Habari za Punde

Rais Dk. Shein Azungumza na Wanamichezo wa Zanzibar. Katika Tamasha la Tano Uwanja wa Amaan leo.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa mazoezi ni kinga na tiba mbadala ya maradhi mbali mbali yanayoisumbua jamii katika maisha ya kila siku hivyo kufanya mazoezi kunapunguza uwezekano wa kupata maradhi.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hotuba yake aliyoitoa  katika maadhimisho ya siku ya mazoezi Kitaifa yaliyovishirikisha vikundi mbali mbali vya mazoezi kutoka Unguja, Pemba na Tanzania Bara pamoja na vikosi vya SMZ yaliyoanzia katika uwanja wa Tumbaku na kuishia katika uwanja wa Amaan mjini Zanzibar yaliosimamiwa na Chama Cha Mazoezi ya Viungo Zanzibar (ZABESA).

Viongozi mbali  mbali walishiriki katika maadhimisho hayo akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd pamoja na viongozi wengine wa Seriali na vyama vya siasa na wananchi ambapo katika maelezo yake Dk. Shein alisisitiza kuwa kufanya mazoezi kunasaidia kupunguza uzito wa mwili na kuwataka wananchi kufanya mazoezi na kutosubiri hadi wakaambiwa na daktari.

Dk. Shein aliwasisitiza wananchi kuzingatia usemi maarufu wa mabingwa wa lugha ya kiswahili kwamba “Tahadhari kabla ya athari” na “Kinga ni bora kuliko tiba”, hivyo alisisitiza ni vyema kila mmoja akajiwekea muda maalum wa kufanya mazoezi yanayolingana na afya na umri wake.

Pia, Dk. Shein alitangaza rasmin kuwa maadhimisho hayo ya Siku ya Mazoezi Kitaifa hapo mwakani yatafanyika Kisiwani Pemba huku akiitaka Wizara ya Habari,  Utalii, Utamaduni na Michezo kukitafutia ofisi Chama Cha Mazoezi ya Viungo Zanzibar (ZABESA) ili kiweze kufanya kazi zake kwa ufanisi zaidi.

Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kwa mara nyengine tena kuipongeza timu ya “Zanzibar Heroes” kwa kufikia hatua ambayo haijawahi kufikiwa tangu mwaka 1995, ilipopata ubingwa wa mashindano Kombe la  Chalenji la CECAFA huku akiahidi kuwa mashindano yajayo popote pale yatakapofanyika timu hiyo itachukua ubingwa.

Pia, alitoa pongezi kwa vijana wa “Zanzibar Sand Heroes”(Mashujaa wa Mpira wa Ufukweni) kwa kufika fainali na kuifunga timu ya Malawi magoli matatu kwa mawili na kuchukua kikombe cha mashindano hayo. Pia, aliyapongeza mashindano ya “ZBC Watoto Mapinduzi Cup” yanayozishirikisha timu za watoto kutoka Wilaya zote za Unguja na Pemba.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alieleza azma ya Serikali hadi kufikia mwaka 2020 kumaliza viwanja vitano katika Wilaya za Unguja na Pemba kikiwemo kiwanja cha Kitogani ambacho ujenzi wake unaendelea huku akieleza hatua nzuri za ujenzi zinazoendelea katika uwanja wa Mao Tse-Tung.

Akitoa maelezo juu ya Mashindano ya “Mapinduzi Cup” yanayoendelea, Dk. Shein aliitaka  Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo kupunguza fedha za viingilio katika mashidnano hayo yanayofanyika katika uwanja wa Amaan ili wananchi wote wapate kuyaona kwani mashindano hayo ni ya Serikali na sio ya ZFA bali wao ni wasimamizi tu, hivyo wananchi wanafursa ya kuyaangalia kwa fedha wanazozimudu.

Dk. Shein alieleza kuwa  mashindano ya “Mapinduzi Cup” hayana mbadala na kuwaeleza wale wote wanaobeza Mapinduzi wajue kuwa na wao wanabezwa kwani Mapinduzi yaliwagomboa watu wote na yamemnufaisha kila mtu na yataendelea kuwa Mapinduzi, hivyo wanaoendesha mashindano hayo ni vyema wakatambua hilo.

