Habari za Punde

196 waanguka kutoka juu ya mikarafuu Pemba


NA HAJI NASSOR, PEMBA

WANANCHI wawili kisiwani Pemba, wameripotiwa kufariki dunia, baada ya kuanguka kutoka juu ya mkarafuu, kati ya wananchi 196 walioanguka, baina ya msimu wa mwaka 2015 hadi mwanzoni mwaka huu.

Akizungumza na wadau wa zao la kafaruu, Mdhamini wa Shirika la Taifa la Biashara Zanzibar ‘ZSTC’ Pemba Abdalla Ali Ussi, kwenye mafunzo ya haki za binadamu, yaliofanyika mjini Chakechake, alisema waliopewa fidia katika kipindi hicho, walikuwa 147, ambapo baadhi hawakupewa kutokana na sababu mbali mbali.

Alisema katika kipindi hicho shilingi milioni 130 zilitumika kupitia Shirika la Bima Zanzibar, kwa ajili ya kuwalipa fidia wananchi hao walioanguka mikarafuu na wengine kufariki.

Alisema kwa msimu wa mwaka 2015 hadi 2016, wananchi walioanguka mikarafuu walikuwa 113, ambapo kati ya hao 108 pekee ndaio waliolipwa fidia, sawa na shilingi milioni 100 na waliobakia, hawakulipwa kutokana na kuwa nje ya vigizo na utaratibu wa Shirika husika.

Aidha Mdhamini huyo wa ZSTC, alisema msimu mwa mwaka 2016/2017 uliomalizika, kulikuwa na wachumaji wa zao la karafuu 63 walioanguka kutoka juu ya mkarafuu, na kuripoti kwenye vyombo husika na 39 tu ndio waliolipwa, sawa na shilingi milioni 30, huku wengine wakikosa malipo hayo kwa vile wanaendelea na matibabu.

Alieleza kuwa, kazi ya kufanya tathimini, kuangalia vipimo vya kiwango cha fedha kwa muangukaji wa mkarafuu, hufanywa na Shirika la Bima Zanzibar, ambapo ZSTC hutoa fedha hizo kila msimu.
‘Sisi kila msimu ndio tunawapa fedha wenzetu wa Shirika la Bima, lakini suala la kutoa fedha na viwango husika, jukumu hilo bado wanalo wenyewe Bima”, alifafanua.

Katika hatua nyengine, Mdhamini huyo wa ZSCT Pemba, aliwataka wananchi kuacha tabia ya kuhifadhi karafuu zao majumbani, kwani zinatabia ya kupungua uzito kila baada ya muda.

“Mkizihifadhi zinapungua uzito, na kama mnataka kuziweka basi njooni ZSTC mchukue kibali au museme muhifadhiwe, lakini usikae nazo nyingi bila ya kufuata taratibu zinavyoelekeza”, alifafanua.

Akiwalisha ufafanuzi wa sheria ya no 2 ya mwaka 2014 ya maendeleo ya karafuu, Afisa Mipango wa ZLSC tawi la Pemba, Mohamed Hassan Ali, alisema sheria hiyo imefanyiwa marekebisho na kueleza maana ya magendo na aina zake.

Mapema akifungua mafunzo hayo, Mratibu wa Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar ZLSC tawi la Pemba, Fatma Khamis Hemed, alisema kituo kimekuwa na mpango wa kuyawezesha makundi kadhaa kitaaluma, ili yafahamu sheria.

Alisema wadau hao wa zao la karafuu, ni moja kati ya hao wengi, ambapo iwapo watakuwa makini kwenye mafunzo hayo, wataweza kuwaleimisha wenzao.

Wakichangia mada kadhaa washiriki hao, walisema bado jamii haijaelimishwa vya kutosha juu ya kanuni na sheria za karafuu, hali iliopelekea wananchi kuhisi wanaonewa juu ya maamuzi mbali mbali ya serikali.


Katika mafunzo hayo ya siku mbili, mada kadhaa zilijadiliwa ikiwa ni pamoja na taratibu za upatikanaji wa fidia kwa wanaoanguka mikarafuu, kanuni na sheria ya maendeleo ya karafuu, haki za binadamu na majukumu ya wadau wa wazao la karafuu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.