Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk Shein Amewataka Wajumbe wa Bodi Kuzipa Kapaumbele Sheria Tatu Muhimu.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                               31.07.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza haja ya kuzifahamu vyena na kuzifanyia kazi sheria zilizounda Bodi za Wakurugenzi za Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji ili Bodi hizo ziweze kufanya kazi kwa ufanisi sambamba na kuimarisha mashirikiano kati ya Bodi na Wizara.

Dk. Shein aliyasema hayo Ikulu mjini Zanzibar kwa nyakati tofauti wakati alipokutana na uongozi wa Wizara  hiyo pamoja na Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Usafiri Baharini na Uongozi wa Mamlaka ya Usafiri Baharini, Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Bandari na Uongozi wa Shirika la Bandari pamoja na  Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Meli na Uongozi wa Shirika hilo.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alieleza kuwa mafanikio makubwa yatapatikana katika kufikia malengo yaliokusudiwa iwapo sheria zilizopo zinazoziongoza Bodi hizo zitafanyiwa kazi vizuri kwa lengo la kutekeleza mambo muhimu yaliokusudiwa.

Aidha, Dk. Shein alisisitiza haja kwa uongozi wa Bodi hizo kuzipa kipaumbele Sheria tatu muhimu ikiwemo Sheria namba 1 ya mwaka 1997, Sheria namba 2 ya mwaka 2001 na Sheria namba 4 ya mwaka 2002, ili ziwe Dira katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Dk. Shein alisisitiza haja ya kushirikiana na kupendana kwa wafanyakazi wa Bodi hizo, Mamlaka na Mashirika, pamoja na viongozi wa Wizara hiyo ili kutimiza azma ya kuleta maendeleo na kukuza uchumi wa nchi.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alieleza umuhimu kwa Bodi hizo za Wakurugenzi wa kutoa taarifa kwa Serikali kupitia Wizara hiyo ili mipango inayopangwa iweze kuleta tija huku akitumia fursa hiyo kupongeza mafanikio makubwa yaliopatikana katika Mamlaka ya Usafiri Baharini, Shirika la Bandari pamoja na Shrika la Meli.

Aliongeza kuwa kazi za Bodi sio kulumbuna ama kupambana na Wizara bali ni kushirikiana na Wizara katika kuhakikisha mipango ya maendeleo iliyopangwa inakwenda vyema kwa lengo la kuleta manufaa kwa taifa na jamii kwa ujumla.

Aidha, alieleza kuwa ni lazima ifahamike kuwa Bodi hizo za Wakurugenzi, Mamlaka na Mashirika yaliomo katika Wizara hiyo yote hayo ni ya Serikali, hivyo ni vyema yakafuata taratibu, kanuni na sheria ziliopo ambazo zimewekwa na Serikali na kuepuka kujipangia mambo wenyewe.

Dk. Shein Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa uongozi wa Bodi hizo, Mashirika na  Mamlaka  ya Usafirishaji na uongozi wake pamoja na uongozi wa Wizara hiyo kwa mafanikio makubwa yaliopatikana sambamba na mabadiliko makubwa yaliyofanywa katika kuhakikisha yanasaidia katika kuimarisha uchumi wa nchi.

Nae Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, alipongeza juhudi zinazochukuliwa na Bodi hizo, Mamlaka pamoja na Mashirika hayo yaliyomo katika Wizara hiyo na kusisitiza haja ya kuweka mikakati maalum ya kutambua mizigo inayopitishwa katika Bandari ya Zanzibar ili kuepuka bandari hiyo kufanywa njia ya kupitishwa bidhaa zisizofaa.

Waziri wa Wizara hiyo Balozi Ali Karume alitumia fursa hiyo kueleza mashirikiano mazuri yaliopo kati ya uongozi wa Wizara, Bodi na wafanyakazi wake huku akieleza,

Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alieleza kuwa lengo la kuundwa kwa Mamlaka na Mashirika ya Serikali ni kuchangia mapato katika Mfuko Mkuu wa Serikali hivyo ni vyema juhudi zikachukuliwa katika kuhakikisha hilo linafanikiwa.

Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Said Hassan alisisitiza haja ya Uongozi wa Bodi hizo za Wakurugenzi kuendelea kushirikiana vyema na Ofisi yake huku akieleza umuhimu wa ukaguzi kwa meli za ndani.

Aliongeza kuwa mbali ya kujua sheria za zilizopelekea kuundwa kwa Bodi hizo ni vyema wajumbe na viongozi husika wakazitambua sheria nyengine ili ziweze kuwarahisishia kazi zao ikiwemo Sheria namba 2 ya mwaka 2002.  

Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Mustafa Aboud Jumbe alitumia fursa hiyo kutoa historia ya Uanzishwaji wa Mamlaka pamoja na Mashirika na hatimae Bodi hizo

Nao Wakurugenzi Wakuu wa Wizara hiyo walieleza mafanikio yaliopatikana sambamba na mashirikiano mazuri yaliopo kati yao na Bodi za Wizara hiyo hatua ambayo imepelekea kuweza kupiga hatua kubwa ya maendeleo ya kiuchumi katika sekta ya huduma ya usafiri na usafirishaji.

Wenyeviti wa Bodi hizo kwa nyakati tofauti walieleza mafanikio makubwa yaliopatikana sambamba na changamoto zilizopo ambazo walieleza kuwa zimo katika hatua za kupatiwa ufumbuzi huku wakiahidi kuendeleza mashirikiano yaliopo kati yao na uongozi wa Wizara.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.