Habari za Punde

Mkuu wa Wilaya Chake Awataka Wananchi Kuripoti Vitendo Vya Udhalilishaji Polisi na Dawati la Mkono kwa Mkono.


Na.Hasina Khamis - Pemba.
WANANCHI wa Shehia ya Vitongoji ,wametakiwa kuacha tabia ya kuwaachia watoto kuzurura ovyo nyakati za usiku pamoja na kwenda kutizama televisheni ama kucheza gemu kwani vitendo hivyo vinachangia
udhalilishaji kwa watoto.



Hayo yaliyaelezwa na Mkuu wa Wilaya ya Chake Chake Pemba, Rashid Hadidi Rashid, kwenye mkutano na wananchi wa Jimbo la Vitongoji, alipokuwa akizungumza na wananchi hao kwenye Uwanja wa Skuli ya
Vitongoji.



Alisema vitendo vya  Udhalilishaji, imeongezeka katika Wilaya yake ambapo kesi mbali mbali zimeripotiwa kwenye vituo vya Polisi ,Dawati na Mkono kwa mkono Hospitali.

“Tabia ya kuwaacha watoto kuzurura usiku sio maadili mazuri kwa jamii,tunayoishi kwani kunachangia mtoto kushawishika na vitendo hivyo pale wanapotaka pesa ya kutumia au kuchezea gemu”,alieleza.

Mkuu huyo wa Wilaya, alisema ni vyema Jamii kutoa ushirikiano katika masuala ya udhalilishaji wa kijinsia na madawa ya kulevya kwa kuwafichua wanaofanya hivyo.

Alisema “suala la muhali tusilipe kipao mbele kwenye jamii yetu kwani tutakuwa tunamlinda adui wa watoto wetu ,ili tuweza kupambana na vitendo hivyo kwenye jamaii iliyotuzunguka ni lazima kuacha muhali”.

Wakati huo huo Mkuu huyo wa Wilaya,  alisema suala la wizi wa mifugo na mazao limekithiri katika maeneo ya Vitongoji hivyo aliwataka wananchi kushirikiana kupambana na wizi hao na kwenda kuripoti Polisi
pale wanapombaini muhalifu hiyo wa mazao yao.

Afisa wa Afya wa Wilaya, Kombo Omar Abdalla,  aliwatanabahisha wananchi hao kujikinga na maradhi ya mripuko ya kupindupindu na matumbo ya kuharisha kwa kusafisha eneo yaliyowazunguka na kuchimba
Choo .

“Katika kipindi hichi cha mvua ni wajibu kwa kila wananchi kutunza mazingira na kuhifadhi kinyesi pamoja na Pempasi za watoto, kutupa taka na kuchoma moto kwenye majaa ili kuepuka maradhi hayo”, alisema.

Mwajuma Ali Salim, mkaazi wa Vitongoji, alisema changamoto zinazowakabili ni kukosa dawa za kuulia wadudu kutoka Wizara ya Kilimo baada ya zao la njugu kuvamiwa na wadudu kwenye Mashamba hayo.

 Kwa upande wake ,Said Ali Burhani,  mkaazi wa Vikutani aliomba Wizara ya Mawasiliano Pemba, kuwaekea matuta katika Barabara ya Ole Kengeja kwani licha ya kutomalizika, lakini tayari ajali sita zimeshatokea na
mwengine kupoteza maisha.

Katika mkutano huo viongozi mbali mbali wa Serikali walihudhuria akiwemo, Mkurugenzi wa Baraza la Mji ,Nasor  Suleiman Zaharani,Daktari dhamana wa Wilaya ya Chake Chake  Muhammed Ali Jape ,kamati ya ulinzi
na usalama ya Wilaya na Ofisa wa Afya, Kombo Omar Abdalla kwa lengo la kusikiliza changamoto zinazowakabili za wananchi wa jimbo hilo .

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.