Habari za Punde

Rais Dk Shein aipongeza Serikali ya Oman kwa kuendeleza uhusiano na ushirikiano mzuri uliopo



STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                13.10.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameipongeza Serikali ya Oman chini ya uongozi wa Sultan Qaboos bin Said kwa kuendeleza uhusiano na ushirikiano na Zanzibar na kueleza kuwa ujio wa meli ya Fulk Al Salamah kutoka Oman ni ishara upendo wa kihistoria kati ya pande mbili hizo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika mazungumzo kati yake na Waziri wa Mafuta na Gesi wa Oman Dk. Mohammed bin Hemed Al Ruhmi , Ikulu mjini Zanzibar ambaye yupo Zanzibar kwa ziara maalum ya kuendeleza uhusiano, umoja na upendo akiongoza ujumbe kutoka Serikali ya Oman ambao umefika nchini kwa kutumia usafiri wa meli maalum ya Sultan Qaboos iitwayo Fulk Al Salamah.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alimueleza Waziri Mohammed bin Hemed Al Ruhmi kuwa ujio wa kiongozi huyo pamoja na ujumbe wakiwemo mawaziri kutoka Serikali ya Oman kuja Zanzibar unaonesha jinsi nchi hiyo ilivyokuwa na dhamira ya dhati ya kuendeleza uhusiano na ushirikiano wa kihistoria kati yake na Zanzibar.

Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Oman imekuwa na uhusiano na ushirikiano mwema na Zanzibar na bado inaendelea kuiunga mkono katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo sekta ya afya, elimu na nyenginezo.

Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi za pekee kwa Sultan Qaboos kwa misaada yake mbali mbali ikiwa ni pamoja na msaada wa kujenga msikiti wa  Jaamiu Zinjibar, uliopo Mazizini mjini Zanzibar aliouzindua hivi karibuni ambao mbali na kutumika kwa ajili ya ibada pia, ni kituo cha kutoa mafunzo ya dini ya Kiislamu.

Dk. Shein alisema kuwa ujio wa ujumbe huo unaoongozwa na Waziri Dk. Mohammed bin Hamed Al Ruhmi kuja Zanzibar kwa kutumia usafiri wa meli ni kuonesha historia ya pekee ya watu wa Oman na Zanzibar jinsi walivyokuwa wakisafiri kwa kutumia majahazi kwa kufuata pepo za Kusi na Kaskazi wakati huo.



Nae Waziri Waziri wa Mafuta na Gesi wa Serikali ya Oman Dk. Mohammed bin Hamed Al Ruhmi ameeleza kuwa ujio wao una lengo la kufikisha salamu za mashirikiano, uhusiano na upendo kwa ndugu zao wa Zanzibar kutoka kwa Sultan Qaboos wa Oman.

Waziri Mohammed ambaye amefuatana na Kiongozi wa Taasisi ya Uwekezaji Dk. Salem bin Nasser Al Ismaily pamoja na Bi Maitha Al Mahrooqiya, Mshauri wa Waziri wa Utalii na Balozi Mdogo wa Oman anayefanya kazi zake hapa Zanzibar Dk. Ahmed Hamoud Al Habsy alieleza kuwa uwamuzi huo wa kuja Zanzibar ni uwamuzi wa kihistoria na kidugu kati ya pande mbili hizo.

Aliongeza kuwa watu wa Zanzibar wameonesha furaha kubwa kwa ndugu zao hao wa Oman waliofika kwa ajili ya kuwatembelea na kusifu pamoja na kupongeza mapokezi makubwa waliyoyapata wakati walipowasili hapa Zanzibar ikiwa ni nchi ya mwanzo kutembelewa na meli hiyo yenye kuchukuwa watu zaidi ya 300.

Pamoja na hayo, Waziri huyo alimueleza Dk. Shein haja ya kuendeleza na kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na Oman huku akiahidi kuwa Oman itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo.

Aidha, kiongozi huyo alimueleza Dk. Shein azma ya Serikali ya Oman chini ya uongozi wa Sultan Qaboos ya kujenga hospitali hapa Zanzibar sambamba na kulifanyia ukarabati jengo la Bait Al Ajab liliopo Forodhani mjini Unguja ambalo lina historia kubwa ya Zanzibar

Wakati huo huo, Dk. Shein alifanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtandaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mapango wa UKIMWI (UNAIDS)  na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Michel Sidibe, Ikulu mjini Zanzibar ambapo Mkurugenzi huyo alipongeza juhudi za Zanzibar katika kupambana na UKIMWI.

Katika maelezo yake Mkurugenzi huyo wa (UNAIDS), aliiopongeza Zanzibar katika juhudi zake za kupambana na UKIMWI na kueleza kuwa ni za kupigiwa mfano katika Bara la Afrika na duniani kwa jumla.

Aidha, alisisitiza kuwa mafanikio na juhudi hizo zimeweza kupatikana zaidi kutokana na uongozi, sifa, uzoefu na utaalamu alionao Dk. Shein katika suala zima la kupambana na UKIMWI, kwani juhudi hizo amezianza muda mrefu na kumfanya atambulike Kimataifa.

Pia, kiongozi huyo alieleza haja kwa nchi zinazoendelea zikiwemo nchi za Bara la Afrika kuweka mpango maalum wa kuhakikisha inaziimarisha sekta za Afya kwa kujiandaa na matukio yanayotokea hivi sasa ya kimisaada duniani.

Nae Dk. Shein  kwa upande wake alieleza juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kupambana na UKIMWI na kulipongeza Shirika hilo pamoja na mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika mapambano dhidi ya UKIMWI.

Dk. Shein alieleza kuwa mbali ya mafanikio yaliopatikana katika kupambana na UKIWMI pia, juhudi za makusudi zimechukuliwa na Serikali anayoiongoza na kuweza kufanikiwa kwa kiasi kikubwa katika kupunguza vifo vya akina mama na watoto.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.