RAIS wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk: Ali Mohamed Shein, amewataka
watendaji wa serikali kisiwani Pemba, kutojiingiza kwenye biashara haramu ya
magendo ya karafuu, na badala yake wawe wasimamizi wakuu wa kutotoroshwa kwa
zao hilo la taifa.
Alisema msimu mwengine wa uchumaji wa
zao la karafuu unakuja, hivyo kila mmoja awe mlinzi wa biashara hiyo kwa
mwenzake, na wasiwe sehemu ya kurahisisha uvuushaji wa karafuu, kwa njia ya
magendo na hatua za kinidhamu zitachukuliwa kwa atakaebainika.
Dk Shein alieleza hayo, ukumbi wa
kiwanda cha mafuta ya makonyo Wawi Chakechake, alipokuwa akizungumza na
watendaji wakuu wa serikali kisiwani Pemba ikiwe ni sehemu ya ziara ya siku
tano kisiwani humo.
Alisema serikali kwa msimu ujao,imejipanga
vyema kuzuia magendo ya karafuu, hivyo lazima kila mmoja atekeleze wajibu wake
wa kuzuia biashara hiyo ya magendo hayo.
Alieleza kuwa, msimu uliopita wapo
baadhi ya watendaji walikuwa na sura ya kuhusika na magendo ya karafuu, na kisha
kuvutana wenyewe kwa wenyewe, jambo ambalo halipendezi.
“Msimu wa karafuu unakuja, sasa
nyinyi watendaji wa serikali lazima mshirikiane kuhakikisha hakuna mtendaji
anaeshiriki biashara hii haramu ya magendo ya karafuu’’,alifafanua.
Kuhusu karafuu za mikoa ya Morogoro
na Tanga Tanania bara zinazoingia kisiwani Pemba kwa njia ya magendo, alisema
bado serikali inaendelea na msimamo wake, wa kutozinunua karafuu hizo, kwa vile
zinaweza kuharibu ubora wa karafuu za Zanzibar.
Alisema bado karafuu ya Zanzibar inahadhi
kwenye soko la dunia na hata bidhaa zake, hivyo iwapo watazikubali karafuu hizo
kununuliwa na ZSTC ubora utapotea.
“Nilipokea maombi kwa wenzangu juu ya
kuzikubali karafuu za nje ya Zanzibar, lakini tunaendela kuzikataa, maana
hazina ubora kama za kwetu’’,alifafanua.
Akizungumzia uhaba wa madaktari kwenye
hospitali na vituo vya afya Dk Shein alisema, hata hao wachache waliopo kazini,
wamekuwa wazito kutekeleza wajibu wao jambo ambalo halileti taswira nzuri
kwenye matibabu.
Alisema utendaji wa kazi wa madaktari
umeshuka kwa kiwango kikubwa, na kisha kujificha kwenye kiza cha uhaba wa
madaktari na kukosekana kwa usimamizi imara.
“Kweli serikali na wizara husika
inaelewa kuwa kuna uhaba wa madaktari Unguja na Pemba, lakini hao waliopo
wamekosa uzalendo na usimamizi haupo wa kutosha’’,alieleza.
Kuhusu maneo kwamba serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar imegomewa na mashirika mbali mbali ya fedha, Rais huyo wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk, Ali Mohamed Shein, amesema
hakuna nchi wala shirika lolote la fedha duniani, lililoigomea Zanzibar katika
kuwasaidia miradi mbali mbali ya maendeleo.
Alisema hakuna, benki yoyote ya
kimatifa ilioiacha mkono Zanzibar na wanaendelea kupokea misaada mbali mbali ya
baadhi ya nchi kadhaa na mashirika mengine huingia Zanzibar kimnya imnya.
Alisema sio sahihi juu ya maneno
yanayosemwa kuwa, wafadhili mbali mbali wa kimataifa wameigomea serikali ya
Zanzibar kutoa ufadhli wao, jambo ambalo sio sahihi hata kidogo.
Alisema bado Zanzibar inaomarafiki wa
kweli, kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya nchi husika na wakati mwengine hata kukopeshwa
fedha kutoka nchi za nje
“Bado marafiki wetu kama ADB, IMF,
Seikali ya China na nyengine wanaendelea kutusaidia kwa kasi kubwa na hata
katika bajeti zilizopita walitusaidia”,alifafanua.
Kuhusu utendaji wa kazi, amewataka watendaji
hao kuziacha ofisi zao na kwenda kwa wananchi moja kwa moja, ili kutambua kwa
kina matatizo yanayowakabili.
“Nampongeza sana Mkuu wa wilaya ya
Chakechake, amekuwa mfano mzuri anakwenda kwa wananchi moja kwa
moja, kujua nini kinachowasibu na wengine waige mfano huo’’,alifafanua.
Katika hatua nyengine rais huyo wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa baraza la Mapinduzi Dk Ali Mohamed Shein, amewataka
watendaji hao kushirikiana kwa karibu na waandishi wa habari ili kutangaaza
kazi wanazozifanya kwa wananchi.
“Waelezeni wananchi mlichokifanya kwa
kuvitumia vyombo vya habari, maana ndio vinavyowaunganisha nyinyi na wananchi,
hawa waandishi msiwakimbie’’,alieleza.
Baadhi ya watendaji hao wa serikali kisiwani
Pemba, wamempongeza rasi huyo wa Zanzibar kwa kufikia mwaka mmoja wa utawala wake
wa kipindi cha awamu ya pili na kuahidi kuendelea kushirikiana nae.
Mkuu wa mkoa wa kaskazini Pemba Omra
Khamis Othaman kwa niaba ya Mkuu wa mkoa
mwenzake wa kusini, alisema wamekuwa na ushirikiano mzuri na maafisa wadhamini,
jambo linalosababisha kurahisisha utendaji wao wa kazi.
Nae Mkuu wa wilaya ya Chakechake
Salama Mbarouk Khatib alisema, kikwazo kikubwa kilichomo ndani ya wilaya yake
kwa sasa, ni kuongezeka kwa migogoro ya ardhi pamoja na uhaba wa madaktari kwa
hospitali zilizomo ndani ya wilaya hiyo.
Kwa upande wake Mdhamini Shirika la
taifa la biashara la ZSTC Pemba, Abdalla Ali Ussi tatizo lililop kwa wakulima
wa zao la karafuu kisiwani humo ni kuibuka kwa wizi wa karafuu.
“Wakulima wamekuwa wakilazimika
kulala kwenye mashamba yao, maana karafuu zikianza kupea huibiwa, sasa hili ni
tatizo maana na sisi ZSTC soko la dunia litashuka hadhi’’,alifafanua.
Dk Shein yupo kisiwani Pemba kwa
zaiara ya siku tano, ambapo pamoja na mambo mengine, anatarajiwa kutembelea
ukarabati wa barabara ya Madenjani- Mzambarau takao, ujenzi wa chuo cha amali
Daya Mtambwe, kuzungumza na waalimu pamoja na kamati za chama.
No comments:
Post a Comment