Habari za Punde

Profesa Idris Akutana na Makamu wa Rais wa Taasisi ya CNRIFFI ya China.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                              21.09.2017
---
UHUSIANO na ushirikiano wa vyuo vya ndani na nje ya Zanzibar unaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa katika kuimarisha sekta ya elimu kwa vyuo vikuu vya Zanzibar kikiwemo Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).

Hayo yalielezwa na Makamo Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), Profesa Idris Ahmada Rai wakati alipokuwa akizungumza na  Makamo wa Rais wa Taasisi ya ‘China National Research Institute of Food and Fermentation Industries’ (CNRIFFI) Profesa Huang Yutong huko katika ofisi za chuo hicho Tunguu Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja.

Katika mazungumzo hayo, Profesa Rai alimueleza Makamo wa Rais wa Taasisi hiyo ya (CNRIFFI) ya nchini China kuwa  uhusiano na ushirikiano kati ya SUZA na Taasisi hiyo utasaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha mahusiano kati ya Zanzibar na China.

Alisema kuwa uhusiano huo utaweza kuimarisha zaidi azma ya kukuza sekta ya elimu hapa nchini sambamba na kuendeleza sekta nyengine muhimu za kimaendeleo ikiwemo sekta ya utalii.

Profesa Rai alitumia fursa hiyo kutoa pongezi na shukurani kwa Serikali ya China na kueleza kuwa nchi hiyo ina uhusiano na urafiki mwema na Zanzibar kwani tayari taasisi na vyuo vingi vikuu vya nchi hiyo vimeshaonesha azma ya kushirikiana na Chuo hicho cha Taifa cha Zanzibar hatua ambayo alisema inaleta matumaini makubwa katika kuimarisha sekta ya elimu nchini.

Aliongeza kuwa Chuo Kikuu cha SUZA kupitia Tawi lake la Chuo cha Utalii kilichopo Maruhubi kitahakikisha kinatoa mafunzo katika kada mbali mbali za utalii ikiwa ni pamoja na mafunzo juu ya mapishi, ukarimu na mengineyo kwa kutambua kuwa bado kuna mahitaji ya mafunzo hayo kwa wafanyakazi walio wengi hapa nchini hasa wale wanaoifanya kazi sekta ya utalii.

Pamoja na hayo, Profesa Rai alimpongeza Makamo huyo wa Rais wa Taasisi ya (CNRIFFI) kwa kuja Zanzibar yeye na wakufunzi wenye ujuzi mkubwa na kuitikia wito kwa vitendo wa kuja kutoa mafunzo kwa watendaji wa Serikali wanaotoa huduma za upishi na ukarimu kwa viongozi wakuu wa nchi pamoja na walimu kutoka Taasisi ya Utalii iliyopo Maruhubi.


Nae Makamo wa Rais wa Taasisi ya ‘China National Research Institute of Food and Fermentation Industries’ kutoka nchini China Huang Yutong alionesha kuvutiwa na mipango pamoja na mikakati ya Chuo Kikuu cha SUZA katika kutoa elimu hasa katika sekta hiyo ya utalii na kueleza kuwa taasisi yake iko tayari kushirikiana na SUZA katika azma kuendeleza utalii hapa nchini ambao tayari umeonesha kuimarika.

Kiongozi huyo aliongeza kuwa uhusiano na ushirikiano kati ya Taasisi hizo utaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa katika kufikia lengo la Serikali la kutoa mafunzo yatakayoinua sekta ya utalii.

Alieleza kuwa mafunzo ya mapishi, ukarimu na yale yote yanayohusiana na kada hiyo yanaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa katika kutoa elimu hiyo itakayosaidia kuimarisha sekta ya utalii na hata utamaduni wa hapa nchini.

Pamoja na hayo, Huang Yutong alieleza kuvutiwa kwake na aina ya vyakula mbali mbali vya Zanzibar na kusema kuwa iwapo mikakati maalum itawekwa katika kuvitangaza na kuvipa kipaumbele vyakula hivyo itakuwa ni kivutio chengine kikubwa cha utalii mbali ya kuweko vivutio kadhaa vikiwemo viuongo.

Huang Yutong alimuhakikishia Profesa Rai kuwa Taasisi ya (CNRIFFI) imekusudia kutoa mafunzo kwa wapishi wakuu ili waweze kuhudumia na kuwa na sifa za kutoa huduma za kitaifa na kimataifa.

Wakati huo huo, Huang Yutong alitembelea Taasisi ya Kilimo Kizimbani ambapo alipata maelezo kutoka kwa Mwalimu wa taasisi hiyo Foum Ali Garu nakumueleza kuhusu hatua zinazochukuliwa katika kuyaimarisha mazao ya viungo na umuhimu wake katika matumizi ya mwanaadamu sanjari na kuwa kivutio kimoja wapo kikubwa cha utalii.

Nae Profesa Yutong kwa upande wake ametoa shukurani kwa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kumuandalia ziara hiyo ya kutembelea Taasisi ya Kilimo Kizimbani pamoja na mashamba ya viungo  na kuweza kuna viungo hivyo kwa uhalisia.

Alisifu jitihada zinazochukuliwa na uongozi wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo ya Kizimbani kwa kuendelea kuvihifadhi viungo vilivyopo na kuweza kuwapa taaluma ya uhakika wageni wanaotembelea eneo hilo.

Sambamba na hayo,Makamo huyo wa Rais wa Taasisi ya (CNRIFFI)  inayohusiana na mambo ya mapishi na ukaribu ilichopo mjini Beijing nchini China,  ameahidi kuendelea kuziunga mkono jitihada zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kulitangaza eneo hilo lenye viungo vyenye thamani kubwa duniani.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.