Habari za Punde

Jizee la miaka 56 labaka kitoto cha miaka 9 Kangagani


NA ZUHURA JUMA, PEMBA

MOHAMED Bakar Mshindo (56) mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba, anatuhumiwa kumbaka mtoto wa miaka tisa, huko katika nyumba anayoishi Kangagani.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, wanafamilia wa mtoto huyo, Mjini ole Wilaya ya Chake Chake, walisema kuwa, mzee huyo alikuwa akimchukuwa mtoto wao skuli wakati wa mapunziko (rises), na kwenda naye nyumbani kwake kimfanyia udhalilishaji.

Walisema kuwa, ni zaidi ya miezi miwili tokea kuripoti tukio hilo kituo cha Polisi Mchangamdogo, ingawa hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa na kupelekea mtuhumiwa kupita mitaani na kujigamba kwamba yeye ni mwenye pesa na hawezi kutiwa hatiani.

Akielezea tukio hilo mlezi wa mtoto huyo (60) alisema kuwa, mtoto wake alitoka kwenda skuli na aliporudi akamuona hali yake sio ya kuridhisha, ambapo alimuuliza kama anaumwa ampeleke hospitali.

“Aliniambia anaumwa na jipu na ndipo nilipomwambia asiende skuli na nilimtafutia dawa ili ajipake, ingawa hali ilizidi na kuwa mbaya na kutaka kumpeleka hospitali kwa siku ya pili”, alisema mlezi huyo.

Alieleza kuwa, siku ya pili kabla ya kupeleka hospitali alikwenda mazikoni na kupewa taarifa na mwalimu wake wa darasa kwamba amekuwa na matumizi makubwa, jambo ambalo lilimshitua na kuanza kumpeleleza kwani yeye alikuwa akimpa si zaidi ya shilingi 200.

Kwa upande wake mama mdogo wa mtoto huyo (19) alieleza kuwa, walipomgundua mtoto wao siku aliyokwenda pwani na watoto wenzake kuvua kaure, ambapo hakuweza kuokota kutokana na maji chumvi kumuumiza sehemu alizoathirika.

“Aliporudi pwani hali yake ilikuwa mbaya hata kwenda alikuwa hawezi na ndipo tulipotumia nguvu kumuangalia, tukamuona kwamba tayari ameshaathirika”, alisema mama huyo.

Alieleza kuwa, walimuuliza aliyemfanyia kitendo hicho na kusema kuwa ni Muhamadi Bakar Mshindo mkaazi wa Kangagani, ambaye alikuwa akimchukuwa skuli wakati wa mapumziko na kwendanae, katika nyumba anayoishi na kumbaka.

Bibi wa mtoto huyo (40), alisema kuwa, baada ya kuwaeleza hivyo walikwenda kituo cha Polisi Mchangamdogo, ingawa hadi leo haijachukuliwa hatua yoyote ya kisheria kesi hiyo.

Nae mtoto (9) aliyefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, babu huyo alimfanyia kitendo hicho mara mbili na alikuwa akimfunga matambara ya mdomo, pamoja na kumuwekea panga kwa kumtishia ili asiseme.

“Alikuwa akinipa chipsi, pesa na akija skuli kunita wakati wa mapumziko (rises) mimi na mjukuu wake, lakini siku aliyonibaka alinivuta ndani na akaziba matambara na baadae mjukuu wake alikimbia”, alisema mtoto huyo.

Mratibu wa wanawake na watoto Shehia ya Kangagani Awena Salim Kombo alieleza kuwa, kesi hiyo ipo kwa muda mrefu sasa na imeshafikishwa kituo cha Polisi Mchangamdogo, ingawa hakuna chochote kilichoendelea zaidi ya mtuhumiwa kupita mitaani na kujigamba.

Sheha wa shehia ya Mjiniole Khamis Shaaban Hamad alieleza kuwa, pamoja na matukio ya udhalilishaji kutokea lakini wananchi wamehamasika kuyaripoti kupitia elimu waliyopatiwa na mradi wa kukuza usawa wa kijinsia na kuwawezesha wanawake GEWE.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba Haji Khamis Haji alisema kuwa, upelelezi wa kesi hiyo tayari umekamilika na tayari jalada lishapelekwa kwa Mkurugenzi wa mashitaka.

Kamanda huyo alisema kuwa tukio hilo liliripotiwa Kituo cha Polisi Mchanga mdogo Oktoba 13 mwaka huu, ingawa lilikaa mda mrefu kabla halijaripotiwa na kuwataka wanajamii kuripoti kuharakisha kuripoti matukio yanapotokea.


Jumla ya matukio manne yametokea ndani ya kipindi cha miezi miwili katika shehia sita zilizopata elimu kupitia mradi wa GEWE, juu ya kuviripoti vitendo vya udhalilishaji vinavyotokea katika jamii, ikiwemo Kangagani, Mjiniole, Mchangamdogo, Kinyikani, Kiungoni na Shengejuu Wilaya ya Wete.  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.