MKE wa Rais wa Zanzibar
Mama Mwanamwema Shein amesema kuwa kuanzishwa kwa Chanjo mpya ya maradhi ya
Saratani ya Shingo ya Mlango wa Kizazi itatokomeza maradhi hayo kama
yalivyotokomezwa maradhi mengine hapa Zanzibar.
Mama Shein aliyasema
hayo leo huko Skuli ya Dunga iliyopo Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja katika
uzinduzi wa Chanjo mpya dhidi ya maradhi ya Saratani ya Shingo ya Mlango wa
Kizazi, hafla ambayo imehudhuriwa na viongozi pamoja na wananchi kutoka maeneo
mbali mbali.
Katika hotuba yake,
Mama Shein alisema kuwa ugonjwa wa ndui uliathiri watu wengi hapa Zanzibar na
kupelekea watu wengi kupoteza maisha na wengine kubaki na kovu mpaka kufa kwao
lakini kutokana na chanjo ugonjwa huo ulitokomezwa kabisa.
Aliongeza kuwa baadhi
ya maradhi kama shurua, pepo punda, donda koo, kifaduro pamoja na polio
yalikuwa yakiwasumbua watoto kwa kiasi kikubwa yamepungua kutokana na chanjo
ambapo hivi sasa maradhi ya polio yametokomezwa kabisa hapa Zanzibar.
Kwa hivyo, Mama Shein
alisema kuwa maradhi ya Saratani ya Shingo ya Mlango wa Kizazi nayo yanaweza
kutokomezwa kama yalivyotokomezwa maradhi hayo ukiwemo ugonjwa wa ndui.
Aidha, Mama Shein
alisema kuwa lengo la Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar kutoa huduma za chanjo ni kuokoa maisha ya wananchi
wakiwemo watoto, kwa maradhi ambayo yamethibitika kuwa yanaweza kuzuilika kwa
chanjo.
Hivyo Mama Shein
aliwashajiisha wanawake wenziwe kuwahamasisha vijana waendelee kujitokeza kwa
wingi kwenda kufanikisha zoezi hilo kwa manufaa yao binafsi, wazazi na nchi
nzima kwa jumla.
Zanzibar imeweza
kupunguza maambukizo ya maradhi ya Malaria ambapo hivi sasa kiwango cha
maambukizo kipo chini ya asilimia moja, hivyo anaamini kuwa uzinduzi wa chanjo
hiyo kwa Unguja na Pemba ni safari nyengine ya mafanikio ambayo wananchi wa
Zanzibar wameanza kwa kujiandaa vizuri.
“Tumuombe Mola wetu
atujaalie iwe safari ya salama na ya mafanikio, ili Zanzibar na Tanzania kwa
jumla iendelee kuwa mfano bora duniani katika kupambana na maradhi mbali mbali”
Juu ya hili mimi sina shaka kutokana na juhudi zinazofanywa na Serikali yetu
inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dk. Ali Mohamed Shein” ,alisema Mama Shein.
Aidha alisema kuwa
wakati jamii inahamasishwa kushiriki katika chanjo ni vyema ikaendelea
kutekeleza vyema mikakati na mipango iliyopo ya mapambano dhidi ya unyanyasaji
wa kijinsia na udhalilishaji wa wanawake na watoto.
Mama Shein alitoa
nasaha zake kwa jamii na kutaka itoe ushirikiano kwa vyombo vinavyohusika kwa
kuwaripotia watu wanaobainika kufanya vitendo vya aina hiyo ili sheria ichukue
mkondo wake.
Pamoja na hayo, Mama
Shein alitoa shukurani kwa uongozi wa Wizara ya Afya na wahusika wengine
waliofanikisha hafla hiyo sambamba na kulishukuru Shirika la Kimataifa
linaloshughulikia Huduma za Chanjo (GAV), Shirika la Afya Duniani (WHO) na
Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) kwa michango yao mbali
mbali katika kuhakikisha wananchi wa Zanzibar wanapatiwa huduma za chanjo
zilizo katika kiwango cha ubora kabisa.
Nae Waziri wa Afya Hamad
Rashid Mohamed alitoa pongezi kwa Mashirika ya Umoja wa Mataifa kwa kuiunga
mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya yakiwemo UNFPA, UNICEF na WHO
hasa kwa kutambua kuwa chanjo hiyo ni muhimu sana.