“Hatuna mbadala na Mapinduzi yetu, tutayaenzi Mapinduzi yetu tutayaendeleza Mapinduzi yetu, tutayaenzi Mapinduzi yetu na wale wote wanaoyabeza Mapinduzi yetu na sisi tunawabeza hivyo hivyo”,alisisitiza Dk. Shein.

Pia, Dk. Shein aliiagiza Wizara hiyo kufikiria eneo jipya la kuanzia mazoezi hayo hadi kuishia katika viwanja vya Mao Tse Tung huku akiitaka ZFA kufikiria kuanzisha mashindano ya ZFA yatakayofanyika kwa njia ya kutoana yaana ‘knock out” yatakayoandaliwa kwa kuzishrikisha timu za madaraja yote kama yalivyokuwa zamani na yanayofanyika kwenye nchi mbali mbali.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa licha ya mafanikio yanayoendelea kupatikana katika kuimarisha sekta ya michezo hapa nchini bado jitihada za ziada zinahitajika kwa ajili ya kuimarisha Ligi Kuu ya Mpira wa Miguu ya Zanzibar ligi yake imekosa msisimko kutokana na kutotangazwa katika vyombo vya habari.

Hivyo, aliiagiza Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo iuelekeze uongozi wa Gazeti la ‘Zanzibar Leo’ uandae utaratibu ili kila siku wasomaji wapate kuuona msimamo wa ligi kuu ya Zanzibar pamoja na kuchapisha orodha ya mechi zinazochezwa kwa wiki nzima, ili kuwavutia wananchi kwenda viwanjani.

Nae Waziri wa Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo Rashid Ali Juma alimpongeza Dk. Shein kwa kuendeleleza sekta ya michezo hapa nchini na juhudi zake katika kulifanikisha tamasha hilo na kutumia fursa hiyo kuwapongeza wale wote waliounga mkono na kufanikisha maadhimisho ya tamasha hilo la mwaka huu.

Mapema Kamishna wa Michezo Sharifa Khamis alisema kuwa huu ni mwaka wa tano tokea Dk. Shein ayatangaze rasmin maadhimisho ya siku hiyo ya Kitaifa ya michezo na tokea mwaka huo yamekuwa yakienda vizuri huku akimpongeza Dk. Shein kwa zawadi alizoizawadia timu na viongozi wa timu ya “Zanzibar Heroes”.

Katika risala yao nao Wafanya Mazoezi ya Viungo  walieleza kuwa kufanya mazoezi ni njia moja ya kukuza uchumi wa Taifa ikiwa ni pamoja na kupunguza kununua dawa na fedha hizo kuzielekeza kwenye kuiletea maendeleo nchi yao.

Sambamba na hayo, walimpongeza Rais Dk. Shein kwa juhudi zake za kuiinua Zanzibar  kimaendeleo hasa katika sekta ya michezo, elimu, afya, kilimo, mawasiliano na miundombinu pamoja na sekta nyenginezo huku kaulimbiu ya Tamasha hilo mwaka huu ikiwani “Fanya mazoezi kwa maendeleo yako na Taifa lako”.

Walieleza kuwa hivi sasa kumekuwa na taasisi mbali mbali ambazo kwa kuimarisha na kuhamasisha ufanyaji wa mazoezi wamekuwa wakihamasisha wafanyakazi wao kufanya mazoezi pamoja na kuwepo taasisi zinazofanya utaratibu wa kupima afya za wafanyakazi wao kwa kuwasogezea karibu huduma za upimaji wa afya.

Mapema Dk. Shein, alipokea maandamano ya vikundi vya mazoezi kutoka ndani na nje ya Zanzibar vilivyowashirikisha vijana, wazee, watoto, wanawake na wanaume pamoja na walemavu na kuonesha mazoezi mepesi kiwanjani hapo pamoja na mashindano kwa wenye uzito wa zaidi ya kilo mia moja na baadae alitoa vyeti maalum kwa vikundi vya mazoezi vilivyoshiriki Tamasha hilo huku Balozi Seif Ali Idd akitoa vyeti maalum kwa waliochangia kufanikisha Tamasha hilo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.