Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein Alihutubia Baraza la Eid El Fitry Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapnduzi Dk. Ali Mohamed Shein, akiwahutubia Waislam katika Ukumbi wa Sheikh.Idrisa Abdulwakil Kikwajuni Zanzibar wakati wa Baraza la Eid El Fitry, baada ya kumaliza Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan, 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein amewataka wananchi kuzingatia suala la kuendeleza malezi bora ya watoto kwa mujibu wa maadili, silka na utamaduni ulioachwa na wazee.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hotuba yake ya Baraza la Idd al Fitri aliyoitoa huko katika ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdul Wakil, Kikwajuni Mjini Zanzibar, ambapo hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein na viongozi wengine wastaafu.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alisema kuwa hivi sasa malezi yamekuwa yana mtihani kwani kila mzazi amekuwa akiishi na mwanawe wakati hapo zamani watoto hulelewa na kiambo au mtaa mzima na kila mzee katika mtaa alikuwa ni mzee wa watoto wote na walitakiwa wamuheshimu na wamtii.

Alhaj Dk. Shein alisema kuwa utamaduni huo ulisaidia sana watu kuheshimiana na kuwapa usalama watoto katika mitaa, hata pale wazazi wao wanapokuwa hawapo.

Kwa hivyo, Alhaj Dk. Shein alieleza kuwa wazazi na walimu wana wajibu wa kushirikiana katika kuhakikisha kwamba jamii inapata mustakabali mwema.

Alieleza kuwa miongoni mwa jitihada za kuhakikisha kwamba wananchi wanatimiza wajibu wao katika kuzingatia mpango wa miaka mitano wa kupambana na unyanyasaji na udhalilishaji wa kijinsia wazazi na walezi wote inawalazimu kuongeza nguvu na kushirikiana katika malezi ya watoto wao.

“Ili tuweze kushinda vita vya unyanyasaji na udhalilishaji wa kijinsia, lazima kila mmoja wetu atimize wajibu wake kwa kuzingatia mpango wa miaka mitano wa kupambana na unyanyasaji na udhalilishaji wa kijinsia ambao tuliuzindua mwezi wa Agosti mwaka 2017…naiagiza Wizara ya Kazi, uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto kulishaughulikia suala hilo”,alisema Dk. Shein.  

Aidha, alilitaka Jeshi la Polisi, Ofisi ya Makurugenzi wa Mshtaka na Mahakama nazo kuendelea kuyatekeleza majukumu yao vizuri ili kesi za udhalilishaji na unyanyasaji wa kijinsia ziweze kusikilizwa kwa haraka.

Dk. Shein aliwaasa wazazi na walezi kwamba linapotokezea kosa la udhalilishaji ambalo limefanywa na mtu wa familia, hawapaswi kulitolea hukumu na kulimaliza kifamilia kwani wanapoamua hivyo wanadhoofisha jitihada za Serikali na kuyaendeleza maovu.

Aliongeza kuwa katika jitihada za kuwajengea watoto misingi imara ya maisha yao ya baadae ni kuimarisha ustawi wao na kuwaandaa kuwa raia wema wenye elimu, maarifa na uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya karne ya 21.

Rais Dk. Shein alieleza hatua zilizochukuliwa na Serikali anayoiongoza katika kuhakikisha elimu ya msingi na sekondari inatolewa bure kwa lengo la kutekeleza dhamira ya Mapinduzi matukufu ya 1964 kwa misingi iliyoasisiwa na Marehemu Mzee Abeid Karume.

Alieleza kuwa katika kuona kuwa watoto hasa wa Skuli za Sekondari wanapata mazingira mazuri ya kusoma, Serikali imeiagiza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali ilifanyie kazi suala la kuziendeleza huduma za dakhalia kwa ukamilifu.

Dk. Shein aliwahakikishia wananchi kuwa Serikali itahakikisha kwamba huduma za dakhalia zinaendelezwa na zinafanikiwa kwani huduma hizo mbali ya kuwapa wanafunzi muda mzuri wanapata utulivu wa kushughulikia masomo yao na wazazi wanapata utulivu kwa kujua kwamba watoto wao wanaishi katika mazingira salama.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein aliwataka wafanyakazi wenzake walioko katika ajira kuwa ni wajibu kuithamini na kuishukuru neema ya kupata ajira kwa kutekeleza dhamira na majukumu yao kwa misingi ya uadilifu.

Aliwataka kuzilinda na kuziheshimu mali za umma na sehemu zao za kazi huku wakitambua kwamba wenzao hivi sasa wana mahitaji ya kutaka kufanya kazi, ili wawe wafanyakazi kama wao lakini bado hawajapata nafasi ya kuajiriwa.

Alitoa pongezi kwa wananchi kwa kuzingatia maelekezo ya wataalamu wa afya katika kukabiliana na kujikinga na maradhi ya miripuko na kudumisha usafi huku akieleza jinsi Serikali ilivyoongeza bajeti ya afya ya TZS bilioni 12.7 kwa mwaka 2018/2019  kutoka TZS bilioni 7.0 za mwaka 2017/2018 sawa na ongezeko la asilimia 81.4.

Pia, alitumia fursa hiyo kuwataka wafanyakazi kuyaendeleza mafunzo ya Ramadhani kwa kuendelea kuwa wakweli, waadilifu, wastahamilifu na kuwa wakinaifu huku Serikali yao ikiendelea kuwachukulia hatua wale wote wanaoendelea na vitendo vya rushwa, ubadhirifu wa mali za umma na wanaoshindwa kusimamia dhamana walizopewa.

Mapema, Alhaj Dk. Shein aliungana na wananchi katika Sala ya Idd-El-Fitri huko Katika viwanja vya Maisara Suleiman mjini Zanzibar ambapo viongozi mbali mbali walihudhuria katika ibada hiyo, huku waislamu wakitakiwa kuwa wachamungu na kuyatumia vyema mafunzo ya Ramadhan.

Wakati huo huo, Rais Dk. Shein aliungana na viongozi, Masheikh na Maulamaa waliofika Ikulu Mjini Zanzibar kwa ajili ya kusalimiana na kutakiana kheri ya Sikukuu ya Idd el Fitr ambapo Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza haja ya kuendeleza umoja na mshikano.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alitoa mkono wa Idd kwa wananchi wote waliofika katika viwanja vya Ikulu ya Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.