawi ambaye ni Naibu Katibu Mkuu Habari, katika Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo na baadae michango mbali mbali ilitolewa.
 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.