Habari za Punde

Dk Shein: Serikali itawapelekea maendeleo wananchi popote walipo



STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Pemba                              03.04.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein amewataka wananchi watambue kwamba huu si wakati tena wa kukaa maskani wakapeana ahadi zisizokuwepo na badala yake wafanye kazi na Serikali yao itaendelea kuwaunga mkono kwa kuwapelekea maendeleo popote pale walipo.

Dk. Shein aliyasema hayo katika hafla ya uzinduzi wa barabara ya Mgagadu-Kiwani, Mkoa wa Kusini Pemba, iliyojengwa kwa fedha za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ambapo kazi za ujenzi imefanywa ka kusimamiwa na Wizara ya Ujenzi Mawasiliano na Usafirishaji kupitia Idara ya Ujenzi na Utunzaji UUB.

Katika hotuba yake kwa wananchi, Dk. Shein aliwaeleza wananchi kuwa wakati wa kupiga siasa umekwisha na kilichokuwepo hivi sasa ni kufanya kazi kwa kila mmoja alieajiriwa na asieajiriwa na wale wanaojishughulisha na kilimo waendelee na shughuli zao hizo kwa lengo la kujiletea maendeleo.

Alisema kuwa uchaguzi haupo tena hadi mwaka 2020 na kuongeza kuwa vyama vya siasa vipo lakini hakuna chama kitakacholeta Serikali nyengine kwani tayari Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ipo madarakani ambayo imekuwa ikiwaheshimu na kuwapelekea maendeleo wananchi popote pale walipo.

Dk. Shein alisema kuwa yeye ndie Rais wa Zanzibar na kila analosema ana uhakika nalo kwani hana kawaida ya kusema uwongo, hivyo aliendelea kuwaasa wananchi kisiwani humo kuendelea na shughuli zao na kutosikiliza tumbaku za mitaani.

“Wananchi wafanye kazi na zingatieni maelezo ninayosema mbali ya kuwa mimi ndie Rais wenu pia, ni mwenenu na ndugu yenu…mjue kuwa hapa hakuna Serikali nyengine itakayokuja kwani serikali halali ya Mapinduzi ya Zanzibar ipo na itaendelea kuwepo”alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein aliwaeleza wananchi katika hafla hiyo kuwa barabara hiyo ni ya watu wote na waitumie kwa maslahi yao kwani fedha zilizojengewa zinatokana na kodi za wananchi wa Unguja na Pemba huku akiwataka waitunze na kuienzi.

Alisema kuwa Serikali inaendelea kutimiza ahadi yake ya kuwapelekea wananchi maendeleo huku akiwaeleza wananchi kuwa bado ujenzi wa barabara nyengine muhimu unaendelea tena kwa kiwango cha lami kisiwani humo.

Pamoja na hayo, Dk. Shein aliwaeleza wananchi wa Kiwani na vitongoji vyote ilikopita barabara hiyo, kuanzia Mgagadu, Kivumoni, Minazini, Kirimdomo, Kendwa, Jundamiti hadi kufikia Kiwani Pwani kuwa kufunguliwa kwa barabara hiyo ni furaha kubwa kwao.

Miongoni mwa barabara ambazo Dk. Shein alizitaja kuwa zimo katika ujenzi ni barabara ya Ole-Vitongoji, Pujini hadi Kengeja yenye kilomita 35 imeanza kwa kifusi na baadae itatiwa lami huku akieleza azma ya ujenzi wa barabara  ya Chake Chake-Ziwani hadi Wete nayo itajengwa kwa kiwango cha lami ambapo ujenzi wake utaanza si muda mrefu.

Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar inaendelea kwa kasi kubwa katika kuimarisha sekta zake za maendeleo na kuwahakikishia wananchi kuwa ahadi zote zilizoahidiwa zitatekelezwa.

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliwaahidi wananchi wa Kiwani kuwa kisima chao kitatiwa umeme chini ya miezi miwili na nyumba ya daktari itajengwa, ahadi hizo zinatokana na ombi la wananchi hao lililotolewa na Mzee Omar Khamis ambaye nae alitumia fursa hiyo kumshukuru Dk. Shein kwa niaba ya wananchi wa Kiwani.

Nae Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji Balozi Ali Karume alisifu mashirikiano makubwa yaliopo katika Wizara yake hali ambayo ndio chachu ya mafanikio katika Wizara hiyo.

Balozi Karume alisifu juhudi za Dk. Shein za kutekeleza ahadi anazoziahidi na kueleza kuwa ni kiongozi wa pekee anaefuatilia kwa karibu miradi ya maendeleo katika Serikali anayoiongoza huku akisisitiza umuhimu wa uzalendo.

Mapema Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji Mustafa Aboud Jumbe  akitoa taarifa fupi juu ya ujenzi wa barabara hiyo alisema kuwa ujenzi huo ni mojawapo ya jitihada ambazo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikichukua tokea Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964 ya kujenga ustawi wa wananchi katika kuimarisha miundombinu ya barabara za mijini na vijijiji kwa Unguja na Pemba.

Alisema kuwa ujenzi huo ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya maendeleo, Mkuza III, Sera ya Taifa ya Usafiri pamoja na Mpango Mkuu wa Usafiri Zanzibar na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi.

Aliongeza kuwa Mradi wa ujenzi wa barabara ya Mgagadu-Kiwani ulianza rasmi mwaka 2009 na umechukua muda mrefu kukamilika kutokana na changamoto mbali mbali zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wake.

Katibu huyo alieleza kuwa Februari 2017 barabara hiyo imekamilika rasmi kwa kiwango cha lami mpaka pwani ambapo ujenzi wake ulikuwa wa awamu tatu.

Mradi huo umefadhiliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia fedha za maendeleo kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina kwa hatua ya awali pamoja na Mfuko wa Barabara Zanzibar kwa hatua za ukumilishaji wa ujenzi kwa gharama za Tsh Bilioni 1.4 .

Alieleza kuwa Barabara hiyo ina kilomita 8.85 ambapo hapo awali ilipangwa kujengwa kilomita 7.6 na ongezeko la kilomita 1.25 limekuja kutokana na agizo la Rais mara baada ya wananchi wa Kiwani Likoni kumuomba barabara hiyo iwekwe lami hadi pwani na yeye alikuba kutokanan na umhimu wake.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.