Habari za Punde

Wizi wa mbegu za muhogo wajitokeza Mkoani Pemba

NA HAJI NASSOR, PEMBA

WAKULIMA wa zao la muhugo wilaya ya Mkoani Pemba, wamelalamikia tabia iliojitokeza kwa kuibiwa mbegu zao za  muhogo, ambapo baadhi yao huiba na muhogo, jambo ambalo linawarejesha nyuma.

Walisema mara baada ya mvua kuanza kunyesha kwa kasi, wapo baadhi ya wenzao, wamekuwa na mtindo wa kukata mbegu na wengine kuiba na muhogo, na kuziuza kwa wakulima wengine.

Wakizungmza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti kufuatia mkulima Mohamed Salim Juma wa Mtuhaliwa kung’olewa visiki vyake vya muhogo 200 alivyovipanda siku moja, walisema hali kwa sasa inatisha.

Walisema imekuwa ni jambo la kawaida hasa baada ya mvua kuanza, kuibiwa mbegu zao au wakati mwengine hata kuibiwa mbegu ambazo tayari zimeshapandwa kabla ya kuanza kuota.

Mmoja kati ya wakulima hao, Mohamed Salim Juma wa Mtuhaliwa, alisema yeye juzi alipofika kwenye shamba lake, aligundua kung’olewa kwa mbegu zake 200 alizokwishazipanda.

Alisema baada ya mvua kuanza, alipigisha matatu kadhaa, na siku ya pili kununua mbegu za muhogo na kuzipanda, ingawa hakuzikuta.

“Visiki vyangu 200 vya muhogo vimeibiwa kimoja baada ya chengine, jamani huu ni kuzidishana umaskini, baada ya kuniibia muhogo, sasa na mbegu mpaka nilizokwisha kuzipanda’’,alilalamika.

Nae Mwamini Haji Ussi wa Mkanyageni alisema, yeye aliibiwa mbegu kwa katwa katwa na kisha watu hao wasiofahamika kung’oa na muhogo robo eka.

“Hata mie ni kweli juzi niliibiwa mbegu na muhogo kwenye shamba langu, maana kipindi hichi cha mvua, kila mmoja anataka kulima, ni kutokana na uhaba wa mbegu’’,alifafanua.
Kwa upande wake Kassim Bendera Vuia wa Mtambile, alisema alilazimika kutoa taarifa kituo cha Polisi Mtambile kufuatia kuibiwa mbegu zake zaote.

“Mimi niliibiwa mbegu tu, lakini muhogo wala haukung’olewa, na bahati nzuri, nilizikamata eneo la Jiondeni Mkoani, ingawa mwizi sikumjua’’,alinifahamisha.

Alifafanua kuwa, alipotaka taarifa za ndani juu ya wapi mbegu hizo mnunuaji huyo amezipata, alimueleza kuwa alinunua eneo la Mizingiani njia ya Wambaa, ingawa baada ya kufuatilia aligundua kuwa ndie aliefanya hivyo ni jirani yake.

Mwananchi Bakari Haji Bakari wa Kengeja, alisema wamekuwa wakati mwengine wakilinda mashamba yao kwa kwenda mapema na kuchelewa kurudi kwa kuhofia wizi wa mbegu.

Sheha wa shehia ya Mtambile Rajab Risasi, alisema hayajapokea taarifa zozote za wizi wa mbegu, na kuitaka jamii kuendelea kukinawirisha kikosi cha polisi jamii.


Katika wiki tatu sasa tokea kuanza kwa msimu huu wa mvua, kumekuwa kikiibuka malalamika kila siku, kutokana na wakulima wa zao la muhugo kuibiwa mbegu na muhogo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.