STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Pemba 23.08.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, amesema kuwa lengo la
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar la kuliimarisha zao la karafuu ni
kuwaneemesha wakulima wa zao hilo na kuwafanya wawe na maisha bora zaidi kuliko
ilivyo sasa.
Amesema mipango ya kuliongezea thamani zao hilo
pamoja na kuyatambua mashamba ya Serikali inalenga kuwaongezea kipato wananchi
pamoja na kuwaweka utaratibu mzuri ambao baadae utawafanya wanaoyatumia vyema
na kwa uadilifu mashamba hayo kuweza kumilikishwa.
Dk. Shein aliyasema hayo leo mara baada ya kushiriki
kikamilifu katika shughuli za uchumaji na uchambuaji wa karafuu huko katika
kambi ya Karafuu ya Mshashani ya mkulima Mohammed Kai Bakari iliyopo Kifundi,Wilaya
ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba.
Amesema utaratibu wa sasa ambapo wakulima wa
karafuu wanauza karafuu zao Shirika la Taifa la Biashara (ZSTC) kama zilivyo
baada ya kukaushwa na ZSTC kuuza kwenye soko la dunia, haziipi faida kubwa
serikali wala mkulima kuliko ambavyo zao hilo lingeongezwa thamani.
Kutokana na hali hiyo, Dk. Shein amesisitiza kuwa
tafiti zitaendelea kufanywa kwa lengo la kuliongezea thamani zao hilo la
karafuu na kuna haja ya wanasayansi waongeze kasi katika kuliongezeza thamani
zao hilo.
Aidha, amesema mchakato wa sasa ambao serikali
unaendelea nao wa kuyatambua mashamba yake hatimaye utaweka utaratibu mzuri wa
kuwamilikisha wakulima wanaoyatumia vizuri.
Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar imefanya uwamuzi wa makusudi wa kuliongezea bei zao hilo kwa lengo la
kulipa heshima zao la karafuu.
Aliongeza kuwa Serikali haina nia wala lengo la
kuwanyanganya wakulima mashamba ya karafuu kama inavyoelezwa na baadhi ya watu
wachache bali ina mpaongo wa kuyatambua mashamba yake yote ya karafuu pamoja na
eka za serikali.
Dk. Shein alieleza kuwa kila mwenye haki ya kupewa
shamba ama heka atapewa kwa taratibu zitakazopewa na wale wenye kuyashughulikia
mashamba hayo hivi sasa watapewa kipaumbele.
Nae Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi
Hamad Rashid Mohamed alitoa shukurani kwa Rais Dk. Shein kwa kushiriki vyema
katika shughuli ya uchumaji na uchambuzi wa karafuu.
Aliongeza kuwa ukulima wa zao la karafuu ni mgumu
hivyo hatua za serikali za kuwaongezea wakulima beo za zao hilo na kutoa agizo
kuwa asilimia 80 ya bei ya dunia walipwe wakulima ni mfano mzuri wa kuonesha
kuwa Rais Dk. Shein na Serikali anayoiongoza inawajali wakulima.
Mapema Dk. Shein alipata maelezo juu ya
ukodishwaji wa zao hilo la karafuu ulioanza tarehe 5 mwezi huu na tayari
mashamba 100 yameshakodishwa yenye thamani ya TZS 158.9.
Shamba la mzee Mohammed Bakari Kai lima mikarafuu
125 bado halijakodoshwa lakini wakati ukifika wa ukodishwaji kipaumbele
kitawekwa kwa msimamizi wa shamba hilo ambaye ni mkulima maarufu na mwenye sifa
za kilimo ambaye aliwahi kupewa zawadi ya mkulima bora hapo mwaka juzi.
Balozi Ali Karume ambaye ni Kaimu Waziri wa
Bishara, Viwanda na Masoko alieleza haja ya kulithamini zao hilo kwani ni zao
la uchumi hapa nchini.
Nae mkulima huyo Mohammed Kai alitoa pongezi kwa
Rais Dk. Shein kwa hatua yake ya kufika katika shamba na hatimae katika kambi
yake na kujionea shughuli za kambini hapo na kuungana na wakulima kwa kuchambua
karafuu.
Mkulima huyo alieleza anavyofarajika na juhudi za
Dk. Shein chini ya Serikali anayoiongoza katika kuliimarisha zao hilo la
karafuu huku akieleza uzoefu wake katika kilimo cha karafuu pamoja na zawadi
alizowahi kupewa kutokana na ukulima wake.
Mapema Dk. Shein aliweka jiwe la Msingi katika
Skuli ya Chiba na kueleza azma ya Serikali ya kuiendeleza skuli hiyo ili watoto
wapate fursa ya kusoma na kuondoa tatizo la kwenda skuli za mbali na makaazi
yao.
Dk. Shein aliwapongeza wazee pamoja na Mfuko wa
Halmashauri kwa juhudi kubwa walizozichukua katika ujenzi wa madarasa manne ya
skuli hiyo pamoja na ofisi za mwalimu mkuu ambapohadi kufikia hatua hiyo ujenzi
umegharimu TZS milioni 37.3.
Aidha, aliwataka watoto wa Chimba wasome kwa
juhudi kubwa na kuwasisitiza kuwa Chimba itajengwa na wanachimba wenyewe.
Aidha, aliwata walimu kuwasomesha watoto vyema na
wasichanganye elimu na siasa wala wasisomeshe kwa kuwababaisha kwani lengo ni
kuwapa elimu bora watoto wote.
Pamona ja hayo, Dk. Shein aliwahakikishia wananchi
wa Chimba kuwa barabara yao yenye urefu wa kilomita 8.9 itajengwa kwa kiwango
cha lami.
Akiwa katika ziara hiyo Dk. Shein aliweka jiwe la
msingi katika Tawi la CCM Njuguni na baadae kupigisha harambee kwa lengo la
kumaliza ujenzi wa Tawi hilo ambapo zilipatikana fedha zote milioni saba ambapo
yeye alichangia milioni mbili.
Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa ujenzi
wa matawi ya chama ni njia moja wapo ya kukiimarisha chama hicho na hatimae
kuweza kuongeza wanachama na kuweza kufanya vyema shughuli za chama kwa ufanisi
zaidi.
Kabla ya hapo Dk. Shein alipokea taarifa ya Mkoa
wa Kaskazini Pemba hapo katika ukumbi wa Chuo Kikuu cha Taifa SUZA,
Mchangamdogo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment