Habari za Punde

Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein, Atembelea Kituo cha Watoto Djibout.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Djibouti                                                          9.05.2017
---
MKE wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein ameeleza kuwa Wanawake wana nafasi kubwa ya kusimamia na kuendeleza Sera na Mipango ya Serikali ya kuendeleza na kusimamia wa wanawake na watoto.

Mama Shein aliyasema hayo kwa nyakati tofauti katika hotuba yake aliyoitoa mara baada ya kutembelea Kituo cha Watoto pamoja na Makao Makuu ya Kitaifa ya Wanawake wa Djiboti vyote vilivyopo mjini Djibouti.

Katika hotuba yake, Mama Shein alisema kuwa katika ziara yake hiyo amefurahishwa kwa kiasi kikubwa kuona juhudi za makusudi zinazochukuliwa na Serikali ya Djibouti katika kuwawezesha wananwake sambamba na kuwatunza watoto.

Aliongeza kuwa amepata kujifunza mambo mengi ambayo yanawapasa akina mama na watoto katika maendeleo yao utoaji wa elimu na mafunzo mbali mbali wanayopewa wanawake ambayo baada ya kumaliza huweza kuyafanyia kazi na kuweza kujiajiri wenyewe huku watoto nao wakipata mafunzo ambayo huwaendeleza katika maisha yao.

Aidha, Mama Shein alisema kuwa umefika wakati kwa Wanawake wa Zanzibar kushirikiana na kufanya kazi kwa pamoja na wanawake wa Djibouti kwa lengo la kuwaendeleza wanawake kiuchumi, usawa wa kijinsia pamoja na haki za watoto.

Alisisitiza kuwa ni vyema kwa kila mmoja kwa pande mbili hizo kulifanyia kazi suala hilo ili kuhakikisha linafanikiwa.

Pamoja na hayo, Mama Shein alieleza haja ya kuwepo kwa ziara mbalimmbali za kubadilishana uzoefu na utaalamu kati ya viongozi wa kike wa Zanzibar na wa Djibouti.

Sambamba na hayo, Mama Shein alitoa pongezi na shukurani za pekee kwa Rais wan chi hiyo Ismail Omar Guelleh kwa mwaliko wake aliofanya kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kutembelea nchi hiyo hatua ambayo itazidisha na kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya pande mbili hizo.

Pia, Mama Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa wananchi na viongozi wote wa Djibouti wakiwemo viongozi wanawake wan chi hiyo kwa moyo wao mzuri waliouonesha katika mapokezi makubwa ya ujumbe wa Zanzibar ulioongozwa na Rais Dk. Shein nchini humo na kueleza faraja yake kwa hatua hiyo.

Nao viongozi wa vituo hivyo walimueleza Mama Shein hatua wanazozichukua katika kuhakikisha watoto wanatunzwa na kuendelezwa kielemu na kijamii pamoja na kumueleza hatua zinazochukuliwa katika kuwawezesha na kuwaendeleza wanawake nchini humo.

Katika ziara hiyo Mama Shein amefuatana na Rais Dk. Shein pamoja na viongozi mbali mbali wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ziara ambayo inatokana na mwaliko wa Rais wa nchi hiyo, Rais Ismail Guelleh kwa Dk. Shein.

Miongoni mwa viongozi aliofuatana nao Dk. Shein ni Mama Shein, Waziri wa Ujenzi Mawasiliano na Usafiri, Baalozi Ali Karume, Waziri wa Afya Mahmoud Thabik Kombo, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dk. Susan Alphonce Kolimba.

Wengine ni Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Uwekezaji Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA) Salum Khamis Nassor, Mshauri wa Rais Masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Uchumi na Uwekezaji, Balozi Mohammed Ramia Abdiwawa pamoja na watendaji wengine wa Serikali.
Rais Dk. Shein anatarajiwa kurejea nchini Mei 10 2017.
 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.