MKURUGENZI Baraza la mji
Wilaya ya Mkoani Kisiwani Pemba, amewataka wananchi wilayani humo kuendeleza na
kudumisha usafi wa mazingira yaliyowazunguka katika kipindi hichi cha
mvua, ili kujikinga na maradhi ya mripuko
yakiwemo kipindupindu na kuharisha.
Aliyasena hayo, alipokuwa
akizungumza na gazeti hili, huko ofisini kwake Mkoani kufuatia mvua za masika
zilizoanza kunyesha.
Alieleza katika kipindi
hichi cha mvua ni vyema wananchi wakawa makini katika kudumisha usafi wa
mazingira, kwani kutofanya hivyo inaweza kuwa sababu ya kupata maradhiya
kipindupindu ama kuharisha.
Alifahamisha kuwa wananchi
waache tabia ya kutupa taka ovyo na badala yake wayatumie madampo yaliyojengwa
na baraza la mji, ili mji uweze kuwa safi na wenye kupendeza.
"Kutupa taka ovyo
kunachangia kuleta maradhi ya mripuko lazima wananchi wawe makini na
waangalifu",alisema.
Alisema ni jambo la
kushangaza kwa wananchi kutoyatumia madampo hayo, wakati baraza la mji huo
limejenga kwa gharama ili kuweza kutumiwa kwa kutupia taka.
Akizungumzia kuhusu usafi
kwa wafanya biashara alisema hatomvumilia mfanya biashara yoyote atakayekwenda
kinyume na maagizo watakayopewa na Serikali kuhusiana na kudumisha usafi na
namna ya kuzihifadhi biashara zao.
Alisema kutodumisha usafi
katika biashara ya vyakula kuna uwezekano mkubwa wa kupata maambukizo ya
maradhi hayo, kwani wanaonunuwa biashara hizo ni watu wa maeneo tofauti.
"Biashara nazo
zinahitaji kuwekwa katika hali ya usafi kwani zikiwa na vimelea vya maradhi ya
kuharisha vinaenea kwa haraka na kusababisha janga kubwa katika nchi",alisema.
Kwa upande wao wananchi
Wilayani humo, walimuomba Mkurugenzi huyo kuendelea na mkakati wake wa kupitia
nyumba kwa nyumba kuangalia hali ya usafi wa mji huo kwani imechangia
kudumishwa usafi na muonekano wake unaridhisha .
Hivyo walisema kila mmoja
atakuwa mlinzi wa mwenzake kuhakikisha usafi unadumishwa ili wilaya hiyo iweze
kuwa salama na kuepukana na maradhi ya mripuko.
No comments:
Post a Comment