Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk Shein Azungumza na Uongozi wa Wizara ya Ardhi na Bodi ya ZURA na ZAWA Ikulu leo.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                            03.07.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza matumaini yake makubwa kwa kuundwa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati Zanzibar (ZURA) na kuanza kazi zake vyema tena kwa muda mfupi na kueleza kuwa kazi za Mamlaka hiyo zitaenda vizuri iwapo wataenda sambamba na sheria ya Mamlaka hiyo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzbar wakati alipokutana na uongozi wa Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira pamoja na Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma ya Maji na Nishati Zanzibar (ZURA) na Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA).

Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa Mamlaka ya ZURA imeweza kuleta matumaini makubwa katika kutatua changamoto kadhaa zilizokuwepo hapo siku za nyuma katika suala zima la uhaba na upandishaji wa bei ya mafuta kiholela uliokuwa ukitokea na kuleta usumbufu kwa wananchi.

Hivyo, aliitaka ZURA kuendelea na kasi na ari waliyonayo ya utendaji wa kazi na kusisitiza haja ya kuiangakia kwa umakini sheria ya Mamlaka hiyo kwani ina mambo mengi ya msingi yanayoigusa Bodi, Wizara na Jamii.

Dk. Shein alieleza kuwa kwa upande wa wananchi wanapaswa kuijua na kuitambua ZURA na kazi zake ili kuweza kupeleka malalamiko yao hasa katika suala zima la bei ya mafuta.

Nae Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, alitoa pongezi kwa ZURA na Bodi yake na kueleza haja ya kuangalia ujenzi wa vituo vya kuuzia mafuta kwa kufuata sheria na taratibu za ZURA.

Waziri wa Wizara hiyo Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Salama Aboud Talib, alipongeza mashirikiano yalipo kati ya Wizara na Bodi hiyo huku akieleza changamoto iliyopo katika suala zima la ujenzi wa vituo vya kuuzia mafuta ambao ujenzi wake umekuwa haufuati taratibu.

Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alieleza haja ya kutafutwa sehemu mbadala ya eneo la kuhifadhia mafuta liliopo Mtoni ambalo kwa hivi sasa liko karibu sana na maakazi ya wananchi.

Aidha, alisema kuwa tayari eneo la Mtoni miundombinu yake imechakaa ambapo pia, meli za mafuta hivi sasa haziwezi tena kufika katika eneo hilo sambamba na kueleza umuhimu wa kuwepo utaratibu wa kuuza maji kwa magari ambayo hupeleka mahotelini kwani hiyo ni rasilimali ya Serikali.

Pia, Dk. Abdulhamid aliitaka ZURA kushirikiana na vyombo vya ulinzi katika kupambana na wauza mafuta ya magendo.

Nao uongozi wa ZURA ulieleza kuwa juhudi zimekuwa zikichukuliwa katika kulitafutia ufumbuzi suala zima la miundombinu ya vituo vya mafuta ambavyo vingi vimekuwa na vifaa vichakavu.

Wajumbe wa Bodi ya ZURA walimueleza Rais kuwa tokea kuanza kwa kazi kwa ZURA suala la kuwepo kwa uhaba wa mafuta mara kwa mara limeondoka sambamba na lile la wafanyabiashara kupandisha bei ya mafuta kiholela.

Walieleza kuwa kwa hivi sasa wameweza kujipanga vizuri na kupelekea kuongeza mapato na kueleza mpango wao wa kutekeleza miradi mikubwa ukiweo wa ujenzi wa ofisi zitakazojumuisha ofisi za Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira pamoja na ujenzi wa bandari kwa ajili ya shughuli za mafuta na gesi huko Mangapwani.

Aidha, Mamlaka ya ZURA imeleeza mipango yake ya kutaka kubadilisha mfumo wa uletaji mafuta hapa nchini ambapo mafuta yataletwa moja kwa moja hapa Zanzibar hali ambayo itasaidia kushuka kwa bei ya mafuta na kuweza kuwasaidia wananchi.

