Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (katikati) akizungumza na wajumbe wa Baraza la Wauguzi na Wakunga la Zanzibar walipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo,[Picha na Ikulu.] 08/06/2017.
Baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wauguzi na Wakunga la Zanzibar walipokuwa wakimsikiliza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (hayupo pichani) alipozungumza nao leo walipofika Ikulu Mjini Zanzibar,[Picha na Ikulu.] 08/06/2017.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Baraza la Wauguzi na Wakunga la Zanzibar pamoja na Viongozi wengine baada ya mazungumzo yalitofanyika katika ukumbi wa Ikulu Mjini Zanzibar leo,[Picha na Ikulu.] 08/06/2017.
STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 08.06.2017
RAIS wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ametoa wito kwa Baraza
la Wauguzi na Wakunga la Zanzibar kusimamia vyema Sheria ya Baraza hilo
sambamba na maadili kwa lengo la kuwahudumia vyema wananchi na kuzifanya huduma
za afya zizidi kuimarika na kuendelea kuijengea sifa Zanzibar kama ilivyokuwa
hapo siku za nyuma.
Dk.
Shein, aliyasema hayo leo wakati alipokuwa na mazungumzo na Wajumbe wa Baraza
la Wauguzi na Wakunga waliofika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya
kujitambulisha kwa Rais wakiwa wameongozana na uongozi wa Wizara ya Afya chini
ya Waziri wa Wizara hiyo Mahmoud Thabit Kombo.
Katika
maelezo yake Dk. Shein aliwaeleza Wajumbe hao haja na umuhimu mkubwa wa
kuipitia na kuisoma vyema vifungu vyote na hatimae kuifanyia kazi Sheria ya
Baraza la Wauguzi na Wakunga la Zanzibar ya mwaka 2014 ili waweze kuliongoza
vyema na kwa ufanisi zaidi Baraza hilo.
Dk.
Shein, alisema kuwa iwapo Sheria hiyo itasimamiwa vyema fani ya Uuguzi itaendelea kuwa na mafanikio
makubwa sana hapa Zanzibar.
Alieleza
matumaini yake makubwa kwa wajumbe hao ambao wamechaguliwa kutokana na kuwa kazi
hiyo wanaiweza na kuwapongeza kwa kufanya mambo mengi tokea kuzinduliwa Baraza
hilo lenye Wajumbe 13 Mrajis na wasaidizi wake wawili mmoja Pemba na mmoja
Unguja mnamo mwezi June mwaka 2015.
Aidha,
Dk. Shein alisisitiza suala zima la maadili ambalo ndio jambo muhimu katika
fani yoyote duniani na kueleza kuwa katika fani ya Uuguzi suala la maadili ndio
jambo la kulipa kipaumbele ili kuweza kutoa huduma nzuri ya afya kwa jamii.
Sambamba
na hayo, Dk. Shein alieleza umuhimu wa kuwepo kwa usimamizi katika suala zima
la uuguzi kwani hatua hiyo itaipelekea Zanzibar iweze kutajika na kuirudisha
katika hali yake ya zamani ambapo wananchi kutoka ndani na nje ya Zanzibar
walikuwa wakija hapa nchini kufuata huduma za afya.
Akieleza
suala zima la upungufu wa wauguzi, Dk. Shein alisema kuwa upungufu wa wauguzi
ni suala la muda mrefu na kusisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
itaendelea na juhudi zake za kuhakikisha inatatua changamoto hiyo hatua kwa
hatua.
Dk.
Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Baraza hilo kwa hatua yake ya
kusimamia vyema suala la mafunzo kwa wauguzi ambapo tayari kwa maelezo ya
Wajumbe hao kuna wauguzi 893 wenye Diploma ya Uuguzi, 97 wenye Digirii ya
Kwanza, 25 wenye Digrii ya Pili na 1 anaefanya Shahada ya Uzamivu (Phd) katika kada
hiyo.
Aliongeza
kuwa kwa kutambua umuhimu wa kada hiyo, Baraza lina kazi kubwa ya kuteua Kada
muhimu za mafunzo katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) sambamba na
wajibu mkubwa wa kusimamia utafiti.
Katika
kutilia mkazo jambo hilo, Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
chini ya uongozi wake imeamua kwa makusudi kuanzisha Taasisi ya Utafiti ya Afya
kwa kutambua kuwa utafiti husaidia kutoa huduma bora za matibabu katika sekta
ya afya.
Mapema
Waziri wa Wizara ya Afya Mahamoud Thabit Kombo
alieleza kuwa mkutano kati ya Rais pamoja na Baraza hilo umekuja wakati
muwafaka ambapo Wizara yake imeahidi mambo mbali mbali katika Baraza la
Wawakilishi linaloendelea na kwa mashirikiano ya pamoja kati ya Wizara na
Baraza hilo yanaweza kutekeleza kile alichokiahidi katika Baraza hilo hivi
karibu katika Bajeti yake.
Waziri
Kombo alieleza miongoni mwa changamoto ni pamoja na kuwekwa pembeni maadili ya
uuguzi, lugha isiyofaa zidi ya wagonjwa, wagonjwa kutozwa fedha za dawa ambazo
zipo hospitalini na zimenunuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa ajili
yao mambo ambayo ameahidi kuyavalia njuga katika kupambana nayo kwa
mashirikiano na Baraza hilo.
Nae
Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee
alieleza haja ya kujua mahitaji ya wauguzi pamoja na upangaji wa wauguzi katika
hospitali za hapa nchini kwani licha ya kuwepo kwa idadi ndogo ya wauguzi lakini
suala zima la usimamizi limekuwa likikosekana katika eneo hilo kama ilivyo kwa
taasisi nyengine za Serikali.
Dk.
Abdulhamid alisisitiza kuwa licha ya Utumishi kufanya juhudi za makusudi katika
sekta ya afya lakini kinachoonekana ni kuwa wengi wanaoajiriwa katika sekta
hiyo hufanya kazi kinyume na ajira yao na ndipo unapotokea upungufu wa
wafanyakazi huku akieleza kuwa ni vyema mafunzo yakawa yanaleta mabadiliko ya
kiutendaji kwa watendaji wa kada hiyo ya Uuguzi pamoja na kada nyengine ndani
ya taasisi za Serikali.
Nae
Mwenyekiti wa Baraza hilo Bi Amina Abdulkadir Ali alitumia fursa hiyo kutoa
historia kwa ufupi ya Baraza hilo hapa Zanzibar pamoja na hatua, utekelezaji na
maendeleo ya kazi za Baraza sambamba na mafanikio na changamoto zilizopo.
Akitaja
miongoni wma mafanikio, Bi Amina aliseama kuwa ni pamoja na kupata ofisi na
vitendea kazi, kuweza kufungua akaunti,kudumisha mashirikiano na Wauguzi wa
Tanzania Bara pamoja na wale wa nchi za Afrika ya Mashariki na Jumuiya za
Kimataifa.
Aliongeza
kuwa kuweza kuwachukulia hatua kwa onyo au kusimamisha kwa wauguzi waliokuwa na
makosa ya maadili na kosa la kughushi vyeti, idadi ya wanafunzi wanaotaka
kusoma Uuguzi imeweza kuongezeka ikilinganishwa na miaka miwili iliyopita
sambamba na kuadhimisha Siku ya Wauguzi Duniani tarehe 12, Mei mwaka huu huko
Pemba kwa pesa za Baraza kupitia Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar bila ya
kuwahusisha wahisani.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment