Habari za Punde

Wakala wa Ulinzi Zanzibar wajinadi kwa wawekezaji, wafanyabiashara

 Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Ulinzi Zanzibar  Luteni Kanali Jabir Hamza, akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi Kikwajuni mjini Zanzibar.
 Mwenyekiti wa Bodi ya Wakala wa Ulinzi Zanzibar Kanali Mstaafu Makame Mabrouk Hassan, akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi Kikwajuni mjini Zanzibar.

Waandishi kutoka  vyombo mbalimbali vya habari, wakifuatilia mazungumzo ya viongozi ya Wakala wa Ulinzi wa Serikali yaliyofanyika katika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi Kikwajuni mjini Zanzibar. (Picha na Miza Othman- MAELEZO)



Na  Ali Issa-MAELEZO

WAKALA wa Ulinzi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, umesema kuwa umeundwa kwa lengo la kutoa huduma bora za ulinzi zinazoendeshwa kisasa.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi, Mkurugenzi Mtendaji wa wakala huo Kanali Jabir Hamza, amesema serikali imechukua hatua hiyo baada ya kubaini kasoro zinazowapa mwanya wahalifu kuhujumu miradi katiia maeneo ya uwekezaji hasa utalii na mengine.

Kanali Hamza amesema kuwa, wakala huo ambao ni taasisi ya serikali upo kisheria, ukiwa umeanzishwa  chini ya kifungu cha sheria namba mbili ya mwaka 2015.

Alifahamisha kuwa, kuja kwa wakala huo ni njia iliyokusudiwa kutoa ulinzi kwa kutumia silaha za kijeshi na kuwahamasisha wamiliki wa kampuni na miradi kuondokana na ulinzi wa silaha za kienyeji kama marungu.

“Katika ulimwengu huu ambao wahalifu wanabuni mbinu mpya kila uchao, hatuwezi kuendelea kulinda kwa magongo kwani ulinzi wa aina hiyo hauna usalama kwa walinzi wala wanaolindiwa,” alisema.

Hata hivyo, Mkurugenzi huyo alisema wakala huo haukuja kwa nia ya kuzifuta kampuni binafsi zinazotoa huduma za ulinzi, bali upo kwa ajili ya kuzielekeza kampuni hizo kwa kutoa miongozo itakayozifanya zibadii mfumo wao wa ulinzi.

Aidha alisema, lengo la wakala huo ni kuepusha majanga ya kutekwa kwa walinzi wasiokuwa na silaha za kisasa wala ujuzi wa kupambana na wahalifu, hali inayosanabisha kuibiwa mali za wawekezaji na wafanyabiashara wengine, na hata kushambuliwa kwa silaha za moto na mapanga.
Alieleza matumaini yake kuwa, kampuni nyengine za ulinzi zina haki ya kutoa huduma, lakini wakala wake utaendelea kuwashajiisha wamiliki wa mali na miradi kutumia ulinzi wa uhakika kwa kuwa kazi hiyo inafanywa kibiashara na serikali inategemea mapato.

Mbali ya mapato, kwa serikali, Kanali Hamza alisema, fedha zinazopatikana pia zinasaidia kugharamia mahitaji mengine ya Jeshi la Kujenga Uchumi.

Kwa upande mwengine,  alisema kuundwa kwa wakala huo, kutasaidia kupunguza uhaba wa ajira kwani litatoa fursa kwa vijana hasa waliopata mafunzo kupitia Jeshi la Kujenga Uchumi, kuajiriwa na kwa wale waliofikia umri wa miaka 27 kupewa ajira za mkataba.

Nae Mwenyekiti wa Bodi ya Wakala huo Kanali mstaafu Makame Mbarouk Hassan, alisema kazi yao nyengine ni kuvipa elimu na miongozo vikundi vinavyoendesha ulinzi kwa njia ya doria.
Aidha, alisema kwa kuwa serikali inategemea zaidi sekta ya utalii kiuchumi ambapo mara kadhaa wageni wamekuwa wakishambuliwa, wakala huo ndio muarubaini wa kukomesha vitendo hivyo vinavyoitia doa Zanzibar.

Alitumia fursa ya mkutano huo na waandishi wa habari, kuomba ushirikiano wa kutosha kutoka kwa kampuni na watu binafsi akiwahakikishia kuwa huduma zao zinalindwa na mikataba iliyotengenezwa na wanasheria wa serikali

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.