Habari za Punde

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                                                                              22.07.2017
---
WANANCHI katika Mkoa wa Kusini Pemba wameelezea kufurahishwa kwao kutokana na utekelezwaji wa ahadi mbali mbali zilizotolewa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein na kutoa wito kwa viongozi wengine wa kisiasa kuiga mfano huo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika mahojiano maalum baada ya kukabidhiwa mashua mbili za kuvushia wananchi kutoka kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, wananchi wa Kisiwa Panza na Chokocho katika Wilaya ya Mkoani, wameeleza kuwa wamekuwa wakishuhudia mabadiliko makubwa ya kimaendeleo katika Wilaya yao kwenye sekta mbali mbali za kiuchumi na kijamii ndani ya kipindi cha miaka sita iliyopita.

Wamesema sehemu kubwa ya maendeleo hayo yanatokana na utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015 – 2020, ahadi zilizotolewa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi wakati wa kampeni za uchaguzi wa mwaka 2010-2015 na 2015-2020 na ahadi alizozitoa wakati wa ziara zake katika nyakati tofauti Wilayani humo.

Mkuu wa Wilaya ya Mkoani Hemed Suleiman Hemed amesema tatizo la usafiri wa baharini kwa wananchi wa vijiji vya Kisiwa Panza na Chokocho ni la muda mrefu lakini limezidi kuwa kubwa mara baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, ambapo wanaomiliki vyombo vya usafiri waliamua kutoa huduma kwa ubaguzi kwa kuzingatia misingi ya kisiasa.

Faki Mohamed Khamis na Khamis Juma Othman wamesema kuwa kwa miaka mingi viswa hivyo havijawahi kushuhudia hatua kubwa za maendeleo ya muda katika kipindi kifupi kama ilivyo mara hii ambapo huduma za maji safi na salama, umeme na elimu zimeimarika zaidi.

Kauli kama hiyo pia, imetolewa na Bi Mwamize Vuai Haji na Chum Abdalla ambao wamesema wanajivunia huduma hizo, huduma ya usafiri wa baharini ambayo imetolewa hivi karibuni na Dk. Shein na ujenzi wa ukuta unaozuia maji ya chumvi yanayoingia kwenye makaazi ya watu kutokana na mabadiliko ya tabia nchi.

Uamuzi wa kununua mashua hizo zilizogharimu shilingi milioni 27, ulichukuliwa na Rais Dk. Shein kufuatia malalamiko ya wananchi wa Kisiwa Panza na Chokocho, ambao walimuelezea kilio chao kutokana na usumbufu mkubwa wanaoupata wa usafiri hasa baada ya huduma hiyo kuanza kutolewa kwa njia za kibaguzi.

Akikabidhi mashua hizo kwa niaba ya Rais Dk. Shein, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum Mheshimiwa Haji Omar Kheir amesema mashua hizo ambazo zitakuwa chini ya usimamizi wa Kikosi maalum cha kuzuia magendo zitatoa huduma chini ya misingi ya usawa bila ya kujali rangi, dini wala chama cha siasa kama ilivyotokezea hapo siku za nyuma kwa kubaguliwa kwa wananchi wanaotoka chama fulani.

Akizungumza kwenye sherehe za kukabidhi mashua hizo, Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba Mwanajuma Majid amesema kilio cha wananchi wanaoishi kisiwa Panza na Chokocho kitaondoka baada ya mashua hizo kuanza kazi rasmi hivi karibuni.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.