Pia, uongozi huo wa Mamlaka ya ZURA ulieleza kuwa tayari kumejitokeza Makampuni kadhaa yanayotaka kushirikiana na Mamlaka hiyo katika ujenzi wa Bandari huko Mangwapwani katika eneo maalum lililotengwa kwa ajili ya bandari pamoja na eneo kwa ajili ya mafuta na gesi.

Sambamba na hayo, ZURA ilieleza azma yake ya kulishughulikia suala zima la maji na umeme ambalo limo katika majukumu yao kisheria ili wananchi wapate kuzitumia vyema huduma hizo huku wakieleza mashirikiano yao yaliopo kati yao na Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji Tanzania (EWURA).

Wakati huo huo, Dk. Shein alikutana na uongozi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA), uongozi wa Wizara husika pamoja na Bodi ya Mamlaka hiyo na kutaka kuzitafutia ufumbuzi changamoto zilizopo hasa katika suala zima la upatikanaji wa maji.

Dk. Shen pia, alieleza namna Serikali inavyoangalia haja ya kuyahifadhi maji kwani maji yamekuwa yakipotea ovyo hasa mara baada ya kumalizika kunyesha kwa mvua huku akiitaka ZAWA, Bodi, Uongozi wa Wizara kuijua Sheria na kuifanyia kazi.

Nae Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd, alieleza umuhimu wa kutafuta ufumbuzi wa malalamiko ya upatikanaji wa maji katika maeneo kadhaa ya wananchi hapa nchini.

Mkurugenzi Mkuu wa ZAWA Mustafa Ali Garu alieleza jitihada zinazochukuliwa na ZAWA ikiwa ni pamoja na kuendeleza miradi mikubwa ukiwemo Mradi chini ya ufadhili wa Serikali ya China, Mradi wa ADB, Serikali ya India ambao umo katika matayarisho, pamoja na Mradi kutoka Serikali ya Japan kupitia Shirika lake la misaada la JICA.

Alisema kuwa visima katika mradi wa ufadhili wa China unaenda vizuri katika maeneo mbali mbali kama vile Donge, Chaani, Pangeni na maeneo mengine ambayo tayari miudombinu ya maji imeshaanza kuwekwa.

ZAWA ilieleza kuwa mapato yameongezeka kwa kiasi kikubwa lakini hata hivyo bado wanahitaji kujiimarisha katika kuongeza mapato hayo na kueleza kuwa hilo linawezekana iwapo jitihada zaidi zitafanyika.

Alieleza kuwa hali ya maji yaliopo Zanzibar ni ya kutosha na kueleza jinsi ilivyohuwika hasa katika kipindi kilichopita cha mvua za masika ambapo maji yameweza kuongezeka kwa kiasi kikubwa.

Dk. Garu alieleza changamoto zilizopo ambazo ni pamoja na upotevu wa maji huku akieleza kuwa hali ya miundombinu chakavu nayo hipo lakini jitihada zimekuwa zikifanyika katika kuodoa tatizo hilo kupitia miradi husika.

Nao Wajumbe wa Bodi ya ZAWA walieleza ponhezi zao kwa Rais kwa kuwepo kwa mradi wa Ras-el kheiman ambao kukamilika kwake kutatatua changamoto kubwa ya maji kwa upande wa Unguja na Pemba.

Walieleza changamoto zilizokuwepo ikiwa ni pamoja na kuwepo kwa miundombinu chakavu na kuongeza kuwa Mita za kawaida hazijaweza kutosheleza ambapo bado kuna wateja wengi wanaohitaji huduma hiyo kuipata.

Uongozi wa Wizara kwa upande wake ulieleza juhudi, malengo na mikakati liyoiweka katika kuhakikisha changamoto ya sekta ya maji inapatiwa ufumbuzi huku ikiitaka jamii kuitumia vyema rasilimali hiyo iliyopo kwa kuihifadhi vyema pamoja na vianzio vyake.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.