Habari za Punde

Uchumi wa Zanzibar Umeendelea Kuimarika Kutokana na Uongozi wa Thabiti wa CCM.-Dk. Shein.


MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa uchumi wa Zanzibar umeendelea kuimarika kutokana na uongozi thabiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) huku akisisitiza kuwa hatokuwa na msamaha kwa yeyote atakaebainika kufanya ubadhirifu wa fedha za umma.

Dk. Shein ambaye pia, ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi aliyasema hayo katika ukumbi wa ‘Jamhuri Hall’  huko Wete wakati alipokuwa akizungumza na Mabalozi wa Wilaya ya Wete katika Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Aliongeza kuwa uchumi wa Zanzibar umezidi kuimarika kwa kiasi kikubwa na kutumia fursa hiyo kuendelea kusisitiza kauli yake aliyoitoa katika maadhimisho ya kilele cha Mei Mosi mwaka huu kwa wale wote wanaodiriki kufanya ubadhirifu wa fedha za umma.

Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alieleza jinsi Zanzibar ilivyokuwa na uwezo mkubwa wa kifedha na uchumi hatua iliyompelekea kuongeza mishahara mara nne katika uongozi wake sambamba na kuimarikaka kwa sekta za maendeleo.

Dk. Shein aliendelea kusisitiza kauli yake kuwa ataendelea kuiongoza Zanzibar kwa uadilifu mkubwa na kusisitiza kuwa viongozi wote walioteuliwa wanatekeleza Ilani ya CCM.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein aliwaeleza viongozi hao kuwa ujenzi wa Chuo cha amali cha Daya-Mtambwe utaanza hivi karibuni pamoja na ujenzi wa barabara ya Finya-Kicha itakayojengwa kwa kiwango cha lami sambamba na kuzitafutia ufumbuzi changamoto nyengine walizoziorodhesha.

Akiwaeleza wajibu wao kwa mujibu wa Katiba ya CCM, Dk. Shein aliwaeleza viongozi hao wajijue kuwa wao ni Wenezi na Wahamasishaji wakuu wa CCM pamoja na kuwa na wajibu wa kuwaeleza wanachama katika maamuzi yote ya CCM na kufikisha mapendekezo ya wanachama katika vikao vya juu.

Alisema kuwa WanaCCM wote wakiwemo viongozi hao wana kazi kubwa ya kufanya katika kusaidia ushindi wa CCM na kila mmoja kwa ngazi yake kwa namna yake na kuwa na wajibu wa kufanya yeye mwenyewe kwa uwezo wake kusaidia ushindi huo.

Aidha, alisisitiza kuwa ushindi kwa CCM ni suala la lazima kutokana na maelekezo ya Katiba ya chama hicho na hakuna mbadala wa ushindi kwa kufuata taratibu na namna zote za kidemokrasi kwa  lengo la kuyalinda Mapinduzi ya Januari 12,1964 pamoja na Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Alisisitiza haja ya kupambana na udhalilishaji wa kijinsia kwa watoto na wanawake na kuwataka wananchi wote kuzingatia maadili ya Kizanzibari.

Aliongeza kuwa Zanzibar imeimarika kwa kiasi kikubwa na sio ile ya mwaka 1964 na imebadilika kwa kila hali sambamba na kuongezeka kwa idadi ya watu hali iliyotokana na kuwepo kwa amani na utulivu pamoja na chakula cha kutosha kwa watu wake.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Abdalla Juma Mabodi alieleza kuwa  ziara ya Dk. Shein ya kukutana na Mabalozi wote wa Zanzibar ni shemu ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM huku akitumia fursa hiyo kueleza umuhimu wa Mabalozi, Mashina na Matawi yake.

Naibu Katibu Mkuu huyo wa CCM Zanzibar pia, alitumia fursa hiyo kueleza jinsi ya hatua mbali mbali zinazochukuliwa na Chama hicho kupitia Mabaalozi wake na kusisitiza azma walyokusudia ya kuwafuatilia Wawakilishi ni kwa vipi wanazitumia fedha za mfuko wa Jimbo.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Pemba Mberwa Hamad Mberwa alieleza juhudi kubwa zinazochukuliwa na Mabalozi hao pamoja na viongozi wote wa Chama hicho katika Wilaya ya Wete.

Katika risala ya Mabalozi wa Wilaya ya Wete iliyosomwa na Balozi Ali Khamis Ali  ilieleza utekelezaji wa Ilani ni wenye mafanikio makubwa hasa kwenye maeneo ya huduma za jamii kama vile Maji safi na salama, Afya, Elimu, Miundo mbinu, Biashara, Viwanda pamoja na sekta nyenginezo.

Aidha, walitoa shukurani zao na kumpongeza sana kwa kushirikisns nso kstiks uzinduzi wa umeme katika Kisiwa cha Fundo.

Sambamba na hayo, Mabalozi hao wamempongeza Dk. Shein kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi asilimia mia moja katika Mkutano Mkuu wa CCM Taifauliofanyika mwishoni mwa mwaka 2017.

Pia, Mabalozi hao walimuomba Dk. Shein kuwapelekea salamu zao kwa Mwenyekiti wa CCM Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Pombe Magufuli kwa kuchaguliwa kwa asilimiamia moja katika Mkutano Mkuu wa CCM Taifa na kumpongeza kwa kazi nzuri anayofanya.

Dk. Shein amemaliza ziara yake ya kukutana na Mabalozi wa Wilaya zote za Kisiwani Pemba ambapo kuanzia kesho anatarajiwa kuendelea na ziara zake za kukutana na Mabalozi wa Wilaya za Unguja ambapo pia, katika ziara hiyo Mama Mwanamwema Shein alishiriki kikamilifu.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.