Habari za Punde

Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano Tanzania Profesa Mbarawa : Asema Serikali Imedhamiria Kuondoa Msongamano Katika Jiji la Dar es Salaam.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa akipata maelezo kutoka kwa Mhandisi wa Miradi kutoka Ofisi ya Wakala wa Barabara Nchini  (TANROAD), Mhandisi Julius Ngusa kuhusu utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa barabara za kupunguza msongamano Jijini Dar es Saalam wakati uliotembelea mradi wa ujenzi wa Barabara ya Goba-Madale
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa akipata maelezo kutoka kwa Mhandisi wa Miradi kutoka Ofisi ya Wakala wa Barabara Nchini (TANROAD), Mhandisi Julius Ngusa kuhusu utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa barabara za kupunguza msongamano Jijini Dar es Saalam wakati uliotembelea mradi wa ujenzi wa Barabara ya Goba-Madale 

Mradi wa Ujenzi wa Barabara ya Goba-Madale yenye urefu wa kilometa 5 ukiwa unaendelea kama unavyonekana katika picha.

Na Thobias Robert, Maelezo Dar es Salaam. 
WAZIRI wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa ameiagiza Wakala wa Barabara nchini (TANROAD) kusimamia kwa karibu Kampuni za ukandarasi wa miradi ya awamu ya tatu ujenzi wa barabara za pembezoni mwa Jiji la Dar es Salaam inayokusudia kuondoa msongamano wa magari Jijini humo.

Aliyasema hayo leo Jijini Dar es Salaam wakati wa ziara yake ya kukagua miradi ya ujenzi wa Barabara za Kifuru-Msigani, Goba-Makongo, Goba-Madale zenye urefu wa Kilometa 14, na kueleza kuwa Serikali imedhamiria kuhakikisha kuwa tatizo la Msongamano katika Jiji la Dar es Salaam linakuwa historia.
Waziri Mbarawa anasema tangu mwaka 2008, Serikali ilianza utekelezaji wa Awamu tatu za miradi ya ujenzi wa Barabara tisa katika maeneo ya pembezoni Jiji la Dar es Salaam hatua iliyolenga kudhibiti na kukabiliana changamoto ya  msongamano wa magari na kuharakisha ukuaji wa biashara.
Kwa mujibu wa Waziri Mbarawa anasema Serikali imebuni mipango na mikakati mbalimbali ya kupunguza msongamano Jijini Dar es Salaam ikiwemo mradi wa mabasi wa haraka, ujenzi wa barabara za juu katika maeneo ya Tazara na Ubungo, hivyo aliwataka wananchi kuunga mkono juhudi hizo zinazofanywa na Serikali yao.
“Hadi sasa mradi wa Awamu ya kwanza tayari umekamilika, awamu ya pili ipo ukingoni na sasa tumeanza awamu ya tatu, nimewaagiza TANROAD kuhakikisha wanafanya kazi kwa masaa 24 kusimamia kiwango cha miradi ya barabara hizi ili ifikapo mwaka 2018 mradi huu uwe umekamilika” alisema Mbarawa.
Waziri Mbarawa alisema katika kutekeleza miradi hiyo, Serikali ilitenga kiasi cha Tsh. Bilioni 24 na hivyo aliitaka TANROAD kuhakikisha kuwa Wakandarasi wa miradi hiyo wanajenga barabara zenye viwango vinavyoendana na thamani halisi ya gharama zilizotumika.
Aidha Waziri Mbarawa alisema Serikali itaendelea kutoa kipaumbele kwa Wakandarasi wazalendo wanaotekeleza kwa viwango na ubora kwa miradi ya ujenzi nchini, hivyo alizitaka Kampuni zilizopewa miradi ya ujenzi wa barabara hizo za pembezoni mwa Jiji la Dar es Salaam kuzingatia maadili ya taaluma ya ujenzi.
Kwa upande wake, Mhandisi Miradi wa Ofisi ya TANROAD Mkoa wa Dar es Salaam, Julius Ngusa alisema utekelezaji wa ujenzi wa barabara za kupunguza msongamano Jijini Dar es Salaam ulianza mwaka 2008 ambapo hadi sasa mradi wa barabra tatu zenye urefu wa kilometa 19.4 tayari umekamilika.
Anasema kuwa barabara zilizokamilika katika awamu ya kwanza ni pamoja na Ubungo Bus Treminal-Kigogo-Barabara ya Kawawa iliyokamilika mwaka 2010 na kugharimu kiasi cha Tsh Bilioni 11.44, pamoja na barabara ya Kigogo Roundabout-Msimbazi Valley-Jangwani/Twiga yenye urefu wa kilometa 2.72 iliyogharimu kiasi cha Tsh. Bilioni 7.64.
Aidha Mhandisi Ngusa alisema awamu ya pili ya miradi hiyo iliyohusu ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilometa 27.5 na Daraja la Kinyerezi katika Mto Msimbazi lenye urefu wa mita 40 ujenzi wake tayari ulikamilika mwaka 2014.
Kuhusu Awamu ya tatu ya miradi ya ujenzi, alisema mradi wa barabara ya Kifuru-Msigani ujenzi wake unatarajia kukamilika mwezi Disemba 2016 mwaka huu, wakati ujenzi wa Barabara za Goba-Madale na Goba Makongo zinatarajia kukamilika mwanzoni na mwishoni mwa mwaka 2018.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.