Alisema kuwa kazi
iliyoko mbele ni kujenga Taifa ambalo lenye afya hivyo alisisitiza haja ya
kumtunza mama hasa katika wakati wa ujauzito hadi pale anapozaa kwa kumpa
msaada mapenzi na huruma huku akisisitiza matumizi mazuri ya lugha kwa akina
mama hao.
Waziri Rashid alisema
kuwa Zanzibar imepata mafanikio makubwa kutokana na uchumi wa Zanzibar kukua
kwa asilimia 7.5 na kuondokana na
utegemezi kutoka asilimia 31 hadi 7 hivi sasa licha ya baadhi ya wanasiasa kufanya
kampeni nje ya nchi ili Zanzibar isisaidiwe huku akieleza kuwa hivi sasa kila mfanyakazi
wa sekta ya umma amekuwa akipata mshahara si zaidi ya tarehe 25 baada ya nyongeza
ya mshahara huo.
Aliongeza kuwa utafiti
umefanywa kwa miaka mitano na chanjo hiyo haina tatizo na kuwataka wananchi
kuachana na wale wanaosambaza uzushi kuwa chanjo hiyo inawazuia watu kuzaa na
kusisitiza kuwa huo ni uzushi na hakuna haja ya kwenda kwa waganga na badala
yake waendelee kupata chanjo hiyo na kusisitiza matumizi ya lugha nzuri kwa
akina mama kutoka kwa wafanyakazi wa sekta ya afya.
Nae Mwakilishi wa
Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia masuala ya Idadi ya Watu Duniani
(UNFPA) Batula Abdia kwa niaba ya
Mashirika ya Umoja huo aliahidi kuimarisha mashirikiano na Wizara ya Afya
katika kupambana na maradhi mbali mbali huku akisisitiza haja ya jamii
kuelimishwa.
Aliongeza kuwa
saratani ya Shingo ya Mlango wa Kizazi ni saratani ya pili kwa ukumbwa
inayoisumbua jamii ulimwenguni ambapo inakisiwa wanawake wapatao 270,000
wanakufa kila mwaka duniani ambapo asilimia 88 ya wanawake hao wanaishi
katika nchi masikini kama Zanzibar na
kusisitiza kuwa chanjo hiyo ni muhimu sana na uwekezaji bora kwa Zanzibar.
Mapema Mkurugenzi wa
Kinga na Elimu ya Afya, Dk. Mohamed Dahoma akitoa maelezo ya kitaalamu alisema
kuwa chanjo hiyo ina madhumuni ya kusaidia kupambana na kasi ya uendeleaji wa maradhi ya saratani ya shingo ya mlango wa
kizazi.
Aliongeza kuwa maradhi
hayo yanayosababishwa na virusi kwa njia ya kujamiiana ambapo kwa asilimia 70
ya watu duniani wanatembea wakiwa na virusi hivyo kwa wanawake na wanaume
ambapo wapo wanaoonesha dalili na wasioonesha dalili na uzuri wake ni kuwa
virusi hivyo tayari vimepatiwa chanjo.
Alisema kuwa kwa hapa
Unguja saratani hiyo ni miongoni mwa saratani mbili zinazoongoza ikiwemo
saratani hiyo ya shingo ya mlango wa kizazi na ile ya matiti na kusema kuwa
vijana watakaochanjwa ni wale wa kuanzia miaka 14 ambapo mwaka huu watachanjwa vijana
20815 kupitia skuli na katika vituo wakiwemo na wale kutoka mitaani.
Serikali kupitia kwa
Wizara ya Afya imefanya mikakati mingi sana kuleta chanjo tangu mwaka 1981 ambapo
vituo vyote 175 vilivyopo Zanzibar vitaendelea kutoa chanjo na hivi sasa chanjo
zimeongezeka ikiwemo, kuharisha, kichomi,homa ya ini, uti wa mgongo ambapo
lengo kuu ni kutoa kinga kwa watoto ambao wengi wao wanazaliwa wakiwa hawawezi
kupambana na maradhi.
Alisema kuwa Kimataifa
zoezi hilo litaanza tarehe 23 hadi 26 Aprili ambapo Wizara ya Afya kwa hapa
Zanzibar itaendelea kushajiisha na kuielimisha jamii ili watu wote wawe na
uwelewa wa chanjo hiyo hadi muda huo utakapofika ambapo wanaamini kuwa wananchi
watakuwa wamepata uwelewa mzuri huku akieleza
kuwa ujumbe mkuu wa chanjo hiyo ni “Jamii iliyochanjwa ni jamii yenye afya”.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment